Monday, January 25, 2016

DARAJA LA KIGAMBONI KUANZA KUTUMIKA MACHI MOSI

d1Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (sehemu ya Ujenzi) Eng. Joseph Nyamhanga (wa nne kushoto), akitoa maelekezo kwa Msimamizi na Meneja Mkuu wa mradi wa ujenzi wa daraja la kigamboni kutoka mfuko wa Hifadhi ya jamii (N.S.S.F) Mhandisi John Msemo (wa kwanza kushoto) wakati wa ziara ya kushtukiza iliyofanywa na Katibu huyo kukagua maendeleo ya ujenzi wa daraja hilo.
d2Msimamizi na Meneja Mkuu wa mradi wa ujenzi wa daraja la kigamboni kutoka mfuko wa Hifadhi ya jamii (N.S.S.F) Mhandisi John Msemo, akimuonesha Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (sehemu ya Ujenzi) Eng. Joseph Nyamhanga (wa kwanza kulia) sehemu ya kipande cha km 1.5 kilichopo upande wa Kigamboni kwa ajili ya upanuzi wa daraja hilo.

d3Mwonekano wa Ofisi za Daraja la Kigamboni zitakazotumiwa na wasimamizi wa daraja hilo linalotarajiwa kuanza kazi rasmi mwezi Machi mwaka huu.
d4Lango la kuingilia daraja la Kigamboni linavyoonekana, pembeni ni ofisi za huduma mbalimbali zitakazokuwa zinatolewa darajani hapo.
d5Sehemu ya juu ya daraja la Kigamboni, likiwa katika hatua za mwisho za ujenzi wake.
……………………………………………………………………………..
Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano sehemu ya Ujenzi Eng. Joseph Nyamhanga amesema daraja la Kigamboni litaanza kutumika kuanzia Machi mwaka huu.
Akizungumza mara baada ya kukagua hatua za ujenzi wa daraja hilo Eng. Nyamhanga amemtaka msimamizi wa ujenzi huo kuhakikisha hatua ya ujenzi iliyobaki inakamilika katikati ya mwezi februari na kuanza kazi mwanzoni mwa mwezi Machi.
“Hakikisheni Machi mosi magari yaanze kupita rasmi kwenye daraja hili na hivyo kufungua ukurasa mpya kwa wakazi wa Kigamboni ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikabiliwa na msongamano katika eneo la Magogoni”, amesema Eng. Nyamhanga.
Eng. Nyamhanga amesisitiza kuwa Serikali inaangalia uwezekano wa kuunganisha daraja la Kigamboni na barabara ya Charambe,Mlandizi hadi Chalinze ili kupunguza msongamano wa magari katikati ya Jiji.
Amemtaka meneja wa mradi wa ujenzi wa daraja hilo toka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eng. John Msemo kuhakikisha anatafuta Wakala makini atakayesimamia na kuendesha mradi huo.
Daraja la Kigamboni lenye urefu wa mita 680, unasimamiwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano linatarajiwa kuishi zaidi ya miaka 100 na kuwa na uwezo wa kupitisha mizigo ya tani 56 zinazokubalika katika nchi za jumuiya ya madola.
IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO WIZARA YA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO

No comments: