Monday, October 10, 2016

Watu zaidi ya 400 wanasubiri kunyongwa Tanzania,LHRC waendelea kupinga adhabu ya kifo,Hii hapa Kauli yao leo

1
  Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk.Helen Kijo- Bisimba (katikati), Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Uwajibikaji, Imelda Urio (kulia) na Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa LHRC, Anna Henga , wakionesha jarida la kupinga adhabu ya kifo wakati wa uzindi wake Dar es Salaam leo.
 Wakati leo ulimwengu mzima ukiadhimisha siku ya kupinga Adhabu  ya kifo kituo cha sheria na haki za Binadamu nchini Tanzania LHRC wameendelea kusisitiza kuwa ni wakati sasa wa  serikali kufuta adhabu hiyo  ambayo ipo na kutafuta adhabu mbadala kwenye makosa ya jinai na kwa wafungwa waliopo,vikiwemo vifungo vya muda mrefu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk.Helen Kijo- Bisimba (kushoto), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam leo, wakati akisoma tamko la kupinga adhabu ya kifo. Kulia ni Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Uwajibikaji, Imelda Urio na kushoto ni Mkurugenzi wa Utetezi na Maboresho wa LHRC, Anna Henga.

Akizungumza na wanahabari leo makao makuu ya shirika hilo Kijitonyama Jijini Dar es salaam Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC Bi Hellen Kijo Bisimba amesema kuwa adhabu ya kifo ni adhabu ambayo inakwenda kinyume na haki za Binadamu,ambapo amesema kuwa adhabu hiyo imekua ikiathiri kwa kiwango kikubwa haki ya msingi ya kuishi kwa kuwa ni adhabu inayodhalilisha utu wa Binadamu.



Ameongeza kuwa Tanzania imeridhia mikataba mbalimbali ya kikanda na kimataifa ambayo inaweka wajibu wa kulinda haki hiyo pamoja na kuipa ulinzi ndani ya sheria za nchi ambapo ametaja mikataba hiyo kuwa ni pamoja na Tamko la kimataifa la haki za Binadamu la mwaka 1948 ibara ya 3,Mkataba wa haki za kiraia na kisiasa wa mwaka 1966 (ICCPR) ambao katika ibara ya 6 umeeleza bayana kwamba “Kila mtu anayo haki ya asili ya kuishi haki hii italindwa chini ya sheria na mtu yeyote hatakuwa na mamlaka kuondoa uhai wa mtu kiholela” huku pia mkataba wa Africa wa haki za binadamu na haki za watu wa mwaka 1981 nao katika ibara ya 4 imeanisha “kila binadamu anastahili heshima ya utu wake na haki hiyo haipaswi kuvunjwa”
Ameongeza kuwa kutokana na mkikataba hiyo ambayo Tanzania ni mmoja kati ya mataifa yanayofwata ni lazima tuondoe adhabu ya kifo nchini kwani inakwenda kinyume na mikataba hiyo ya kimataifa na kikanda.



Aidha ameongeza kuwa adhabu ya kifo nchini Tanzania haikuanzia nchini kwetu bali ni sheria ambayo ililetwa na wakoloni ambapo adhabu hiyo imeainishwa kwenye sheria ya kanuni ya adhabu sura ya 16 “Penal Code” ambayo nayo ililetwa na utawala wa kikoloni mwaka 1945 na kuendelea kuwa moja ya sheria zetu hata baada ya uhuru wa Tanzania licha ya marekebisho ya mwaka 2002.

Takwimu zinaonyesha kuwa hadi kufikia mwaka 2015 jumla ya watu 472 walikuwa wamehukumiwa kunyongwa ambao kati yapo 452 ni wanaume na 20 ni wanawake,na kati ya hao wanaosubiri kunyongwa ni 228 na wengine 244 wanasubiri maamuzi ya Rufaa zao.ambapo licha ya adhabu kutokutekelezwa nchini kwa Takribani miaka 22 na miaka 24 ya kwanza ya uhuru Taarifa zinaonyesha kuwa ni watu 72 ambao walishawahi kunyongwa kutokana na adhabu hiyo..

Akitaja sababu ambazo zinawafanya wanaharakati hao kupinga adhabu hiyo ya kifo Bi Hellen Kijo Bisimba pamoja na sababu nyingi ambazo wamezitaja amesema kuwa adhabu ya kifo ni adhabu ya kinyama,na isiyo na staha,ni adhabu ya kibaguzi maana wanaopatikana na hatia na kupewa adhabu hii mara nyingi huwa ni maskini wasioweza kuwa na mawakili,lakini pia hakuna ushahidi wa moja kwa moja ambao unaonyesha kuwa adhabu hii inazuia watu wengine kutokutenda makosa kama hayo.
Wanahabari wakichukua Taarifa Hiyo
Wakati tukiadhimishwa adhabu hii ya kifo nchini Tanzania Taarifa   zinaeleza kuwa duniani kote adhabu hii imeshafutwa katika mataifa yapatayo 140 na kwa mujibu wa shirika la kimataifa la Amnesty kati ya nchi hizo 140 nchi 17 ni nchi za Africa zikiwemo Rwanda,Burundi,Msumbiji,Visiwa vya shelisheli,na Madagascar,Namibia,na Africa kusini pamoja na nchi nyingine,jambo ambalo LHRC wanaeleza sasa ni wakati wa Tanzania kuiga mfano huo na kufuta sheria hiyo Kandamizi na kutafuta mbadala wa adhabu nyingine kali kwa watuhumiwa wa makosa makubwa.

No comments: