Saturday, March 21, 2015

PAMOJA NA HIZI MBWEMBWE ZA MGAMBO,YANGA YAWAGEUZA SUNGUSUNGU JIONI HII

Mashabiki wa mgambo wakiwa wanaingia uwanjani leo



YANGA SC imezidi kuwatoroka mabingwa watetezi, Azam FC katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kufuatia ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya wenyeji Mgambo Shooting Uwanja wa Mkwakwani, Tanga jioni ya leo.

Ushindi huo, unaifanya Yanga SC ifikishe pointi 37, baada ya kucheza mechi 18, ikiwazidi kwa pointi nne, Azam FC ambao hata hivyo wana mchezo mmoja mkononi wanacheza na Coastal Union kesho mjini hapa.
Haukuwa ushindi mwepesi kwa Yanga SC, kwani iliwabidi kusubiri hadi dakika 15 za kumalizia kupata bao la kwanza.

Amisi Tambwe  na Simon Msuva ndiyo waliifungia pia Yanga SC ikishinda 2-1 dhidi ya Kagera Sugar katika mchezo uliopita



Winga Simon Msuva alifumua shuti kali kuipatia Yanga SC bao la kwanza dakika ya 77 baada ya kukutana na mpira uliorudi kufuatia kutokea kizazaa langoni mwa Mgambo kutokana na krosi ya Haruna Niyonzima.

Wakati Mgambo wanajaribu kutafuta bao la kusawazisha, Yanga SC walifanya shambulizi la kushitukiza na kufanikiwa kupata bao la pili dakika ya 83, mfungaji Mrundi Amisi Tambwe aliyemalizia krosi ya Msuva.

Mgambo walionyesha upinzani wa kutosha kwa Yanga SC, lakini wakashindwa kurudia kile walichokifanya kwa Simba SC- kuwafunga 2-0 na Wana Jangwani wamewalipia kisasi watani wao, ambao walitota 2-0 kwa timu hiyo ya JKT wiki iliyopita. 

Kikosi cha Mgambo Shooting kilikuwa; Godson Mmasa, Bashiru Chanacha, Salim Mlima, Ramadhan Malima, Salum Kipaga, Novaty Lufunga, Mohammed Samatta, Ally Iddy, Malimi Busungu, Fully Maganga na Salim Gilla.

Yanga SC; Ally Mustafa ‘Barthez’, Mbuyu Twite/Juma Abdul dk56, Oscar Joshua, Kevin Yondan/Rajab Zahir dk67, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Said Juma ‘Kizota’, Salum Telela, Haruna Niyonzima, Amisi Tambwe, Kpah Sherman/Hussein Javu dk78 na Simon Msuva.




No comments: