Monday, October 24, 2016

SIMBA YAITANGAZIA VITA STAND UNITED,MGOSI SISI NI BORA KULIKO TIMU YOYOTE MSIMU HUU.

Na.Alex Mathias,Dar es salaam.
Baada ya kupata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Toto African ‘wana-kisha mapanda’ uongozi wa Simba umetoa onyo kwa timu za kanda ya ziwa kuwa wajianadae nao kupokea kichapo huko huko kwao kwani wekundu hao wataanza safari kesho kuwafuata Stand na Mwadui FC michezo ya Ligi kuu ya Tanzania.

Akizungumza Meneja wa Simba,Mussa Hassan Mgosi,amesema kuwa kwanza wanamshukuru Mungu kwa kuendelea kuwabariki na kupata matokeo mazuri kwenye Ligi hata hivyo mshikamo kwa wanachama pamoja na sapoti ya mashabiki ni chachu kubwa ya wao  kupata alama tatu muhimu kwa kila timu wanayokutana nayo.
“Dhamira yetu msimu huu ni kuchukua ubingwa ambao tumeukosa kwa misimu minne ndio maana tukimaliza mchezo huwa tunawahimiza wachezaji wetu kuwa dhamira ya klabu ni kuchukua ubingwa na sio kushinda tu na ukizingatia tumejipanga kupambana ili tuweze kuvuna alama nyingi na pia tunaangalia mashindano ya kimataifa”alisema Mgosi
Aidha Simba anatarajia kuanza safari kesho kuwafuata Stand na Mwadui FC zote za mkoa wa Shinyanga na wataanza na Stand katikati ya wiki hii katika mzunguko wa 12 wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara.
Simba mpaka sasa ndio kinara wa Ligi wakiwa wamecheza mechi 11 na kujikusanyia alama 29 kwenye msimamo na hawajapoteza mchezo wowote tangu msimu huu uanze wakiwa chini ya kocha mtaalamu Joseph Omog akisaidiwa na Jackson Mayanja,ngoja tusubiri atauweza mfupa ulioshindwa kutafunwa na Yanga na Azam FC kwa timu ya Stand United ambayo imekuwa mwiba kwa vigogo kwa kushusha kipigo tena wakiwa kwenye uwanja wao wa CCM Kambarage.

No comments: