Friday, December 5, 2014

ZITTO ATOA SHARTI MOJA ILI AREJEE CHADEMA,SOMA HAPA

Harufu ya kuisha kwa mgogoro baina ya Zitto Kabwe na chama chake cha Chadema inanukia, lakini mbunge huyo wa Kigoma Kaskazini anataka kuwapo na mazungumzo kubaini tatizo ili atakayebainika kuwa alifanya makosa awe tayari kuomba radhi hadharani.
Zitto alikiri bungeni kuwa amekuwa “akimiss” harakati zilizokuwa zikifanywa na vyama vya upinzani wakati wa Bunge Maalumu la Katiba, harakati zilizozaa Umoja wa Katiba ya Wananchi na kufurahia kuhudhuria kwa mara ya kwanza vikao vya umoja huo.
Zitto, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), alipata fursa ya kuingia vikao vya Ukawa wakati wapinzani walipoungana tena kupambana dhidi ya wizi wa fedha kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow, sakata ambalo liliwekwa bayana na kamati yake baada ya Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila kulifikisha bungeni, lakini hakudokeza lolote kuhusu Chadema.
Hata hivyo, mapema wiki hii, Zitto, ambaye Novemba mwaka jana alivuliwa nyadhifa zote kwenye chama hicho kwa tuhuma za kukihujumu, lakini akafanikiwa kulinda uanachama wake baada ya kufungua kesi mahakamani na kufanikiwa kupata amri ya kuzuia asijadiliwe.
Baada ya kuongoza PAC kuchunguza wa tuhuma za Escrow na kufanikiwa kulishawishi Bunge kufikia maazimio manane ya kuwashughulikia kisheria wahusika kwenye uchotwaji huo wa fedha, kumekuwapo na wito kutoka kwa baadhi ya wafuasi wa Chadema kutaka pande hizo mbili zimalizane.
“Kabla ya jambo lolote kufanyika, ili kukata kiu ya Watanzania wanaotaka kuona tunaondoa tofauti zetu, ni lazima kusema ukweli na kila upande kuwa tayari kuomba radhi hadharani pindi ikibainika ulifanya makosa,” alisema Zitto alipotakiwa kuzungumzia harakati hizo za kumrejesha Chadema.
“Ukweli wangu ndani ya Chadema ni nini? Lakini mimi ninaona sina kosa ndani ya Chadema. Ninachotaka mimi nielezwe ukweli bila chembe ya shaka makosa yangu mimi ni nini,” alisema na kuongeza:
“Nitakuwa tayari kuomba radhi hadharani kama ikibainika nilifanya makosa na kama ikibainika chama kilifanya makosa, nacho kiwe tayari kuomba radhi hadharani na ukweli uwe mbele katika maridhiano.
“Kama hakutakuwa na ukweli itakuwa vigumu kupata mwafaka. Mimi sina tatizo. Nirudie nilivyosema bungeni kuwa nina-miss sana (ninapenda sana kuwamo kwenye) harakati za mageuzi kipindi hiki za kuiondoa CCM madarakani.”
Katika mkutano na waandishi wa habari mara baada ya kuvuliwa nyadhifa zote, Zitto alisema: “Natambua kuwa wapo ambao wangependa kutumia nafasi zao kudhoofisha mapambano ya siasa za demokrasia nchini mwetu. Napenda wanachama wa Chadema na wapenda demokrasia watambue kuwa, mimi bado ni mwanachama mwaminifu wa chama hiki.
“Kinachoendelea ndani ya chama chetu ni mapambano ya kukuza demokrasia. Ni mapambano baina ya wapenda demokrasia dhidi ya wahafidhina; waumini wa uwajibikaji dhidi ya wabadhirifu; na wapenda siasa safi dhidi ya watukuzao siasa majitaka.”
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, ambaye binafsi aliguswa na mzozo huo, hakuwa tayari kuzungumzia kumaliza matatizo baina ya chama na Zitto.
No comment (sina maoni) kwa hilo. Siwezi kuzungumzia suala hili katika media (vyombo vya habari),” alisema Mbowe
Hoja ya kutaka Zitto arejeshwe Chadema imekuwa ikisambaa katika mitandao ya kijamii na kwa baadhi ya wanasiasa baada ya kuonekana kuwa karibu na viongozi wa chama chake wakati Kamati ya PAC ilipoibua ufisadi wa Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow wiki iliyopita.
Wakati akihitimisha mjadala wa sakata la Escrow, mbali na kueleza bayana kuwa alifurahia kuhudhuria vikao vya Ukawa kwa mara ya kwanza, Zitto alikwenda mbali na kumpongeza “kwa namna ya pekee” Mbowe kwa jinsi walivyoshirikiana katika sakata hilo.
Zitto alisema hilo lilikuwa ni jambo la kitaifa ndiyo maana wabunge wote wa upinzani bila kujali vyama vyao waliungana.
Alisema mara baada ya sakata hilo kumalizika watu mbalimbali wamekuwa wakizungumzia kufanyika kwa maridhiano ili awe sehemu ya Ukawa na kwamba haoni tatizo.
“Katika hili, kipekee namshukuru kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani kwa kuniunga mkono katika sakata hili,” alisema Zitto.
Kuhusu taarifa za kujiunga kwake na chama kipya cha ACT-Tanzania alisema: “Hizo ni taarifa ambazo hazina ukweli wowote.”
Kuhusu kesi aliyofungua mahakamani dhidi ya Chadema, Zitto alisema:
“Nilifungua kesi kwa sababu ya kulinda uanachama wangu, lakini mazungumzo yakifanyika na kujua kosa langu ni nini, nitaifuta kesi hiyo na kuanza upya harakati.”
Zitto.
Kuhusu taarifa za kujiunga kwake na chama kipya cha ACT-Tanzania alisema, “Hizo ni taarifa ambazo hazina ukweli wowote.”
Kuhusu kesi aliyofungua mahakamani dhidi ya Chadema, Zitto alisema: “Nilifungua kesi kwa sababu ya kulinda uanachama wangu, lakini mazungumzo yakifanyika na kujua kosa langu ni nini, nitaifuta kesi hiyo na kuanza harakati.”

No comments: