Wednesday, January 27, 2016

Kama ulikosa kilichotokea bungeni Jioni tizama hapa

Hali ya Sintofahamu imetawala Bungeni jioni ya leo kufuatia wabunge wa Upinzani kupinga TBC kusitisha kurusha live matangazo ya moja kwa moja kuanzia jana kwa kigezo cha kubana matumizi.

Kutokana na vurugu hizo, Polisi wamelazimika kuingia Bungeni na kuwatoa nje wabunge wa Upinzani kufuatia kugoma kutokana na maagizo ya Mwenyekiti wa Kikao cha Bunge, Andrew Chenge.

Chanzo cha vurugu hizo  ni  Wabunge wa Upinzani kupinga kuendelea kwa mjadala wa Bunge wakitaka kauli ya Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo, Nape Nnauye kuhusu TBC kusitisha kurusha matangazo ya moja kwa moja toka Bungeni  ijadiliwe kwanza.

Sakata hilo liliibuka tangu asubuhi ambapo Mwenyeki wa Bunge, Andrew Chenge aliahirisha Kikao cha Bunge mara mbili huku akiitaka kamati ya uongozi kukutana  ili kutoa majibu.

Maamuzi ya kamati ya uongozi  
Baada ya Bunge kurejea jioni hii mwenyekiti wa Bunge Andrew Chenge ameliambia Bunge kuwa maamuzi ya kamati ya uongozi baada ya kuketi mchana wa leo ni kama ifuatavyo.

(a) Mwenyekiti wa Bunge alikuwa sahihi kutaka hoja iliyokuwa mbele ya Bunge kuhusu hotuba ya Rais iendelee.

(b) Hakuna haki yoyote ya Bunge iliyovunjwa kwa Bunge kuendelea na kazi yake baada ya hoja ya Waziri

(c) Hoja ya Bunge iliyo mbele ya Bunge ni hotuba ya Rais na kamati ya uongozi imeagiza shughuli ziendelee kama kawaida.

(d) Endapo kuna Mbunge yoyote ambaye hataridhika atumie kanuni ya 5 (4) kuomba kibali kwa katibu wa bunge ili apate nafasi maalumu.

Aidha kwa mujibu wa ratiba ya kikao cha Bunge ni kwamba Bunge litajadili hotuba ya Rais Magufuli aliyoitoa wakati wa ufunguzi wa Bunge la 11 Novemba 20, 2015 kwa muda wa siku 3. Baada ya kauli hii, vurugu ziliibuka Bungeni
Wabunge  wa  Upinzani walianza kupiga mayowe, ikiwemo kuimba nyimbo mbalimbali suala lililomlazimu Mwenyekiti kuwaondoa Wabunge wa Ukawa wote watoke nje ili wabunge wengine waendelee na kikao cha kujadili hotuba ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

No comments: