Monday, January 25, 2016

RAIS DKT. MAGUFULI AMTEUWA MAHADHI JUMA MAALIM KUWA BALOZI WA TANZANIA NCHINI KUWAIT

BKatibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) leo jijini Dar es salaam.
……………………………………………………….

Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
 Mhe. Rais Dkt. Magufuli amemteua aliyekuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwenye Serikali ya Awamu ya Nne Mahadhi Juma Maalim kuwa Balozi wa Tanzania nchini Kuwait kufuatia uamuzi wa Serikali kufungua Ofisi ya Ubalozi katika nchi hiyo rafiki.
Vile vile Rais ameagiza Wizara ya Mambo ya Nje, Afrika Mashariki na Ushirikiano wa Kikanda na Kimataifa kuwarejesha nyumbani mara moja Mabalozi wawili ambao mikataba yao imeisha na kuwataka Mabalozi hao kukabidhi kazi kwa Afisa Mkuu au Mwandamizi aliyechini yao leo hii.

Mabalozi hao ni Bi Batilda Salha Buriani, aliyeko Tokyo, Japan, Dkt. James Alex Msekela, aliyeko Rome, Italia.
Kwa mujibu wa Balozi Sefue, Rais pia amemrejesha nyumbani Balozi wa Tanzania aliyeko London, Uingereza, Bwana Peter Allan Kallaghe ambaye anarejea Wizara ya Mambo ya Nje, Afrika Mashariki na Ushirikiano wa Kikanda na Kimataifa ambapo atakapopangiwa kazi nyingine.

Balozi Sefue alisema kuwa hadi sasa vituo vya Ubalozi ambavyo viko wazi ni London nchini Uingereza kufuatia kurejea nchini kwa Balozi Peter A. Kallaghe, Brussels nchini Ubelgiji kufuatia aliyekuwa Balozi, Dkt. Deodorous Kamala kuchaguliwa kuwa Mbunge, Rome nchini Italia, kufuatia kuisha kwa mkataba wa Dkt. James Alex Msekela na Tokyo nchini Japan, kufuatia kuisha kwa mkataba wa Bibi Batilda Buriani.

Vituo vingine vya Ubalozi ambavyo viko wazi ni Kuala Lumpar nchini Malaysia, kufuatia aliyekuwa Balozi Dkt. Aziz Ponray Mlima kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje, Afrika Mashariki na Ushirikiano wa Kikanda na Kimataifa na Brasilia nchini Brazil, kufuatia kustaafu kwa aliyekuwa Balozi, Bwana Francis Malambugi.
Wakati huo Balozi Sefue alisema kuwa Rais ametengua uteuzi wa Mhandisi Madeni Juma Kipande kabla hajathibitishwa kwenye cheo cha
Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi kutokana na utendaji kazi usioridhisha.

No comments: