Thursday, January 26, 2017

WAKAZI WA MWANAGATI HATARINI KUPATA MARADADHI YA KANSA

Kiwanda kinacholalamikiwa na wakazi wa Mwanagati ambacho kimejengwa katika makazi ya watu kikiwa kimezungushiwa fensi ya ukuta.

Wananchi wa Kitunda Mwanagati waishio Block 5 na 6 wako katika hatari kubwa ya kupata magonjwa ya Kansa na Kifua kikuu kutokana na uwepo  wa Kiwanda cha kuyeyusha taka za plastiki kilichojengwa katika eneo hilo ambalo ni makazi ya watu kwa takribani miezi mitano sasa.

Kiwanda hicho ambacho kimejengwa katika viwanja namba 133 na 135 block 5 kimekuwa ni tishio kubwa kwa afya za wakazi wa maeneo yanayozunguka na yale yaliyo jirani na kiwanda hicho kutokana na kuzalisha harufu mbaya na kali inayochafua hewa (air pollution) hali ambayo imesababisha baadhi ya wakazi wa maeneo hayo kulalamika kuanza kuathirika na hali hiyo kwa kuugua kifua, tumbo, kichefuchefu na kupungukiwa hamu ya kula.

Wamedai kuwa  kiwanda hicho kimekuwa kikifanya kazi mchana kutwa na usiku na wakati mwingine kinafanya kazi mpaka usiku kucha mpaka asubuhi.  Mbali ya kuchafua hewa kiwanda hicho kimekuwa pia kikisababisha makelele hususan kwa wale walio jirani kabisa na kiwanda hicho na kuwafanya kushindwa kupumzika vizuri majumbani mwao.
 “ Kiwanda hiki kinahatarisha sana afya zetu  kwani kinasabisha tuvute hewa chafu na mbaya sana  kiasi ambacho familia zetu zimeanza kuugua, tunanyemelwa na magonjwa ya kansa na kifua kikuu ” alilalamika mkazi mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja tu la Onesmo. 

Naye mkazi mwingine jirani na kiwanda hicho Bw. Solomoni Mbalaje alisema hali ni mbaya sana kwani mke wake kwa sasa ni mgonjwa na kutokana na harufu kali inayozalishwa na kiwanda hicho hatoki nje badala yake amekuwa akishinda ndani tu. Amesema kuwa mmiliki wa kiwanda hicho ambaye haishi Mwanagati huleta malori yaliyojaa  takataka za plastiki kama vile chupa za maji na mifuko ya plastiki iliyotumika kutoka maeneo mbalimbali hapa Dar es salaam na mikoani na kuyayeyusha kiwandani hapo.


Taarifa zinasema kuwa wakazi wa maeneo hayo ya block 5 na 6 walifikisha malalamiko yao katika ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Mwanagati ambapo baada ya kikao cha pamoja na mmoja wa wamiliki wa kiwanda hicho ilibainika kuwa hawana kibali cha Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira –Nemc na hawana pia hati ya Wizara ya Ardhi ya kubadilisha matumizi ya eneo hilo kutoka makazi kuwa kiwanda. Hata hivyo Serikali ya mtaa wa Mwanagati ilishindwa kushughulikia suala hilo na kuamua kulipeleka kwa Mtendaji wa Kata ya Mzinga ambako mpaka leo hakuna hatua yeyote iliyochukuliwa.

Aidha wakazi wa maeneo hayo wanadai kuwa wamepeleka malalamiko yao kwa Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira na kwamba bado wanasubiri kupata majibu kabla ya kuamua ni hatua gani zaidi wachukue.



No comments: