Saturday, July 12, 2014

KIFO CHA DAUD BALALI SASA WAZI,SOMA HAPA


Mkazi wa Kijiji la Luganga, Wilaya ya Mufindi, Iringa, alikozaliwa Gavana wa zamani wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Daudi Ballali analazimika kutumia saa 32 kufika katika kaburi la kiongozi huyo lililopo eneo la Silver Spring, Maryland nchini Marekani.
Ndugu wa Ballali (pichani) wanaweza kutaka kwenda kuona kaburi la ndugu yao, kutokana na ukweli kwamba wengi wao hawakuwahi kupata fursa ya kumzika Gavana huyo ambaye alikuwa kiongozi wa juu kabisa wa taasisi kubwa inayosimamia masuala ya fedha na uchumi wa nchi.
Mwandishi wa gazeti hili alisafiri kwa saa 24 kutoka Dar es Salaam hadi Washington, Marekani ambako alithibitisha pasi na shaka kwamba Ballali alizikwa Mei 21, 2008 katika makaburi ya Gate of Heaven, baada ya kufariki dunia akiwa nyumbani kwake Maryland, Mei 16, mwaka huo.
Safari hiyo ya siku kumi, ilianza Alhamisi Juni 26, 2014 hadi Jumapili, Julai 6. Mwandishi wa habari hizi aliligundua kaburi hilo baada ya kwenda makaburi ya Gate of Heaven kwa siku tatu mfululizo.

Siku ya kwanza, mwenyeji wa mwandishi ambaye jina lake tunalihifadhi kwa sasa alimfikisha katika makaburi hayo, lakini kaburi la Ballali halikuonekana na hata mwandishi alipokwenda siku ya pili peke yake, kaburi hilo pia halikuonekana kwa kutokana na ukubwa wa eneo hilo.
Siku ya tatu, Mwandishi wa Mwananchi alilazimika kuomba msaada wa Ofisi ya Makaburi ya Gate of Heaven, ambayo ilimsadia kuonyesha eneo lilipo kaburi hilo, hivyo kuwezesha kupata picha zake.
Kaburi lake liko katika msitari wa mwisho kabisa na Ukanda wa Kijani wa miti iliyozunguka makaburi ya Gate of Heaven, likiwa limeandikwa jina la kiongozi huyo, pamoja na maneno ya Kiingereza yanayosomeka
“When the heart weep for what it has lost, the soul rejoices for what it has found”.
Maana ya maneno hayo ni kwamba “wakati moyo ukiomboleza kwa kile kilichopotea, roho hufurahi kwa kile kilichopatikana”. Kaburi hili limezungukwa na makaburi mengine kadhaa ambayo si ya Watanzania, kwani kwa haraka kutokana na mazingira yalivyokuwa, Mwandishi wa
Mwananchi hakuweza kuona kaburi jingine lenye majina yenye asili au kuwa na mwelekeo wa asili ya Tanzania.
Uthibitisho huu ni tofauti na hekaya za miaka nenda rudi zilizogubika kifo cha kiongozi huyo, ambaye tangu alipoondoka nchini kwenda Marekani Agosti 2007, hakuwahi kurejea na badala yake zilisikika taarifa za kuugua kwake, kifo chake na baadaye mazishi yake yaliyokuwa ya siri kubwa yakiwahusisha ndugu wa karibu pekee.
Kutokana na mazingira hayo, kumekuwapo na uvumi kwamba Ballali hakufa na pengine amefichwa kusikojulikana, madai yanayochagizwa na mtu aliyejitokeza katika mitandao wa kijamii ya Twitter na facebook, akidai kwamba yeye ni Ballali na kwamba hajafa, huku akisisitiza kuwa wakati ukiwadia ukweli utafahamika.
Mtu huyo asiyefahamika hadi sasa alianza kujitokeza Twitter, Oktoba Mosi, 2012 pale aliposema “Nitakutana na Rais Kikwete (Jakaya) na ujumbe wake wiki hii hapa Marekani”.
Mtu huyo alidai kwamba alikuja nchini Tanzania na kukaa karibu na Hoteli ya Hyatt Kempinski Kilimanjaro na baadaye kuondoka ghafla kwa kile alichokiita sababu za kiusalama.
Novemba 13 mwaka huo alituma ujumbe akisema:“In Dar es Salaam, Hyatt Regency Dar es Salaam, The Kempinski Kilimanjaro Hotel. Feels good to be close to my former office, BoT,” akimaanisha kwamba niko Hoteli ya Hyatt Regency Dar es Salaam, najisikia vizuri kuwa karibu na ofisi yangu ya zamani BoT.
Mtu huyo ambaye sasa tunaweza kuthibitisha kuwa ni feki amekuwa akiendelea kutuma ujumbe akijitambulisha kwa jina hilo la Ballali.
Ballali alifariki dunia kama ilivyotagazwa, lakini ilikuwaje akaenda safarini Washington, ugonjwa wake na hata kifo chake kilikuwaje? Je ndugu zake wanasemaje, safari ya kwenda Marekani ilikuwaje? Fuatilia mfululizo wa habari hii itakapoendelea kesho.
Chanzo: Mwananchi

No comments: