Thursday, October 22, 2015

UKAWA wametoa Taarifa hii kuhusu atakachokifanya LOWASA kesho,pitia hapa


Kupitia taarifa hii kwa vyombo vya habari, tunapenda kuutaarifu umma wa Watanzania wote nchini kuwa Mgombea Urais wa CHADEMA anayeungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), Mh. Edward Ngoyai Lowassa atahutubia taifa kupitia vituo mbalimbali vya televisheni, redio na njia zingine za upashanaji habari hususan mitandao ya kijamii (live streaming facebook, twitter, forums etc), siku ya Ijumaa, tarehe 23 Oktoba, 2015, saa 3 usiku.


Kupitia hotuba hiyo kwa taifa, Mh. Lowassa atazungumza na Watanzania wote, ndani na nje ya nchi, na watu wa mataifa yote, kuhusu Tanzania mpya itakayotokana na MABADILIKO makubwa ya kimfumo, kiutawala na utendaji wa serikali atakayoiunda baada ya Watanzania kumpatia dhamana ya kuwa Mkuu wa Nchi, Amiri Jeshi Mkuu na Kiongozi Mkuu wa Serikali hapo Oktoba 25, 2015.

Aidha, Mhe. Lowassa atatumia muda huo kuwashukuru Watanzania wote kwa namna walivyomuunga mkono kwa upendo mkubwa yeye, mgombea mwenza wake, Juma Duni Haji, chama na UKAWA kwa ujumla katika uchaguzi huu wa MABADILIKO, ya kuhitimisha utawala wa nusu karne wa CCM kuliandaa taifa na uongozi mpya utakaotoa utumishi wa kuliondoa taifa hapa lilipokwama katika umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi unaowatafuna Watanzania.

Hiyo ni dalili ya wazi kwamba serikali atakayoiunda itatokana na watu kwa ajili ya watu ambao ni umma wa Watanzania wote.

Imetolewa leo Alhamis, Oktoba 22, 2015 na;
Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano

No comments: