Wednesday, November 25, 2015

JAJI MKUU WA TANZANIA MHE. OTHMAN CHANDE ATOA SOMO KWA WAANDISHI WA HABARI.

MO1
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Othman Chande akitoa ufafanuzi kwa wanabari (hawapo pichani) kuhusu uandishi bora wa habari za Mahakama wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa Habari za Mahakama leo jijini Dar es salaam.
MO2
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Othman Chande (kushoto) na Meneja wa Maadili wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) Allan Lawa (kulia) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari za Mahakama yaliyoandaliwa na Mahakama ya Tanzania leo jijini Dar es salaam.
MO3
Rais wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) Jaji Mstaafu Thomas Mihayo akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa Habari namna wanavyoweza kuandika habari za Mahakama kwa kuzingatia weledi wa taaluma zao.
MO4
Washiriki wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa Habari za Mahakama wakiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Othman Chande leo jijini Dar es salaam.
MO5
Baadhi ya wanahabari wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa Habari za Mahakama leo jijini Dar es salaam.
Picha/Aron Msigwa –MAELEZO.

………………………………………………………………………………
Na. Aron Msigwa –MAELEZO.
 Dar es salaam.
Waandishi wa habari nchini wametakiwa kuzingatia weledi wa taaluma zao wanapoandika habari za Mahakama ili kuepuka kuandika habari zinazowatia hatiani watuhumiwa na kushindwa kutofautisha kati ya  mshitakiwa na mtuhumiwa pamoja na haki zake.
Akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo waandishi wa Habari za Mahakama leo jijini Dar es Salaam, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Othman Chande  amesema waandishi wa habari  wanalojukumu la kuwapatia wananchi taarifa sahihi kuhusu masuala yanayowahusu na kuepuka uandishi wa habari zenye kuhukumu.
Amesema  kisheria mtuhumiwa huwa hana hatia mpaka itakapothibitishwa na mahakama kuwa ametenda kosa na kuongeza kuwa kukosekana kwa weledi katika uandishi wa habari za mahakama  huleta mkanganyiko  miongoni mwa jamii  kuhusu ukweli na kuondoa imani ya watu kwa mahakama.
Ameongeza kuwa baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa Vikitoa  habari zisizo mpatia mtu  fursa na haki ya kujibu tuhuma huku vingine vikitoa taarifa nusunusu na kushindwa kuwa na mwendelezo wa habari za mashauri mbalimbali mahakamani.
Mhe.Chande ameeleza kuwa waandishi wamejikita katika uandishi wa taarifa zenye mvuto kwa jamii na kusahau nyingine walizo anza nazo jambo  linalosababisha wananchi kuachwa  njia panda bila kupata taarifa za kina kuhusu mwisho wa mambo yanayoanzishwa.
” Mimi sitaki kuingilia utendaji wa kazi zenu za kila siku ila nachotaka kusema ni kuweka msisitizo wa utoaji wa habari za mashauri mbalimbali mnayoanza kuyaripoti kwa mwendelezo ili msiwachanganye wananchi” Amesisitiza.
Amewataka waandishi wa habari kuandika habari sahihi na kuepuka upendeleo na maslahi binafsi ili kulinda taaluma na imani katika jamii juu ya utendaji wa vyombo vya habari.
Mhe. Chande ametoa wito kwa waandishi wa habari kuepuka uandishi wa habari zilizojaa chuki zinazoweza kuleta mgawanyiko katika jamii na kusisitiza habari za kuisaidia jamii kukabiliana na changamoto mbalimbali.
Kuhusu Mahakama amesema itaendelea kuboresha huduma na miundombinu yake katika maeneo yasiyofikiwa ili kuendelea kutoa haki kwa wakati pia  kushirikiana na waandishi wa habari wa ndani ili kuimarisha utendaji wao.
Aidha amevipongeza vyombo vya habari kwa ukomavu  viliouonyesha wakati wa utoaji wa taarifa za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
Kwa upande wake Rais wa Baraza la Habari Tanzania Mhe. Jaji Mstaafu Mhe.Thomas Mihayo akizungumza kwa niaba ya Baraza hilo ametoa wito kwa waandishi wa habari kuzingatia weledi katika uandishi wa habari za mahakama ili kuepusha madhara katika jamii.
Amewataka waandishi kujikita zaidi katika uandishi wa habari zenye uhakika kuliko kuwa na taarifa zenye mlengo wa kuuza gazeti.
Amesema kuwepo kwa mafunzo hayo ambayo yameandaliwa na Mahakama ya Tanzania ni ishara nzuri ya uboreshaji wa taaluma ya habari hasa uongezaji wa ushirikiano katika kutekeleza majukumu ya kimahakama hapa nchini.
Amewataka wanahabari kujifunza na kufuatilia miongozo na kufuatilia taarifa mbalimbali zinazoweza kuboresha uandishi wao kwa kupata maneno sahihi ya kimahakama.Amesema Semina hiyo itawasaidia waandishi wa habari kujenga weledi katika uandishi wa habari za mahakama.
Ametoa tahadhari kwa waandishi kuepuka uandishi wa habari zenye uchochezi ili kuepuka kushtakiwa na jamii, kuepuka lugha za kishabiki na upendeleo.
Naye Meneja wa Maadili wa Baraza la Habari Tanzania (MCT) Allan Lawa akizungumza kwa niaba ya washiriki wa mafunzo hayo amewataka kuepuka kuandika habari zinaonyesha upendeleo na  kubainisha kuwa kuwa ipo haja kwa vyombo vya habari kutenga maeneo madawati ya habari hizo

No comments: