Monday, July 14, 2014

WAZIRI NYALANDU SASA NGOMA NZITOI--GMS WATISHIA KUMPANDISHA KIZIMBANI

Kampuni ya Uwindaji ya Green Miles Ltd (GMS) iliyofutiwa leseni ya uwindaji imemuweka njia panda Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, baada ya kupinga uamuzi huo uliochukuliwa na waziri huyo na sasa imepanga kwenda mahakamani kudai haki kisheria. 
Waziri Nyalandu alitangaza kuifutia leseni ya uwindaji nchini pamoja na shughuli za utalii kampuni hiyo kwa madai ya kukiuka sheria mbalimbali za uwindaji wanyamapori Julai 11, mwaka huu.
 
Mwanasheria wa kampuni hiyo, ambaye ni Wakili wa kampuni ya Uwakili ya Haki Kwanza, Alloyce Komba, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, alisema GMS itakwenda mahakamani kama viongozi wa juu wa serikali 

watashindwa kushughulikia tatizo hilo. 


      “Iwapo mamlaka za juu za serikali hazitashughulikia jambo hili ili haki itendeke, kampuni ya GMS italazimika kwenda mahakamani kudai haki ya kurejeshewa leseni zake pamoja na kudai kulipwa fidia kutokana na hasara iliyopata baada ya 
kushindwa kufanya biashara,” alisema. 

       Alisema uamuzi huo utafikiwa baada ya kuandika barua kwenda kwa viongozi wa juu wa serikali kwa maana ya Waziri Mkuu na Katibu Mkuu Kiongozi, kwani kampuni inaamini kwamba, Waziri Nyalandu ametekeleza hilo ili kutekeleza lengo lake ovu ili aweze kukigawa kwa rafiki zake. 
Komba alisema ni jambo la kusikitisha kwamba, licha ya kampuni hiyo kufanya uwekezaji mkubwa na kulipa ada zote za serikali, imejikuta ikihujumiwa na waziri aliyepewa dhamana ya kusimamia sekta ya maliasili ya utalii kwa ajili ya kulinda maslahi ya kampuni ya kigeni.
 


         Alisema kampuni ya GMS haikupewa nafasi ya kujitetea na badala yake Waziri Nyalandu aliamua kutoa maamuzi ya kuifutia leseni na siku chache baada ya kufanya hivyo ameondoka nchini na kwenda Marekani ambako yapo makao makuu ya kampuni moja ambayo ina mgogoro na kampuni ya GMS. 


       Julai 11 mwaka huu, Waziri Nyalandu alisitisha kibali cha umiliki wa kitalu kwa kampuni hiyo kufuatia madai ya uwindaji usiozingatia sheria ya uhifadhi wa wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009 kama ambavyo pia ushahidi huo ulielezwa kuthibitishwa kupitia DVD hiyo.

No comments: