Saturday, February 18, 2017

KIPINDUPINDU CHAPIGA HODI JIJINI DAR ES SALAAM CHAUA MTU MMOJA WENGINE 12 WALAZWA HOSPITALI

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.

 Na Dotto Mwaibale

WAKATI jiji la Dar es Salaam likiwa katika  mapambano ya kukabiliwa na dawa za kulevya jiji hilo limekumbwa na ugonjwa wa kipindupindu ambapo mtu mmoja aliyetajwa kwa jina la Ramadhan Kiumbo (maarufu kwa jina la Popo) mkazi wa Kibada Kigamboni amefariki kutokana na ugonjwa huo.

Akizungumza Dar es Salaam leo ndugu yake na marehemu huyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Issa alisema ndugu yao huyo alifariki jana wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Kigamboni ya Vijibweni.

"Ndugu yetu amefariki kutokana na ugonjwa wa kipindupindu na amezikwa leo 'jana' na Halmshauri ya Wilaya ya Kigamboni katika makaburi ya Serikali ya Kisiwani na kuhudhuriwa na ndugu wachache" alisema Issa.

Issa aliongeza kuwa katika Hospitali hiyo kuna wagonjwa 12 wanaotibiwa ugonjwa huo na tayari imeanzishwa kambi maalumu ya wagonjwa hao katika hospitali hiyo ya Vijibweni.

Alisema kutokana na kuibuka kwa ugonjwa huo shule zote za Halmashauri ya Kigamboni zilifungwa siku ya Ijumaa kwa hofu ya wanafunzi kupata maambukizi.

"Siku ya Ijumaa wanafunzi walirudishwa nyumbani na tulipowauliza walisema shule zimefungwa kutokana na ugonjwa wa kipindupindu" alisema Issa.

Baadhi ya maeneo ambayo yametajwa kuwa na ugonjwa huo ni pamoja na Vingunguti na Temeke.

Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Hashim Mgandilwa alithibitisha kuwepo kwa ugonjwa huo ndani ya manispaa yake ambapo mtu mmoja ameshafariki huku wengine wakiwa Hospitalini wakipatiwa matibabu.

" Ni kweli ugonjwa huu umeingia lakini tumefanya uchunguzi na kugundua umeanzia sehemu moja inaitwa Kichangani ambapo watu wote ambao wameletwa Hospitali waliupatia eneo hilo walipoenda kwenye msiba.

" Lakini tayari maofisa wetu wa afya wameshachukua hatua za awali za kukabiliana na ugonjwa huu kwa kutembelea nyumba za wagonjwa hao na kupulizia dawa ili kuweza kuzuia maambukizi kwa watu wengine," alisema Mgandilwa.


No comments: