Sunday, March 22, 2015

CHUKUA MUDA WAKO USOME UJUMBE HUU WA MNYIKA LEO SIKU YA MAJI TANZANIA



Ujumbe wa wiki ya maji kitaifa ni “maji kwa maendeleo endelevu” na maadhimisho yanafanyika Musoma ambao Rais anatajiwa kuhutubia. Kwa kuwa maadhimisho haya ni ya mwisho kwa utawala wake, anapaswa kulieleza taifa ni kwa nini ameonyesha udhaifu wa kushindwa kutekeleza ahadi yake aliyoitoa wakati akizindua Bunge mwaka 2005 ya kwamba anatambua kuwa maji ni kero ‘nambari wani’ na kwamba Serikali yake ingeandaa mpango kabambe wa kuhakikisha matatizo ya maji yanakuwa historia.


Ameonyesha udhaifu 2005-2010 na ameendeleza udhaifu huo mwaka 2010-2015 hivyo aelekeze Waziri Mkuu atekeleze ahadi iliyotolewa na Waziri Mwandosya kwa niaba yake ya Serikali kuwasilisha katika kila Mkutano wa Bunge Taarifa ya Mpango wa dharura kwa kuwasilisha katika Mkutano huu wa 19 wa Bunge taarifa hiyo.

Aidha, nabashiri kwamba Rais atatumia maadhimisho ya Musoma kwenye uzinduzi wa miradi kueleza ‘mafanikio’ makubwa yaliyopatikana kutokana na Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (MMS)- Big Results Now BRN.

Hata hivyo, Rais azingatie kwamba MMS/BRN kwenye Sekta ya Maji haijaweza kushughulikia kwa ukamilifu matatizo niliyoyaeleza kwenye hoja binafsi niliyowasilisha Bungeni kuhusu Hatua za Haraka za Kuboresha Upatikanaji wa Maji Safi na Ushughulikiaji wa Maji Taka Jijini na Nchini (Rejea: http://mnyika.blogspot.com/2013/02/maelezo-na-hoja-binafsi-ya-kupendekeza.html ). Ilani ya CCM ya mwaka 2005 iliahidi ifikapo 2010 maji yangepatikana mijini ikiwemo Jijini Dar Es Salaam kwa asilimia 90 na vijijini kwa asilimia 75 ahadi ambayo haijatekelezwa.

Ili Rais asiendelee kuonekana dhaifu zaidi walau kupitia siku hii ya maji awaagize watendaji katika ofisi yake watekeleze agizo alilowapa la kuitisha kikao cha kazi Ikulu kuhusu matatizo ya maji katika Jiji la Dar Es Salaam mwezi Machi 2013 kama alivyoahidi ( rejea: http://gkitalima.blogspot.com/2013/03/jakaya-kikwete-kukutana-na-mnyika.html na http://www.matukiotz.co.tz/2013/03/mnyika-aitwa-ikulu.html ).

Namshukuru Rais kwamba kuna hatua katika upatikanaji wa fedha na utekelezaji wa miradi ya Ruvu Chini na Ruvu Juu na pia miradi mingine ya visima vya dharura ikiwemo katika Jimbo la Ubungo ikiwemo mradi wa Mpiji Magohe ambao tumeuzindua siku chache zilizopita kama sehemu ya maadhimisho ya wiki ya maji; hata hivyo kasi, nguvu na ari ya mpaka sasa hailingani na ahadi za kufanya tatizo la maji kuwa historia 2010, 2011, 2012, 2013, 2014 na hata 2015.

Zipo hatua zaidi zinaweza kuchukuliwa katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia sasa iwapo tukikutana  na kujadili udhaifu uliopo katika utekelezaji wa Mpango Maalum wa maji Dar es Salaam; hivyo kwa kuwa nimeshamkumbusha yeye mwenyewe na wasaidizi wake mara kadhaa bila kikao hicho kuitishwa ni wakati sasa wa wananchi wa Dar Es Salaam kushiriki kumkumbusha kwa njia mtakazoona zinafaa.

Kwa kuzingatia hali hii kwa wote wenye kutaka kushiriki ujumbe wetu kwake na kwa wengine kitaifa unapaswa kuwa #Maji Na Mabadiliko Kwa Maendeleo ( #MaMaMa ) ili tuitumie siku hii na zijazo kuhamasisha mabadiliko yenye kuwezesha kupatikana kwa maji kwa maendeleo ya wananchi na nchi kwa ujumla. ( #WaterIs #MaMaMa ).
Wenu katika uwakilishi wa wananchi,
John Mnyika (Mb)
Jimbo la Ubungo

22 Machi 2015

No comments: