Monday, July 24, 2017

INGIA HAPA KUANGALIA KILICHOMKUTA LISSU LEO MAHAKAMANI

Leo July 24, 2017 Mbunge wa Singida Mashariki ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA na Rais wa Chama cha Mawakili Tanganyika Tundu Lissu amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa shtaka moja la kutoa lugha ya uchochezi.

Wakili wa Serikali Mutalemwa Kishenyi alimsomea Tundu Lissu shtaka hilo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Wilbard Mashauri ambaye alidai Lissu alitoa maneno ya uchochezi July 17, 2017 maeneo ya Ufipa Dar es Salaam.
Baada ya kusomewa shtaka hilo, Lissu ambaye anatetewa na Mawakili 18 wakiongozwa na Fatuma Karume, alikana kosa hilo ambapo hata hivyo, Wakili wa Serikali, Wankyo Simon aliiomba Mahakama kumnyima dhamana Lissu kwa madai kuwa amekuwa akitenda makosa ya namna hiyo kila wakati ikizingatiwa ana kesi nyingine nne Mahakamani hapo.
Aidha, Wakili mwingine wa Serikali, Tulimanywa Majigo alidai mshtakiwa anapaswa kunyimwa dhamana kwa kuwa akirudi uraiani anaweza kudhurika huku akisema ulinzi na usalama wake ni muhimu kutokana na maneno yake kuwakera wengi na mbali ya usalama wake yanaweza kubomoa misingi ya umoja, mshikamano na upendo uliojengeka kwa Watanzania.
>>>”Mahakama hii inatekeleza majukumu yake kwa sababu ya amani na umoja uliopo kwani hata kifungu anachoshtakiwa nacho kwa kuzingatia kutunza amani na umoja kimeweka adhabu kubwa ambayo si chini ya miaka mitano.” – Wakili Tulimanywa Majigo.
Hata hivyo, Wakili wa utetezi Fatuma Karume alidai kuwa dhamana ni haki ya mshtakiwa na sio Serikali akiwakumbusha Mawakili wa Serikali na Serikali kwamba Lissu hajahukumiwa na upelelezi haujakamilika hivyo wanaitaka Mahakama itumie nguvu kumnyima dhamana mshtakiwa.
“Lissu ni mpinzani na tukumbuke Serikali ya CCM ndio ipo Mahakamani na wao ndio wanalazimisha umfunge mshtakiwa.” – Wakili Fatma Karume.
Tundu Lissu alifikishwa Mahakamani leo takribani ikiwa ni siku nne baada ya kushikiliwa na Polisi akiwa Airport Dar es Salaam akielekea Kigali Rwanda kwenye Mkutano wa Mawakili na kesi yake imeahirishwa hadi July 27, 2017.

No comments: