Monday, April 11, 2016

DROO YA NUSU FAINALI KOMBE LA SHIRIKISHO KESHO

Droo ya Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho (Azam Sports Federation Cup), inatarajiwa kufanyika kesho Jumanne saa 3 usiku moja kwa moja (live) kupitia kituo cha luninga cha AzamTwo.
Hatua ya Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho (ASFC) itafanyika live katika kituo cha AzamTwo, ambao kupitia Azamtv ndio wadhamini wa wakuu wa michuano hiyo iliyoibua msisimiko wa mpira wa miguu na kushirikisha timu nyingi zaidi nchini.
Baada ya timu za Azam FC, Mwadui FC, na Yanga SC kukata tiketi ya kucheza Nusu Fainali, mshindi wa mchezo kati ya Simba SC dhidi ya Coastal Union utakaochezwa leo katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam atungana na timu hizo tatu kwenye droo ya kesho.
Michuano ya Kombe la Shirikisho iliyoanza kwa kushirikisha timu 64 mwishoni mwa mwaka jana, imefikia hatua hatua ya nusu fainali, baada ya Azam FC kuindoa Prisons (3-1), Mwadui FC kuiondosha Geita Gold (3-0) na Yanga SC kuwaondoa Ndanda FC kwa mabao (2-1).
Mshindi wa Kombe la Shirikisho (ASFC) msimu huu, ataiwakilisha Tanzania mwaka 2017 katika michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika (CAF CC).

No comments: