Thursday, January 8, 2015

MICHEZO 24--YANGA YAMTEMA RASMI KASEJA

YANGA SC imetangaza rasmi kuachana na mlinda mlango Juma Kaseja, iliyemsajili kwa Sh. Milioni 40 Novemba 8, mwaka juzi.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Yanga SC, Jerry Muro amewaambia Waandishi wa Habari leo katika hoteli ya Zanzibar Ocean View visiwani hapa kwamba, hatua hiyo imefikiwa baada ya mchezaji huyo kuanza kujiengua katika timu.

“Tumefikia uamuzi wa kuachana na Kaseja, baada ya yeye mwenyewe kuanza kujiengua katika timu,”amesema Muro.

Mwishoni mwa mwaka jana, Kaseja aliwasilisha barua kwa mwajiri wake, Yanga SC kutoa taarifa ya kuvunja makataba wake, uliokuwa umebakiza mwaka mmoja.
Katika barua yake, Kaseja alisema sababu ya kuvunjwa Mkataba huo ni kukiukwa kwa masharti yaliyokubaliwa wakati wa kusainiwa Novemba 8, mwaka jana.

Barua ya Kaseja iliyotumwa kupitia wakili wake, Mbamba & Co Advocates, Kaseja imesema wakati wa kusainiwa Mkataba huo ilikubaliwa malipo ya Sh. Milioni 40 yafanyike kwa awamu mbili.

Alisema awamu ya kwanza, alilipwa Sh. Milioni 20 baada ya kusaini Mkataba huo, na ikakubaliwa fungu lililobaki apatiwe Janauri 15, mwaka jana na kwa sababu malipo ya fedha ndio msingi wa Mkataba wenyewe, kushindwa kulipa fedha hizo kunaondoa uhalali wake.hivyo, Yanga SC baadaye ilikuja kusema imekwishamlipa fedha zake zote Kaseja na hana anachodai, ingawa kipa huyo alifungua madai mapya, akidai anachukiwa na kocha wa makipa, Juma Pondamali hivyo hana amani ya kufanya kazi.

No comments: