Saturday, August 6, 2016

SERENGETI BOYS YAIDINDIA AFRIKA KUSINI


Ibrahim Abdallah wa Serengeti Boys akibanwa na Beki wa Amajimbos, Sechala Makoena 


Ikicheza mbele ya Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na Naibu Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Rosemary Chambe Jairo, timu ya soka ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 maarufu kama Serengeti Boys leo imegoma kupoteza mchezo dhidi ya wenyeji Afrika Kusini baada ya kuibana Amajimbos na kutoka sare bya bao 1-1.

Katika mchezo huo uliofanyika Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, Mji ulioko Kusini –Magharibi mwa jiji la Johannesburg, mabao yote yalipatikana kipindi cha pili yakiwa ni ya penalti kwa kila upande. Afrika Kusini walianza kupata penalti katika dakika 65 iliyofungwa na Linamandlia Mchilizeli kabla ya Ally Msingi kuisawazishia Serengeti Boys katika dakika ya 70.

Penalti ya Afrika Kusini ilitokana na mmoja wa mabeki wa Serengeti Boys kumfanyia madhambi Mchilizeli  wa Amajimbos ndani ya eneo la hatari wakati ile ya Serengeti Boys ilitoakana na beki Luke Donn wa Amajimbos kunawa mpira eneo la hatari.
Naibu Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Rosemary Jairo (wa pili kushoto) na Rais wa TFF, Jamal Malinzi wakiwa wamezungukwa na nyota wa Serengeti Boys.
Afrika Kusini iliyoanza kwa kasi dakika 10 za mwanzo wa mchezo huo, ilipotea dakika zote 30 za kipindi cha kwanza ambao kukosa bahati na umakini kidogo tu kwa nyota wa Serengeti Boys kulisababisha kukosa mabao matano yakiwamo mawili yaliyogonga mwamba hivyo kuwatia hasira Serengeti Boys ambao walionyesha kuwa na njaa ya mabao.

Kubanwa katika kipindi cha kwanza, kulisababisha Kocha Mkuu wa Amajimbos kufanya mabadiliko ya wachezaji wote watatu kipindi cha pili, wakati Bakari Shime kwa upande wake alimpumzisha Ibrahim na nafasi yake kuchukuliwa na Muhsin ambaye alisaidia kuendedlea kuwabana Afrika Kusini waliokjuwa wanawategemea nyota kama na Mswati Mavuso na Lethabo Mazibuko.

Shukrani za pekee zinaweza kwenda kwa Kipa Ramadhani Kabwili aliyeokoa hatari nyingi ikiwamo mpira uliokuwa unakwenda golini uliotokana na adhabu ndogo. Kadhalika Msengi aliyekuwa nyota wa mchezo huo akimiliki vema idarta ya ulinzi akishirikiaana nDickson Job.

Shime maarufu kama Mchawi Mweusi alisema: “Nashukuru kwa matokeo haya. Si mabaya kwangu. Tunarudi nyumbani kujipanga. Afrika Kusini ilikuwa inanitia hofu ndio maana nilisema mechi itakuwa ngumu.”

Kwa upande wake, Naibu Balozi Rosemary alisema: “Ahsanteni vijana (Serengeti Boys) kwa kulinda heshima yangu,” wakati Malinzi alisema: “Sina mengi. Mkiwafunga Afrika Kusini Agosti 21, 2016 kambi inapigwa tena nje ya nchi. Sijui ni nchi gani, lakini mtakwenda kujiandaa nje ya nchi.”

Katika mchezo huo, Kikosi cha Serengeti kilikuwa: Ramadhani Kbawili, Israel Mwenda, Nickson Kibabage, Ally Msengi, Dickson Job, Shaban Ada, Kelvin Naftal, Ally Ng’anzi, Ibrahim Abdallah/Muhsin Makame (Dakika ya 72), Asad Juma na Mohammed Rashid.

Afrika Kusini: Glen Tumelo, Mswati Mavuso, Luke Donn, Sechaba Makoena, Kwenzokuhle Shinga, Mjabulise Mkhize, Bonga Dladla, Linamandla Mchilizeli, Luke Gareth, James Monyane na Siphamandla Ntuli.

…..……………………………………………………………………………………………..
IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA

No comments: