Wednesday, July 12, 2017

RAIS WA WANASHERIA TUNDU LISSU ATAKA WOTE WALIOPATA FEDHA ZA ESCROW WAKAMATWE

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika TLS, Tundu Lissu amesema kuwa watu wote waliopata mgao wa fedha hizo wakamatwe kwakuwa wameuthibitishia umma kuwa ni wala rushwa.

Lissu amesema kuwa kwa sasa hakuna ubishi kuwa watu hao ni wala rushwa na walitumia madaraka yao vibaya kujipatia fedha hizo na kuwa watu hao ni sehemu ya mafisadi ambao wamekuwa wakihujumu nchi.

Ameyasema hayo baada ya aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini wa Serikali ya awamu ya nne na mbunge wa Sengerema, William Ngeleja kurudisha Serikalini kiasi cha shilingi milioni 40.4 za mgawo wa Escrow hali ambayo imeibua mijadala mingi.

Ngeleja ambaye aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria, juzi alisema kuwa amefikia hatua hiyo ya kuzikabidhi fedha hizo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kujiweka kando na kashfa hiyo kwakuwa aliyempa ni mtuhumiwa.

“Sheria inasema kuwa ukikutwa umeiba unakamatwa unafikishwa kwenye vyombo vya dola ukikutwa na hatia unafungwa na fedha unarudisha, kwa hiyo hawa wote waliochukua mgawo huo wakamatwe wafikishwe katika vyombo vya dola na sio kurudisha tu hizo fedha hawa ni wezi,”amesema Lissu


Hata hivyo, ameongeza kuwa bila kujali nafasi ya watu hao katika jamii waliopata mgawo huo wanapaswa kwakuwa hata unapokuwa kiongozi wa dini hupaswi kula rushwa au kuchukua fedha za rushwa.

No comments: