Tuesday, October 11, 2016

Bodi ya Korosho yaendelea kulalamikiwa baada ya kushindwa kuwasilisha taarifa yake kwenye kikao cha kamati ya ushauri cha mkoa (RCC)



Na Mwandishi wetu,Habari24.blogsport.com
Wakati viongozi wa vyama vya msingi vya ushirika  (Amcos ) kutoka wilaya ya Tandahimba na Newala vikilalamika kutoshirikishwa katika mkutano mkuu wa wadau wa korosho uliofanyika mkoani Pwani, Mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego alisema mkutano huo kuacha kufanyika mkoani Mtwara na Lindi ambao ni wakulima wakubwa wa zao hilo ni kuwanyima wakulima fursa ya kushiriki kwa wingi.

Viongozi ao walikutana na mkuu wa mkoa na kutoa malalamiko mbalimbali yanayohusina na mfumo mzima wa korosho hasa kuondolewa kwa tozo tano.


Wakizungumza viongozi hao walidai kutoshirikishwa katika mkutano mkuu ambao pamoja na mambo mbalimbali ulitangaza siku ya kufunguliwa rasmi kwa msimu mpya wa korosho 2016/17 na kupanga bei dira ya zao hilo pia uliwapangia mambo yasiyotekelezeka hasa katika kutekeleza mfumo wa stakabadhi ghalani.

Akisoma taarifa kwaniaba ya viongozi hao, katibu wa makatibu wa Amcos wa wilaya ya Tandahimba, Kazumary Mkadimba alidai kuwa Tanecu ambaye ni msimamizi wa Amcos katika biashara ya korosho  hajatengewa ushuru wowote ndiye msimamizi mkubwa usimamizi wa mfuko wa stakabadhi ghalani licha ya kupangiwa majukumu pasipokuwa na fedha ya kujiendesha.

 “Tanecu ndiye msimamizi wa biashara ya korosho lakini hajatengewa pesa yoyote na ikizingatiwa ndiye msimamizi wa mfumo wa stakabadhi ghalani..hivi ni kweli kuna serikali inaweza kujiendesha pasipo mapato yoyote,na itawezaje kusimamia shughuli za maendeleo kwa watu wake,’alihoji  Mkadimba

Aidha katika taarifa yao waliyomsomea mkuu wa mkoa walidai kuwa bodi ya korosho imekuwa ikishindwa kuchukua hatua kwa watunza maghala ya kuhifadhi korosho zilizopotea katika maghala makuu tangu kuanzishwa kwa mfumo wa stakabadhi ghalani kufuatia upotevu wa korosho zaidi ya Tani 69.

Akizungumza mmoja wa wajumbe, Shahid Masumbuko alisema “CBT imekuwa ikishindwa kuwachukulia hatua wasimamizi wa maghala wanaopoteza korosho za wakulima, na sio kwamba zinapotea zimekuwa zikiibiwa na mtunza ghala kwani toka msimu wa 2007/2008, 2011/2012 na 2012/2013  zimepotea tani kadhaa za korosho lakini mpaka leo hatujapata haki zetu,”alisema Masumbuko

Akizungumza katika kikao cha ushauri cha mkoa (RCC) kuhusu mkutano huo kufanyika katika mkoa wa Pwani,mkuu wa mkoa alisema ni kuwanyima wakulima fursa ya kushiriki kwa wingi kwani asilimia 75 ya korosho zinalimwa mkoa wa Mtwara na Lindi.

"Kwa kweli mkutano mkuu wa wadau kwenda kufanyika Pwani na kuiacha mikoa  ya Lindi na Mtwara ambayo tunalima kwa asilimia 75 ya korosho sio kututendea haki, "alisema Dendego

Kwa upande wake mjumbe wa kikao hicho ambaye ni mbunge wa Jimbo la Ndanda,Cecil Mwambe alimwomba rais kuichukulia bodi ya korosho nchini  (CBT) hatua kwa kushindwa kuwasilisha taarifa yake katika kikao cha ushauri cha kamati ya mkoa (RCC) licha ya kuahirishwa mara mbili na kusema ni kuwadharau wajumbe wakiwemo wabunge wote wa Mtwara.

"Nasikitishwa na kitendo cha bodi ya korosho kwenda kufanyia mkutano Bagamoyo,ni sawa wanalima lakini asilimia 75 ya korosho inayozalishwa inatoka mikoa ya Lindi na Mtwara..lakini tulitegemea katika kikao cha RCC tuone bodi ikileta ripoti yake kwaajili ya mipango ya msimu ujao wa korosho ambao mnada utakuwa hivi karibuni lakini matokeo yake wameshindwa kuleta taarifa na ndio maana kila mara tunalalamika bodi haina uwezo kwasababu hata watendaji wake hawana uwezo wameshindwa kumshauri mtendaji mkuu kuleta taarifa ya ununuzi wa korosho msimu wa 2016/17,"alisema Mwambe

No comments: