Wednesday, May 25, 2016

TANESCO YAWATAKA WATEJA WAKE KUZINGATIA SHERIA NA KANUNI ZA MATUMIZI YA UMEME

TAN1Meneja wa Afya na Usalama Mahali pa Kazi Kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mhandisi Majige Mabula akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) ambapo aliwataka wateja wa shirika hilo kuzingatia sheria na kanuni za matumizi ya umeme ili kuepuka ajali zinazoweza kusababishwa na hitilafu za umeme.Kulia ni Afisa Uhusiano wa Shirika hilo Bw. Yasini Silayo.
TAN2Baadhi ya Waandishi wahabari wakifuatilia mkutano huo. Picha na Hassan Silayo-MAELEZO

…………………………………………………………………………………………..
Frank Mvungi-Maelezo
Shirika la Umeme Tanzania limewataka wateja wake kuzingatia sheria na kanuni za matumizi ya umeme ili kuepuka ajali zinazoweza kusababishwa na hitilafu za umeme.
Kauli hiyo imetolewa leo Jijini Dar es salaam na Meneja wa Afya na Usalama kazini Mhandisi Majige  Mabulla wakati wa mkutano na vyombo vya habari.
Majige amesema kuwa moto hauwezi  kutokea endapo mtumiaji wa umeme atahakikisha kuwa mfumo wa umeme katika nyumba yake umesukwa na fundi ama mkandarasi aliyesajiliwa.
“Kuwa makini katika matumizi bora ya vifaa vinavyotumia umeme kama vile pasi,hita za umeme,kuchaji simu,kompyuta kutasaidia kupunguza au kuondoa tatizo la majanga ya moto” alisisitiza Mabulla.
Akizungumzia hatua nyingine zinazoweza kusaidia kuzuia majanga ya moto Mhandisi  Majige ni kuepuka kuweka vitu vinavyoweza kushika moto kirahisi karibu na nyaya ama maungio ya nyaya za umeme ndani ya nyumba .
Majige alitoa wito kwa watumiaji wa umeme kutoa taarifa pale wanapotaka kuongeza matumizi ya umeme kwa kiwango kikubwa ndani ya makazi ya watu ili tathmini ya uwezo wa nyaya kukidhi mahitaji yaliyoongezeka ifanyike.
Katika kuzuia matukio ya moto TANESCO imekuwa ikihakisha kuwa inamfikishia mteja umeme ulio salama na usiokuwa na madhara kwa mtumiaji kutoka kwenye nguzo mpaka kwenye mita.
Kwa kipindi kirefu sasa kumekuwepo na matukio ya ajali za moto katika makazi ya watu ambayo yamekuwa yakisababisha madhara  ikiwemo kusababisha vifo,majeruhi  na uharibifu wa mali.

No comments: