Thursday, February 9, 2017

Mahakama yatupilia mbali pingamizi la Lema

Arusha. Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, imetupa pingamizi la mawakili wa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema la kuitaka isisikilize kesi ya kuhamasisha maandamano ya Ukuta, bali kwanza ifikishwe Mahakama ya Katiba.


Lema, ambaye ni mbunge kupitia Chadema, anakabiliwa na kesi hiyo akidaiwa kuhamasisha maandamano hayo ya chama chake yaliyokuwa yamepangwa kufanyika Septemba Mosi, mwaka jana.

Mawakili wa Lema, John Mallya na Sheck Mfinanga,  waliwasilisha ombi mahakamani hapo wiki iliyopita wakitaka kesi hiyo isikilizwe Mahakama ya Katiba kwa kuwa kuna hoja za kikatiba ambazo zitahitaji kutolewa maelezo na majaji watatu wa Mahakama hiyo.

Katika kesi hiyo, Lema anadaiwa kuhamasisha maandamano kwa njia ya mtandao wa kijamii (audio clip) aliyoitengeneza na kujirekodi ujumbe mfupi wa sauti na kisha  kusambaza  Agosti Mosi hadi 26, mwaka  jana katika mitandao ya kijamii ya WhatsApp.

Hakimu Bernard Nganga alisema kosa alilofanya Lema siyo la kikatiba na hoja za kutaka kuhamishiwa shauri hilo Mahakama ya Katiba hazina mashiko kisheria.

Alisema sheria ipo wazi, kuwa mtu yeyote akihusika na kushawishi utendaji wa kosa hata kama halina madhara, muhusika ana makosa na adhabu yake ni kifungo cha miaka miwili au kulipa faini.

No comments: