Thursday, January 5, 2017

JULIUS MTATIRO--NJAA SIYO PEPO, HAIONDOKI KWA KUKEMEWA!



Rais wetu ashauriwe upya juu ya msimamo wake kuhusu maeneo yenye njaa. Mkoani Mara, baba yangu amekuwa akilima zaidi ya ekari 10 za Mahindi kwa miaka 4 mfululizo, ni hasara tupu. Hakuna mavuno kwa sababu hakuna mvua za kuhimili misimu ya kilimo. Na hata wakulima wakifuata majira ya mvua "wanaingia mkenge", hayafuatiki, hayaeleweki na hayatabiriki.

Gunia la Mahindi mkoani Mara ni wastani wa Shilingi 100,000 kwa sasa. Gunia la Muhogo na Mtama ni wastani wa Shilingi 62,500. Hali hii ina maana Wakuu wa Wilaya hawana miujiza ya kutekeleza amri ya mkuu ya kuondoa njaa kirahisi. Tatizo la ukosefu na upungufu wa chakula linakua kubwa kila uchwao kwa sababu kadhaa;
#Mojawapo ni Mvua kutonyesha kwa sababu tumekata miti yote, tunaendelea kuikata na hatuna mpango mahsusi wa kupanda miti.
#Sababu ya pili ni kukosekana kwa mipango yoyote ya kukuza kilimo cha umwagiliaji, kama hitaji la kilimo cha umwagiliaji wa kisasa ni asilimia 100, Tanzania tumeweza chini ya asilimia moja.
#Tatu ni suala la kipaumbele cha kilimo, kilimo kimesahaulika na kutupwa mbali kabisa. Ni mhimili wa maisha kwa asilimia 70 ya Watanzania wote lakini hadi sasa kinachangia asilimia chini ya 3 ya pato la taifa.
#Nne, serikali ya awamu ya sasa haina kipaumbele cha kitu kiitwacho kilimo, awamu hii ni viwanda ambavyo haieleweki vitaimarishwa namna gani bila kujengwa juu ya msingi wa kilimo.
#Tano, bado hadi sasa sehemu kubwa ya Wakulima wanatumia jembe la mkono, sawa na enzi za Ujima. Jembe hilo halifui dafu utoshelezaji wa chakula kutokana na ongezeko kubwa la watu.
Rais wetu akumbushwe suala la njaa ni mtambuka na halitatatuliwa kwa amri tu, linahitaji mipango ya muda,mrefu, uwekezaji wa trilioni za shilingi na utashi mkubwa wa kisiasa wa serikali yake na zijazo.

No comments: