Wednesday, January 20, 2016

SERIKALI YAKANUSHA UZUSHI UNAOENEZWA KATIKA MITANDAO YA KIJAMII KUMHUSU RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

E1
Kaimu Mkurugenzi wa idara ya Habari MAELEZO Bi Zamaradi Kawawa akitoa ufafanuzi juu ya taarifa za uzushi unaosambazwa katika mitandao ya Kijamii ya ndani na nje ya nchi kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimwa Dkt. John Pombe Magufuli amefukuza wageni kutoka nje waliokuwa wanafanya biashara hapa nchini kwa kuwa Serikali yake haitataki wageni wafanye bishara zao nchini ambapo ukweli ni kwamba Serikali haijafukuza wageni wanaofanya biashara zao nchini na haina mpango wa kufanya hivyo kwa wageni wanaoishi nchini kwa vibali vilivyotolewa kisheria na Serikali.kushoto ni Naibu Kamishna na Msemaji wa Idara ya Uhamiaji Bw. Abbas Irovya na mwisho kushoto ni Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani Isaac Nantanga,Kulia ni Naibu Kamishna wa Idara hiyo Bw.Wilson Bambaganya.
E2
Naibu Kamishna na Msemaji wa Idara ya Uhamiaji Bw. Abbas Irovya akitoa wito kwa Watanzania kuwafichua wale wote wanaoingia na kuishi nchini kinyume cha sheria ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa mujibu wa Sheria na kanuni na kusisitiza kuwa Ofisi yake itaendelea kufanya oparesheni ya kuwakamata watu hao, kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa idara ya Habari MAELEZO Bi Zamaradi Kawawa na Mwisho Naibu Kamishna wa Idara hiyo Bw.Wilson Bambaganya.
E3
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano Idara ya Habari Maelezo kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji ukilenga kutoa ufafanuzi kuhusu taarifa za upotoshaji zinasozambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa Serikali imewafukuza wafanyabiashara wakigeni wanaofanya kazi zao hapa nchini ,taarifa hizo si za kweli na zinalenga kuichafua Serikali ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

(Picha na Frank Mvungi-Maelezo)
………………………………………………………………………….
Hivi karibuni kumejitokeza uzushi unaosambazwa katika mitandao ya kijamii ya ndani ya nchi na nje ya nchi kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amefukuza wageni kutoka nje waliokuwa wanafanyabiashara zao nchini kwa kuwa serikali yake haitaki wageni kufanya biashara nchini.
Serikali haijafukuza wageni kutoka nje ya nchi kufanya biashara nchini na haina mpango wa kuwafukuza wageni wanaoishi nchini kwa vibali vilivyotolewa kisheria na Idara ya Uhamiaji.
Uzushi huo usiokuwa na ukweli umeenezwa kufuatia Idara ya Uhamiaji kutekeleza jukumu lake la kufuatilia wageni wote wanaoishi nchini bila vibali halali vya ukaazi ambapo kwa mwezi Novemba na Desemba mwaka 2015 wageni 372 walioondoshwa nchini.
Kazi ya kufuatilia wageni wanaoishi nchini bila vibali halali vya kisheria haijaanza katika Serikali ya Awamu ya Tano. Idara ya Uhamiaji nchini tangu Januari hadi Desemba mwaka jana iliondosha nchini jumla ya wageni 1,642 waliokuwa wanaishi na kufanya shughuli zao nchini kinyume na Sheria.
Uzushi unaoenezwa hauna ukweli wowote na hauna nia njema na nchi yetu kwani kati ya mwaka 2014 na 2016 Idara ya Uhamiaji imetoa vibali vya ukaazi (Residence Permits) 40,765 kwa wageni wawekezaji na wafanyabiashara, wageni wanaofanyakazi za kuajiriwa, wageni wanaokuja kwa ajili ya Masomo, matibabu, dini, utafiti na wastaafu kuishi na kufanya shughuli zao nchini.
Serikali inawakaribisha wageni kuja nchini kuwekeza na kufanya shughuli zao kwa kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi.
Aidha, kuna uzushi unaenezwa kuwa Rais Dkt John Pombe Magufuli amepiga marufuku wanawake kuvaa nguo fupi kama njia ya kupunguza kasi ya maambukizi ya ugonjwa wa UKIMWI.
Mheshimiwa Rais tangu aingie madarakani hajawahi kuagiza wala kutoa tamko kuhusiana na uzushi wa kukataza uvaaji wa nguo fupi ili kupunguza maambukizi ya Ukimwi kama inavyoenezwa katika mitandao ya ndani na Nje ya Nchi ambayo inanukuu habari hiyo kuwa imeandikwa na Gazeti la Kenya “The Standard”
Serikali inapenda kuutangazia umma kuwa uzushi huo unaomhusu Mheshimiwa Rais Magufuli umetungwa na watu wasioitakia mema nchi yetu kwa lengo la kumdhalilisha Rais na hauna ukweli hivyo watu wasishiriki kuueneza kwa njia yeyote ile.
Serikali kupitia balozi zake za Kenya na Afrika Kusini zinafuatilia chanzo cha uzushi huu kuhusu Rais Magufuli kwa kushirikiana na nchi husika na watakaobainika kutunga na kueneza uzushi huu watachukuliwa hatua za kisheria.

No comments: