Thursday, January 14, 2016

WATEJA WA TIGO PESA WAANZA KUVUNA GAWIO LA ROBO MWAKA

Mkuu wa Fedha na Tahadhari wa Huduma ya Fedha kwa njia ya mtandao wa Kampuni ya simu ya Tigo, Obedi Laiser (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, kuhusu gawio la mwaka huu  kwa watumiaji wa Tigo Pesa ambalo watumiaji hao wameanza kulipata kuanzia jana. Kulia ni Meneja wa Mawasiliano wa Tigo, John Wanyancha.
Wanahabari wakichukua taarifa hiyo.
Meneja wa Mawasiliano wa Tigo, John Wanyancha (kulia), akizungumza katika mkutano huo.
Na Dotto Mwaibale



Kampuni inayongoza katika kuleta maisha ya kidijitali kwa jamii, Tigo, imetangaza tena malipo ya robo mwaka ya shilingi bilioni 4.4 (dola milioni 2.1) kwa watumiaji wake wa huduma ya Tigo Pesa wapatao milioni 4.6. 

“Gawio hili la faida linalipwa kwa watumiaji wote wa Tigo Pesa wakiwemo wateja binafsi, mawakala wa rejareja na washirika wetu wa kibiashara, kila mmoja kutokana na thamani  ya fedha aliyojiwekea katika akaunti yake ya Tigo Pesa,” alisema Mkuu wa Fedha na Tahadhari wa Huduma ya Fedha kwa njia ya mtandao, Obedi Laiser.

 Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Laiser alisema  kuwa hii itakuwa ni mara ya kwanza Tigo kuwalipa gawio la faida watumiaji wa Tigo Pesa kwa mwaka wa 2016  akibainisha kuwa malipo hayo ni faida inayopatikana kutokana na amana ya mfuko wa Tigo Pesa uliyowekezwa katika benki za kibiashara hapa nchini. 

“Tunayo furaha kubwa kutangaza gawio hili la faida kwa mara ya saba mfululizo tangu tulivyoanza kufanya hivi mwaka 2014. Bila shaka hii inaonyesha ni jinsi gani Tigo inajizatiti kuwaletea watanzania maisha bora ya malipo kwa njia ya mtandao,” amesema Laiser.

Tigo ilikuwa kampuni ya kwanza duniani kutoa gawio kwa wateja wake mwaka 2014 
“Tunaamini gawio hili la kwanza la faida ya Tigo Pesa kwa mwaka 2016 litakuwa ni kivutio kikubwa kwa mamilioni ya watumiaji wa Tigo Pesa katika kufanikisha mahitaji  yao mbalimbali ya kifedha ya mwanzo wa mwaka,” amesema Laiser.

Malipo haya kwa watumiaji wa Tigo Pesa hutolewa kwa mujibu wa mwongozo wa Benki Kuu uliotolewa mnamo Februari mwaka 2014. Mpaka sasa Tigo imelipa jumla ya bilioni 35.5 kwa wateja wake tangu kuanzishwa kwa utaratibu huu mwaka juzi na kampuni hiyo. 

No comments: