Tuesday, October 25, 2016

LHRC WATOA TAMKO KUHUSU MUINGILIANO WA MADARAKA BAINA YA MIHIMILI YA SERIKALI


 

TAMKO KWA VYOMBO VYA HABARI
MUINGILIANO WA MADARAKA BAINA YA MIHIMILI YA SERIKALI
Ndugu Wanahabari,
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu ni shirika lisilo la kiserikali ambalo si la kisiasa wala kibiashara lenye kujibidiisha katika kutetea, kulinda na kuendeleza haki za binadamu na utawala bora nchini. Kituo kwa kupitia dawati la uangalizi wa haki na maboresho kwa mahakama limekuwa likifuatilia mwenendo wa dhana ya uhuru wa mahakama katika mgawanyo wa madaraka wa mihimili mitatu ya dola yaani serikali, bunge na mahakama. 

Mahakama ni muhimili wa dola ulioundwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977.  Ibara ya 107A (1) inasema kwamba mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakuwa ni mahakama. Pia katika Ibara ya 107B ya Katiba imeipa mahakama mamlaka ya kuwa chombo huru, ibara hii inasema kwamba katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya katiba na yale ya sheria za nchi.


Ndugu Wanahabari
Katika siku za hivi karibuni tumeshuhudia mhimili wa serikali ukiingilia utendaji kazi wa mhimili mwingine wa dola yaani mahakama. Kumekuwepo na kutolewa na matamko mbalimbali ambayo yanaashiria mhimili wa utawala/serikali ukiingilia uhuru wa mahakama. Mnamo tarehe 4 Februari, 2016 katika maadhimisho ya siku ya sheria ‘Law Day’ katika hotuba ya  mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliitaka mahakama kuamua kesi za kodi zipatazo 400 zilizopo mahakamani ambazo alidai zikiendeshwa ipasavyo basi serikali inaweza kujipatia kiasi cha trilioni moja. Agizo hili linaonyesha kuwa kesi zote hizo lazima zishinde bila kujali kuwa mahakama inaongozwa na mambo mengi kufikia uamuzi na hasa ushahidi ulioko mbele yake.

Pia tumesoma katika gazeti la Mtanzania la tarehe 11 Julai, 2016 Mkuu wa Wilaya ya Mwanga akidaiwa kumwandikia barua yenye kumbukumbu namba CAB 40/229/01/25 ya tarehe 8 Julai, 2016 Hakimu Mfawidhi wa Wilaya ya Mwanga kutaka taarifa mbalimbali za kesi zinazoendeshwa mahakamani kila mwezi.  Barua hiyo ilitaka taarifa mbalimbali za mahakama zikiwamo idadi ya kesi zilizopo, zilizosikilizwa na changamoto zilizojitokeza zikiwamo za sheria, fedha na vitendea kazi kinyume na Ibara ya 107B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inayosema katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya Katiba na yale ya sheria za nchi. Agizo hili ni kinyume na Katiba na ni kuingilia uhuru wa mahakama.

Katika tukio jingine tarehe 12/10/2016 tumeshuhudia mkuu wa wilaya ya Kinondoni akimwamuru mwenyekiti wa baraza la ardhi la wilaya Kinondoni kwamba shauri no 331/2014 lisikilizwe upya baada ya mlalamikaji katika shauri hilo kutoridhishwa na maamuzi ya baraza la ardhi la wilaya. Iwapo mlaalmikaji hakuridhika na uamuzi wa mahakama anapaswa kukata rufaa au kufuata taratibu nyingine za kumahakama na si mtawala wa seriakali kutoa maagiza kwa mahakama.

Ndugu Wanahabari
 Kituo cha sheria na haki za binadamu kinatoa mapendekezo yafuatayo.

i.                    Mhimili wa serikali katika kutekeleza majukumu yake izingatie sheria na katiba ya nchi na kusiwepo na kuingilia uhuru wa mahakama kama ilivyoanishwa katika Ibara ya 107B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

ii.                  Serikali, Bunge na Mahakama kuheshimu na kuzingatia dhana ya mgawanyo wa madaraka na pasiwepo mhimili mmoja kuingilia mhimili mwingine.
iii.                Ibara ya 107A ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 imeipa mahakama mamlaka ya mwisho ya utoaji haki hivyo kusiwepo na chombo chochote kitakachoingilia kazi ya mahakama. Masual ya kimahakama yafuatiliwe kimahakama na si vinginevyo
iv.                Tungetegemea Jaji Mkuu kutoa muongozo na kuzungumazana na seriakali katika suala hili ili kuweka msimamo katika misingi ya kisheria na kikatiba.

Imetolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu

Dkt. Helen Kijo-Bisimba
Mkurugenzi Mtendaji.
.


No comments: