Wednesday, November 11, 2015

STARS KUREJA LEO


Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager inarejea leo nyumbani kwa shirika la ndege la Fastjet, ambapo inatarajiwa kuwasili uwanja wa JK Nyerere majira ya saa 12 kamili jioni.

Stars iliyokuwa imeweka kambi nchini Afrika Kusini kwa takribani siku 10, inarejea nyumbani ikiwa imefanya mazoezi vizuri kujiandaa na kuwakabili Mbweha wa Jangwani Algeria siku ya Jumamosi katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Akiongelea kuhusu kambi kocha wa Stars, Charles Mkwasa amesema anashukru kwa kambi waliyoipata Afrika Kusini, wachezaji wote wameweza kufanya mazoezi katika kiwango cha juu, hapakua na majeruhi hivyo ana imani vijana wake watafanya vizuri siku ya Jumamosi.
Mkwasa amewaomba watanzania na wapenzi wa mpira wa miguu nchini, kujitokeza kwa wingi uwanjani kuja kuwasapoti katika mchezo dhidi ya Algeria, uwepo wa watanzania wengi uwanjani kuwashangilia utaongeza morali zaidi kwa wachezaji watakaokuwa wanapeperusha bendera ya Tanzania.
Mara baada ya kuwasili jijini Dar es salaam, kikosi cha Mkwasa kitafanya mazoezi kesho Alhamis jioni katika uwanja wa Taifa, na Ijumaa yakiwa ni mazoezi ya mwisho kabisa ya mchezo wenyewe unaosubiriwa kwa hamu.

Wakati huo huo wachezaji Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu wamewasili jijini Dar es salaam leo asubuhi , na moja moja kuingia kambini huku wakiwasubiri wachezaji wenzao wanaowasili leo na kujumuika pamoja kambini.

No comments: