Friday, August 12, 2016

EXCLUSIVE--WARAKA WA VIJANA WA ACT KWENDA KWA RAIS MAGUFULI WAMUONYA KUIINGIZA NCHI GIZANI



RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
DK JOHN MAGUFULI
OFISI YA RAIS IKULU
1 BARABARA YA BARACK OBAMA
11400 DAR ES SALAAM,TANZANIA

Ndugu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dk John Pombe Magufuli
 Sisi vijana wa Chama cha ACT Wazalendo tunakusalimu katika  salam ya Kizalendo.

Tunayo heshima na taadhima kubwa kukuandikia barua hii, iliyobeba ujumbe makhsusi wa masikitiko na malalamiko yetu vijana na jamii nzima ya umma wa Watanzania kwa ujumla.

Masikitiko na malalamiko yetu yametokana na sintofahamu inayozidi kuibuka katika maeneo kadha wa kadha ya mawanda ya utawala wako tangu ulipokabidhiwa rasmi mamlaka ya kuongoza nchi yetu kwa kiapo ulichokula mbele ya hadhara ya Watanzania, pale Uwanja wa Uhuru mnamo tarehe 05 Novemba, 2015.



Kwa sehemu yetu ya  ngome ya Vijana wa chama cha Wazalendo, ujumbe wetu tunaokuletea unawakilisha hisia za maelfu ya vijana wa ACT na wasio wana-ACT nchi nzima.

Hata hivyo, kila mwanachama wa ACT Wazalendo angali anabaki kuwa huru yeye binafsi kukuandikia barua kama alivyoelekeza Kiongozi wa Chama chetu Ndugu Zitto Kabwe katika waraka wake kwa wanachama

UMUHIMU WA KULINDA KIAPO CHAKO CHA KULINDA KATIBA - ISHARA ZA KUDOGOSHA BUNGE NA KUZUIWA WABUNGE WANAOTETEA HAKI ZA WANANCHI

Ndugu Rais kabla ya kueleza kwa kina dhamira ya ujumbe wetu, Kwa unyenyekevu mkubwa, tunaomba kukukumbusha kiapo hicho cha utii na uaminifu kwa nchi yetu na Katiba. Ndugu rais, uliapa hivi;

i). ‘’Mimi, John Pombe Joseph Magufuli NAAPA kwamba nitakuwa mwaminifu kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na nitalinda na kuitetea KATIBA ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ewe Mwenyezi Mungu, nisaidie.

ii). Mimi John Pombe Joseph Magufuli NAAPA kwamba nitafanya kazi zangu za Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Uaminifu, kwa kutimiza wajibu wa kazi hizo kwa bidii na moyo mkunjufu, na kwamba nitawatendea HAKI watu wote kwa mujibu wa sheria, mila na desturi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila woga, bila UPENDELEO, dhuluma wala chuki. Ewe Mwenyezi Mungu nisaidie.

iii). Mimi John Pombe Joseph Magufuli, NAAPA katika kutekeleza madaraka niliyopewa kwa mujibu wa KATIBA ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ewe Mwenyezi Mungu nisaidie.’’ mwisho wa kunukuu.

Ndg. Rais, kiapo cha kwanza hapo juu kilikuwa ni kuhusu ‘kuilinda na kuitetea KATIBA’. Kiapo cha pili kilikutaka kutekeleza majukumu na madaraka yako kwa uaminifu, kwa bidii, kwa kutenda Haki na kwa kufuata SHERIA pamoja na kuepuka Upendeleo na chuki kwa yeyote. Nacho kiapo cha tatu ulichoapa, kilikusisitiza kutekeleza majukumu yako kwa kufuata KATIBA ya nchi.

Hata hivyo tunasikitika kwamba, tangu ukamate madaraka ya kuongoza nchi yetu, umekwishaonyesha Kwa dhahiri Viashiria vya Kukiuka Viapo vyote Hivyo zaidi ya mara moja, umevunja baadhi ya sheria zetu za nchi mara kadhaa, umetumia madaraka yako vibaya kwa lengo la kujinufaisha binafsi kisiasa, wewe na chama chako!- kwa hakika, umekiuka KIAPO ulichokula kwa Watanzania!
Hatua ya kwanza iliyoonyesha dalili mbaya za ukiukaji wa Katiba, ilikuwa ni kitendo cha serikali yako kuamua kuingilia Bunge na kulidhibiti ili lisiwe wazi na kuwajibika ipasavyo kwa umma. 

Serikali yako kupitia kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, ndugu Nape Nnauye, ilisema inasitisha urushaji Mubashara (Live) wa matangazo ya shughuli za vikao vya Bunge kwa hoja mbili dhaifu;

• Kwamba ni kutokana na gharama kubwa Za Kurusha Matangazo hayo ambazo ilidaiwa kuwa TBC (Televisheni ya Taifa) haizimudu tena.

• Kwamba matangazo ya Bunge yamekuwa yakiwafikia wananchi muda wa ‘kazi’.


Mbunge wa Kigoma Mjini ambaye pia ni Kiongozi wetu wa Chama, ndugu Zitto, alisimama BUNGENI na kupinga hatua hiyo ya kugeuza Bunge kuwa la giza,  akijenga hoja kuwa ni HAKI ya wananchi kupewa fursa ya kufuatilia moja kwa moja Baraza lao la Wawakilishi ili wawe na ufahamu wa kutosha juu ya masuala muhimu yanayowahusu na hivyo kuwa na uwezo wa kuwawajibisha wabunge na serikali yao.

Ndugu Zitto alisema kitendo cha serikali na uongozi wa Bunge kuweka vikwazo kwa matangazo ya Bunge kuwafikia wananchi kwa wakati, kinakwenda kinyume na Sera ya Kuendesha Serikali Kwa Uwazi (Open Government Policy), lakini zaidi kinavunja Katiba ya nchi ibara ya 18(d) inayotoa Haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na masuala muhimu kwa jamii. 

Ndugu Zitto aliieleza serikali na uongozi wa Bunge kwamba TBC inaendeshwa kwa ruzuku ya Serikali ambayo ni kodi za watanzania, hivyo si sahihi wala si haki kwa watanzania kunyimwa haki ya kujua kinachotokea Bungeni moja kwa moja kupitia Televisheni yao ya Taifa.

Hata hivyo, ilikuja kudhihirika baadaye kwamba hatua ya kuzuia matangazo ya Bunge Mubashara (Live), sababu haikuwa suala la gharama wala matangazo kwenda hewani muda wa kazi kama ilivyodaiwa na serikali. Televisheni mbili binafsi za Azam tv na Startv, hazikuhitaji malipo yoyote kutoka ofisi ya Bunge kwa ajili ya kurusha Mubashara (live) matangazo ya Bunge, lakini nazo zilinyimwa fursa hiyo!

Wakati hali ikiwa hivyo, Uongozi wa Bunge ulichukua hatua ya kumwadhibu Mbunge wa chama chetu kutohudhuria vikao vya Bunge kwa kile kilichoelezwa kwamba ni kutokana na ‘kufanya fujo’ Bungeni Siku ambayo alisimama ndani ya Bunge Letu Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kupinga Hatua hii ya Serikali yako ya Kulidhoofisha Bunge.

Baada ya Serikali kukosa majibu ya hoja za Ndugu Zitto, hoja zilizokuwa zimebeba Utetezi wa haki za wanachi kuonyeshwa Bunge lao, uongozi wa  Bunge Pamoja Na Serikali inayoongozwa Nawe, kupitia Kamati ya Haki na Maadili ya Bunge, uliugeuza jina mchango wa Zitto Kabwe na kuuita ‘fujo’ ili kuhalalisha dhamira hii ovu ya Kulidogosha Bunge, Kinyume Kabisa Na Katiba ambayo Uliapa kuilinda.

Ndugu Rais, kwa kitendo hicho, serikali yako ilinuia kukanyaga Katiba ya nchi kwa kuwanyima wananchi haki ya kufuatilia Mubashara (live) Bunge lao, huku wabunge waliosimama imara kutetea haki hiyo ya wananchi, serikali yako ilihakikisha wanadhibitiwa! Kwa Baraka zako mwenyewe, Demokrasia ndani ya nchi yetu iliwekwa kando nao utawala wa mabavu na ghiliba ukachukua nafasi. Matukio Haya yalikuwa Ishara thabiti Kuwa serikali yako imeamua kutawala nje ya Misingi ya Katiba Na Demokrasia ya Nchi yetu, Na Kuwa Wewe Binafsi umeamua kutokulinda Kiapo chako.

KUZUIA MIKUTANO YA HADHARA YA "OPERESHENI LINDA DEMOKRASIA"

Baada ya Kiongozi wetu wa Chama kufukuzwa Bungeni, yeye na chama chetu tuliamua kutumia haki yetu ya Kikatiba, Kufanya Mapokezi ya Kumpongeza Kwa Kitendo Chake Cha Kizalendo Cha kusimama Imara Kulinda haki za Wananchi BUNGENI, Pamoja na Kufanya Mikutano ya hadhara ili kuwaeleza wananchi dhamira chafu iliyojificha kimkakati ndani ya vitendo kandamizi vya serikali yako dhidi ya haki za wananchi na wawakilishi wa wananchi katika Baraza lao la Kutunga Sheria na kuisimamia Serikali.

Chama chetu kilifanya Mkutano mmoja wa Hadhara jijini Dar es Salaam katika viwanja vya Zakhem, Mbagala mnamo tarehe 05 Juni, 2016, ambapo mikutano mingine ilikuwa ifuate katika maeneo mengine nchini ikiwa ni utekelezaji wa “Operesheni Linda Demokrasia”.

Katika kufanya mkutano wetu, tulizingatia sheria na taratibu zote za nchi, tulitumia Haki yetu ya Kikatiba Kutoa maoni yetu Na Kwa dhahiri Kupinga Dalili Na Viashiria hivi vya kuminya demokrasia vilivyoanza kujionyesha nchini. Ni Katika mkutano huo ambapo pia tulipinga kauli yako ya kuwaita watoto wa Watanzania masikini kuwa Ni "VILAZA".

Lakini mara tu baada mkutano huo wa Mbagala, uliviamuru vyombo vya dola kumtia misukosuko Kiongozi wetu. Kiongozi wetu aliitwa polisi na kuhojiwa juu ya mambo aliyozungumza kwenye mkutano! Ilikuwa ni baada ya Mkutano huo, polisi walitoa tamko la kusitisha Mikutano yote ya hadhara ya vyama vya siasa nchini!

Pamoja na kutambua kuwa amri hii ya Jeshi la Polisi ilikuwa si amri halali na ni kinyume na katiba, Bado Viongozi wa Chama chetu waliweza kutumia busara na kututaka Vijana tusitishe kwa muda husika maandalizi ya mikutano ya hadhara ya "Operesheni Linda Demokrasia" yaliyokuwa yanaendelea.

KUZUIWA KWA HAKI YA MAWAZO MBADALA YA KISERA DHIDI YA SERA ZA SERIKALI - TAATHIRA ZA KUZUIA KONGAMANO LA UCHAMBUZI WA BAJETI YA SERIKALI YA 2016/17

Ndugu  Rais, Ishara ya pili ya nchi yetu kuendeshwa kinyume na katiba ni hatua ya Serikali ya Chama chako kuzuia Kongamano la Chama Chetu Kujadili Bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha wa 2016/17.

Ndugu Rais, wewe na Chama chako, kikatiba mnayo Dhamana ya Kuongoza Taifa hili Kwa miaka hii mitano, lakini Chama Chetu, Kikatiba Kinayo haki ya Kunadi Sera na mawazo mbadala juu ya namna njema ya kuongoza nchi yetu, ni haki ya Kikatiba na Kidemokrasia. Na si Ugomvi kwa  Chama Chetu kuainisha Sera mbadala dhidi ya sera za Chama Chako. Tukitambua kuwa vyama vyote nchini vina lengo moja tu, Kujenga Tanzania njema, kwa vizazi vya leo na Kesho - Tanzania yenye Utu, Uadilifu Na Uzalendo. Komredi Kwame Nkrumah alipata kusema "Vita Moja, njia tofauti za Kuikabili Vita".

Kwa muktadha huo, Chama chetu kiliona kinao WAJIBU - JAMII wa kuchambua Bajeti KUU ya Serikali yako Kwa mwaka 2016/17. Kwa lengo la Kushauri, kutilia mkazo, kupendekezo vyanzo mbadala vya mapato na pia kushawishi kuondoa kodi mbalimbali ambazo ni kikwazo kwa ukuaji wa Uchumi na zinawakandamiza Watanzania Wanyonge.

Pamoja na umuhimu wa Kongamano husika kwa Taifa, tuliona, nawe ukiwa Shuhuda, Serikali yako ilizuia kwa nguvu kongamano husika na hivyo kulinyima fursa Bunge letu tukufu, watunga Sera wetu, Serikali na Wananchi Kwa Ujumla kuijua Kwa Undani Bajeti ya Serikali ya Mwaka 2016/17 Kiasi Cha Bajeti iliyopitishwa na Bunge kutokueleweka na Watendaji wenyewe wa Serikali pamoja na Wananchi Kwa Ujumla.

Mfano Mkubwa wa hili ikiwa ni miongozo miwili tofauti ya Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Profesa Benno Ndullu na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini, ndugu Alfayo Kidata Juu ya Sintofamu ya Ukusanyaji wa Kodi (VAT) ya tozo za miamala ya simu na Ile ya kibenki. Gavana akiainisha Kuwa Kisheria VAT husika ni kodi anayotozwa mlaji (Mwananchi Mnyonge) huku Kamishna "akilazimisha" VAT husika yatozwe Mabenki na Makampuni ya Simu.

Sote tunajua, nawe Ndugu Rais ukiwa shahidi, Kuwa mpaka sasa suala husika halijapatiwa ufumbumbuzi, huku gharama za Maisha Kwa wananchi Wanyonge zikiwa juu kwa makato hayo ya Kodi.
Ni Imani yetu Sisi Vijana wa ACT Wazalendo, Kuwa Kama Kongamano letu la Kujadili Katiba lisingezuiwa basi sintofahamu hii isingekuwepo. Ni aibu Sana kwa Serikali, Kwa Gavana wa Benki Kuu na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Nchini kupingana Kwa Suala la Kikodi linalohusu Serikali Moja ambayo wote wawili ni watumishi.


Jambo hili linaonyesha kwa dhahiri kuwa Bajeti ya Serikali haikuwa Shirikishi, hakukuwa na Mjadala Mpana wa Bajeti husika. Chama Chetu kiliona ombwe hilo, Na ndio maana kiliona Umuhimu wa Kuandaa Kongamano lile. Hatua ya Serikali yako kulizuia Kongamano husika imekuwa na taathira kubwa sana kwa Taifa.
Lakini, si tu Serikali yako imesababisha athari Kubwa Kwa nchi Kwa kuzuia Kongamano lile, Lakini pia haikuwa, na bado haina msingi wowote wa Kisheria wa kuzuia Kongamano lile. Kwetu Vijana wa ACT Wazalendo tunaona tukio lile kuwa Ni muendelezo wa Kuminya demokrasia nchini na kuzuia mawazo mbadala.


ZUIO LAKO SI HALALI, UMELITIA GIZANI TAIFA

Ndugu Rais, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 19(1) inaeleza; ‘’Kila mtu anao uhuru wa kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kuchanganyika, kushirikiana na watu wengine, na kwa ajili hiyo kutoa mawazo yake hadharani na kuanzisha na kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo.”

Ibara hii ya Katiba ndio kiini na msingi wa mfumo wa demokrasia ya vyama vingi tunaoufuata hapa nchini. Itakumbukwa kwamba kurejeshwa kwa Mfumo wa Vyama vingi nchini mwetu pamoja na shinikizo kubwa la wanaharakati, kwa kiasi kikubwa ulifanikishwa kutokana na msukumo mahsusi wa hoja aliyoweka Baba wa Taifa. Utawala wa awamu ya kwanza chini ya Mwalimu Nyerere ndio uliofuta mfumo wa vyama vingi hapa nchini. Lakini ni Mwalimu Nyerere yule yule aliyelitambua hitaji la mfumo wa vyama vingi na akajisahihisha, kwa hekima ya pekee akaushawishi umma na watawala juu ya haja ya kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi.

 Mwalimu aliona mbali, akasahihisha makosa yake. Alitambua kwamba, chama kilichoko madarakani kinahitaji kupewa changamoto kutoka kwa vyama vingine ili kiwajibike ipasavyo kwa umma.

Mwalimu aliamini na kuutambua ukweli wa kifalsafa kwamba, tunamnukuu "Sharti moja la viumbe wote, hasa viumbe wenye nafsi, ni kuhitilafiana’".

Mwalimu alifahamu ya kwamba watu wote hatuwezi kuwa sawa. Tunatofautiana kifikra, kimawazo na hata kihisia. Kwa hiyo huwezi kumzuia mwingine kueleza kwa uhuru hisia, fikra na mawazo yake. ni ukweli huo wa kifalsafa ndiyo uliomfanya Baba wa Taifa letu kupigania urejeshaji wa mfumo wa vyama vingi ili mawazo ya watu yatolewe kwa uhuru kupitia vyama vya siasa na kwa jinsi hiyo yagongane na kuzaa mawazo na fikra bora zaidi zitakazolifaa taifa letu kupiga hatua za maendeleo.

Ndugu Rais, hatua zako binafsi na za serikali yako za kuminya haki na uhuru wa vyama kuwafikia wananchi na kufanya siasa kama KATIBA na Sheria zinavyoelekeza, inasaliti na kudharau maono ya Mwalimu Nyerere juu ya mfumo wa vyama vingi. Wewe umekuwa ni kiongozi usiyependa changamoto ya kifikra kutoka vyama vya upinzani. Unatumia vibaya vyombo vya dola kuukandamiza upinzani, kinyume kabisa na dhana ya Utawala Bora na Demokrasia.

Wakati ukituzuia sisi vyama vya Upinzani kufanya mikutano ya hadhara, wewe na kwa kofia zako mbili za rais wa Jamhuri na ile ya mwenyekiti wa chama chako, umekuwa ukifanya mikutano ya hadhara sehemu yoyote ya nchi utakavyo! Nayo televisheni ya Taifa TBC, ambayo serikali yako ilidai haina fedha za kurusha Mubashara (live) matangazo ya Bunge, imekuwa ikirusha matukio yako yote moja kwa moja tena mchana, siku na saa za kazi! Hii inaleta tafsri ya wazi kwamba kwa kweli umeamua ndani ya nchi hii usikilizwe wewe peke yako na mihimili mingine ya dola haina nafasi. Umelitia  gizani Taifa.

Huo ndio Uimla tunaoulalamikia, na ambao tunapenda ukomeshwe, kwa sababu ni hatari sana kwa mustakabali mwema wa Taifa letu. Huu ndio Uimla ambao ulitusukuma kuanzisha "Operesheni Linda Demokrasia" ili kuupinga.

Ndugu rais, tulisikitishwa na kufedheheshwa sana na agizo lako la kupiga marufuku viongozi wa kisiasa nchini kufanya mikutano popote nchini na kukutana na wanachama na wananchi kwa ujumla. Tunasema wazi, agizo lako halifai kwa nchi kama ya kwetu inayofuata mfumo wa siasa ya vyama vingi. Agizo lako linaifaa nchi kama Korea Kaskazini inayotawaliwa kwa uimla wa chama kimoja. Ni heri agizo lako hilo ungelipeleka kwingineko kunakohusika na si hapa nchini mwetu.

Ndugu Rais, Katiba na sheria zetu za nchi zimepiga marufuku kuwa na vyama vya kabila au eneo moja pekee ndani ya nchi. Leo hii, Chama chetu kina mbunge mmoja tu kutoka Kigoma Mjini. Kwa agizo lako, unamaanisha kwamba pamoja na kwamba mbunge wetu wa Kigoma mjini ndiye pia Kiongozi wetu wa Chama Kitaifa, ana ruhusa ya kufanya mkutano Kigoma Mjini peke yake. Haruhusiwi kwenda sehemu nyingine za nchi kuzungumza na watanzania na kutafuta wanachama wapya.

Vivyo hivyo na Mwenyekiti wetu wa Chama taifa, ambaye si Mbunge wala si Diwani, haruhusiwi kwenda kukutana na wanachama wake sehemu yoyote ya nchi maana yeye hana Jimbo wala Kata. Hii maana yake ni kwamba umeamua ACT kiwe ni chama cha Kigoma mjini tu, kinyume na matakwa ya Katiba ya nchi. Agizo lako litazaa vyama vya eneo moja tu na kabila fulani tu ndani ya nchi hii!

Ndugu Rais unaligawa Taifa na umeamua uligawe kwa nguvu zako zote ulizokabidhiwa na watanzania walioamini ungezidisha umoja ndani ya nchi! Katika dhamira yako hii tunakutaarifu kwamba, sisi vijana wa ACT Wazalendo, tunalipinga agizo lako maana linalipeleka Taifa Gizani.

KWA NINI TUNAKUKUMBUSHA UMUHIMU WA DEMOKRASIA?

Mbali na matakwa ya Katiba ya nchi, Misingi na Imani ya Chama chetu imejengwa katika himaya ya DEMOKRASIA. Sisi ni kundi la vijana ndani ya chama, ambao tunafunzwa na kulelewa katika maadili ya kuheshimu na kulinda Demokrasia. Chama chetu kinaamini kwa dhati kwamba, DEMOKRASIA ndiyo msingi wa Maendeleo, Umoja wa kitaifa na maelewano katika jamii ya watu waliostaarabika.

ACT Wazalendo inaamini kwamba msingi mama wa Demokrasia ni kuhakikisha kuwa wananchi wanakuwa huru na kwamba sauti zao zinasikika na kuzingatiwa katika mipango ya maendeleo ya nchi.  Jamii isiyofuata Demokrasia haina ustaarabu wala kuheshimiana. Maana watu wake kwa kuzuiwa kusema na kuzungumza, wanatunza na kulimbikiza hasira na vinyongo vifuani mwao.  Hasira na vinyongo hivyo vinapojaa kupita kiasi hulipuka na kusababisha zahama kubwa!

Jamii inayokanyaga Demokrasia, tena kwa makusudi kama unavyofanya sasa, ni jamii inayokaribisha mvurugano na machafuko kwa watu wake.


Sisi kama vijana tunaojitambua na kuelewa wajibu wetu kwa taifa, hatuko tayari kuona tukishinikizwa kwa kauli na vitendo vyako kuingiza taifa letu kwenye machafuko, kwa sababu tu ya jeuri na ubabe wako wa kutojali Haki na Uhuru wa vyama na makundi mengine ya kijamii ndani ya nchi yetu. Tunaamini, sote kwa umoja wetu ndani ya nchi hii, tuna dhamana ya amani na utulivu wa nchi yetu. Ndugu Rais, tunakusihi sana, acha demokrasia ichukue mkondo wake.

Ndugu Rais, Miongoni mwa Malengo ya chama chetu, ni pamoja na Kupigania na kulinda Uongozi bora na Utawala wa Sheria. Uongozi Bora na Utawala wa Sheria hujikita kwenye Kujenga, Kukuza na Kuendeleza Demokrasia ya vyama vingi, Kulinda Rasilimali za nchi na kuwa na Serikali inayowajibika kwa umma wa watanzania. 

Vitendo vyako vya kukandamiza Vyama vya Upinzani, na Sauti Mbadala, vinakwenda kinyume na Malengo hayo anuai ambayo ni muhimu na ya lazima kwa Ukombozi wa watu wa Taifa letu Kisiasa, Kiuchumi na Kiutamaduni.

Sisi tunaamini, hatuwezi kujenga Tanzania iliyo bora kwa kukandamiza maoni na fikra kinzani. Hatuwezi kujenga Tanzania yenye watu werevu na wanaoipenda nchi yao, ikiwa wamejawa na hofu mioyoni mwao kutokana na kuminywa kwa Uhuru wao wa kuzungumza. Ni dhahiri, ukandamizaji huu wa sauti kinzani ukiendelea tutazalisha taifa la watu wajinga wasio na uwezo wa kuhoji.

Ndugu Rais, tunapenda kuhitimisha barua hii kwa kukukumbusha kwamba nchi yetu ilikwishaamua kuwa na mfumo wa vyama vingi kama njia bora na sahihi ya kuyafikia maendeleo ya kweli na endelevu. Hatuhitaji ubabe na ghiliba vichukue nafasi badala ya ‘uwajibikaji’ kwenda sambamba na Demokrasia.

Tutakuunga mkono katika jitihada zote njema za kuleta mabadiliko chanya katika nchi yetu kwa kujenga mifumo na taasisi imara za uwajibikaji na utawala bora unaofuata sheria na katiba, kusimamia uadilifu na nidhamu katika utumishi wa umma, kupambana na rushwa na ufisadi, kubuni mbinu muafaka za kukuza uchumi wa nchi yetu na kutengeneza ajira kwetu vijana kwa kutekeleza sera nzuri ambazo tumekuwa tukipendekeza kwa maeneo mbalimbali ya uchumi.

Sanjali na nia njema na ya dhati kabisa tuliyonayo kwako, ndugu Rais hatuko tayari wala hatutakuwa tayari kuona unaendelea na vitendo, maagizo na kauli zako zinazovunja Katiba na sheria na zinazolenga kunyonga Demokrasia ya vyama vingi hapa nchini. Ili kuona kwamba una dhamira njema ya kujenga upya mifumo na muundo wa uongozi na jamii ndani ya taifa letu ili kuendana vyema na changamoto za karne ya leo na miaka mingi ijayo, tunakushauri na kukusihi sana, uongoze taifa kupata KATIBA mpya kwa kufufua mchakato wa upatikanaji wake kutoka ilipoishia iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya Jaji Joseph Warioba. Kwa kufanya hivyo, ni imani yetu utakuwa umelitendea haki taifa lako.

Tunakutakia kila la heri katika majukumu yako ya utumishi kwa watanzania na ujenzi wa Taifa. Pamoja, tunaweza kuibadilisha Tanzania kuwa mahali bora na salama zaidi.
Edna Sunga

Katibu Ngome Ya Vijana Taifa ACT WAZALENDO
12 Agosti,2016.

No comments: