Wednesday, January 18, 2017

ACT WAZALENDO WAPIGILIA MSUMARI MWINGINE SAKATA LA NJAA TANZANIA-SOMA HII YA LEO


Taarifa za Serikali juu ya Baa la Njaa Nchini Zinajikanganya

Ndugu Watanzania

Kupitia mikutano ya Kampeni za uchaguzi mdogo zinazoendelea huko Dimani (Zanzibar) na katika Kata mbalimbali hapa Tanzania Bara, chama chetu cha ACT-Wazalendo, pamoja na mambo mengine, tumekuwa tukieleza hatari ya njaa ambayo inaikabili nchi yetu hivi sasa. Tumekuwa tukianisha kwa takwimu kupanda kwa bei za vyakula na kiwango kidogo cha akiba ya chakula kwenye maghala ya Taifa (NFRA), mambo ambayo yameongeza mno gharama za maisha kwa wananchi. 

Jana Waziri wa Chakula ameeleza kuwa gunia la mahindi la kg 100 linauzwa kwa shilingi 150,000/- huko mkoani Mara kutoka bei ya shilingi 65,000/- iliyozoeleka. Hali iko hivyo katika maeneo mbalimbali nchini.

Jana pia Mkuu wa Wilaya ya Longido, ndugu Daniel Chongolo alinikukuliwa akisema yafuatayo "Msimamo wangu siombi Chakula cha bure au cha njaa, bali Serikali itupatie chakula cha bei nafuu".

Tunampongeza sana DC Chongolo kwa ujasiri na uwazi wake mkubwa sana, hasa katika kipindi kama hiki ambacho Rais alishatishia kumfukuza kazi Mkuu wa Wilaya yeyote atakayeripoti juu ya uwepo wa njaa kwenye Wilaya yake. Ndugu Chongolo ametuonyesha kuwa 'maisha ya watu wetu ni muhimu kuliko vyeo vyetu', hasa katika Wilaya kama Longido ambayo imeripotiwa kuwa watanzania wenzetu zaidi ya 16,000 wako katika hatari kubwa ya baa la njaa na ikiwa wameshapoteza maelfu ya mifugo yao kwasababu ya ukame, na sasa wamefikia hatua ya biashara ya wakati wa Ukoloni ya 'Barter Trade' ya kubadilishana mifugo yao kwa chakula. Hali hii inasikitisha sana.


Pamoja na serikali kukana uwepo wa hatari ya njaa nchini, wananchi wenyewe ni mashahidi. Mwenye njaa hahitaji kuambiwa ana njaa. Njaa ni hali halisi na sio jambo la kuambiwa au kutangaziwa. Tunawapongeza sana Viongozi wetu wa Dini kwa kutoa matamko ya kuhamasisha watanzania kuliombea Taifa ili tuweze kukabiliana na njaa. Viongozi wa dini wameonyesha utu na uwezo mkubwa wa uongozi wa kutafuta jawabu la mwenyezi mungu kuhusu kadhia hii.


Tunampongeza pia Waziri Mkuu kwa namna alivyoonyesha uongozi kwa kukiri kwake 'kiutu uzima' juu ya uwepo wa tishio la njaa, na tunapongeza hatua ambazo yeye na Waziri wa Kilimo wameahidi kuzichukua katika kuhakikisha kwamba watanzania hawafi kwa njaa.


Hata hivyo, tunapingana nao juu ya propaganda ya kusambaza Tani Milioni 1.5 za chakula ambazo Serikali imeahidi kuzisambaza katika maeneo yote yanayotajwa kuwa na tishio la njaa. Ukweli ni kwamba chakula pekee ambacho serikali inakimiliki na ina uwezo wa kukisambaza ni kile kilicho NFRA, ambacho mpaka mwezi Oktoba kulikuwa ni tani 90,476 tu. Serikali inatoa wapi hizo tani milioni 1.5? Je, Serikali inaahidi kusambaza chakula hewa?


Na hatushangai, maana hata hali hii ya tishio la njaa tuliyonayo sasa ina mchango wa Serikali yenyewe. Kwa mujibu wa Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa iliyotolewa na Serikali yenyewe kupitia Wizara ya Fedha na Mipango mwezi Juni, 2016, uzalishaji wa Mahindi ulipungua kwa 12.3% msimu uliopita. Mazao Kama Ngano na Mtama/Uwele yalipungua uzalishaji kwa 57% na 19% kwa mfuatano huo. 


Serikali inapotuambia kuwa kulikuwa na ziada ya chakula tani 3m haisemi ukweli wote. Mchele tu Ndio uzalishalishaji uliongezeka kwa 15%. Serikali ilitoa Vibali vya kuuza mchele nje baada ya kuwa soko la Ndani limejaa mchele kutoka Pakistan na kadhalika. Ukiongeza na vibali vya Mahindi (au unga wa mahindi ) utaona kuwa kuna kila sababu ya kutaka ukaguzi maalumu wa CAG kwenye mchakato wa utoaji wa vibali vya kuuza nafaka nje ya nchi.


Tunaiomba ofisi ya CAG ifanye ukaguzi maalumu kukagua vibali vya kuuzwa chakula nje ili kujua ukweli wa jambo hili. Jambo hili likithibitika kuwa ni kweli ni wazi kuwa serikali itabidi iwajibike kwa kuweka mbele maslahi ya kibiashara badala ya maslahi ya maisha ya wananchi. 


Jana Pia, Chama cha Mapinduzi, kupitia Katibu wao wa uenezi, kimevituhumu vyama vya upinzani kutumia matatizo ya wananchi kama mtaji wa kisiasa. Sisi kama cha siasa kinachofuata falsafa ya ‘Siasa ni Maendeleo’, tunaamini kwamba chama cha siasa lazima kihangaike na matatizo ya wananchi. Tunaamini kabisa kwamba kukabiliana na matatizo ya wananchi ndiyo mtaji sahihi wa kisiasa kwa chama cha siasa. Baba wa Taifa, ambaye ndiyo muasisi wa CCM, aliwahi kusema mara nyingi kuwa “Chama cha siasa lazima kishughulikie matatizo ya wananchi. Chama cha siasa kisichojihangaisha na matatizo ya wananchi kitakufa”. 


Mtaji wa CCM mpya ni dola. Sisi mtaji wetu wa kisiasa ni kuhangaika na matatizo ya wananchi. Sasa hii CCM mpya ya akina Polepole isitulazimishe tuwe kama wao. Wao waendelee tu kuitetea dola na serikali yao. Sisi tutaendelea kuwatetea wananchi kwa bidii na heshima kubwa.


Tunaikumbusha CCM kutekeleza jukumu lake la msingi la kuisimamia serikali badala ya kuhangaika na vyama vya upinzani vinavyotekeleza wajibu wake wa kikatiba na kisheria. Hasira na vijembe havisaidii kutatua matatizo ya wananchi, ikiwemo njaa. Uongozi ni dhamana. 


Wamekabidhiwa dhamana na wananchi na sisi ni jukumu letu kuibana serikali kutekekeza wajibu wake. Kwamba CCM imewekwa mfukoni mwa serikali haituhusu. Sisi tutaendelea kutekeleza wajibu wetu wa kuikosoa serikali kila inapobidi na kuwatumikia wananchi kwa bidii na heshima bila woga.



Ado Shaibu

Katibu - Kamati ya Itikadi, Mawasialiano ya Umma na Uenezi, ACT Wazalendo

Dar es salaam

Januari 18, 2017.

No comments: