Monday, February 9, 2015

RAIS KIKWETE AANZA ZIARA MKOANI KILIMANJARO,HIKI NDICHO ATAKACHOKIFANYA



RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Jakaya Kikwete leo anatarajia kuanza ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Kilimanjaro ambapo miongoni mwa shughuli anazotazamiwa kufanya ni pamoja na
kufungua jengo la kitega uchumi la Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii
(NSSF).
 
Mbali na ufunguzi huo Rais Kikwete pia anatarajia kufungua jengo la Upasuaji na kuweka jiwe la msingi katika jengo la wodi ya wazazi na watoto katika hosptali ya rufaa ya mkoa wa Kilimanjaro ,Mawenzi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ,mkuu wa mkoa huo Leonidas Gama alisema Rais Kikwete atawasili mkoani humo leo jioni majira ya saa 11:00 jioni ambapo atapokelewa katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) na kuelekea Ikulu ndogo kwa ajili ya kupokea taarifa ya Mkoa.

Alisema Kesho (February 10) Rais Kikiwete  atafanya shughuli katika Hospitali ya Rufaa ya Mawenzi ikiwemo ufunguzi wa jengo la Upasuaji (Theater) ambalo limekuwa tatizo la muda mrefu katika hosptali hiyo.

“Kwanza kama mnavyo fahamu tumekuwa na tatizo la muda mrefu ya wodi ya upasuaji katika hospitali yetu ya Mawenzi,lakini kwa juhudi zilizofanywa na serikali na ushirikiano wa wadau mbalimbali lile jengo

la Upasuaji limekamilika na liko katika kiwango kizuri kwa hiyo shughuli ya kwanza atakuja kulifungua rasmi jengo la upasuaji.”alisema Gama. 
RAS-Seviline Kahitwa (shoto) RC Gama (Kulia)

Gama alisema pia Serikali tayari  imefanya juhudi za kujenga jengo jipya la Wodi kwa ajili ya Wazazi na Watoto katika hosptali hiyo na kwamba Rais Kikwete ataweka rasmi jiwe la msingi  kwa ajili ya muendelezo wa ujenzi wa jengo hilo.

Alisema kwa mujibu wa ratiba shughuli ya mwisho anayotazamia kufanya Rais Kikwete ni ufunguzi rasmi wa jengo la kitega Uchumi la NSSF,jengo
ambalo litatumika kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi .

“Ufunguzi rasmi wa jengo hili utabadilisha taswira ya mji wetu,ni jengo la kisasa lenye Hotel,Maofisi mbalimbali,Kumbi za mikutano na maduka mbalimbali makubwa kwa madogo ambayo yatahudumia wananchi wote”alisema Gama.

Gama alitoa wito kwa viongozi na wananchi wote wa mkoa wa Kilimanjaro kujitokeza kwa wingi katika ufunguzi wa jengo hilo la NSSF majira ya saa 2:00 asubuhi ambapo rais Kikwete pia atapata nafasi ya kuzungumza na wananchi.

“Lengo la Rais Kikwete kuja ni kutuunga mkono sisi wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro katika miradi yetu ya maendeleo hivyo basi tufike mapema katika maeneo hayo ili tumsubiri na tumuone rais na kumshangilia”alisema Gama.
Hili ndio jengo jipya la kisasa la kitega Uchumi la Mfuko wa Hifadhi ya Jami NSSF mkoani Kilimanjaro

No comments: