Friday, July 28, 2017

UN YAJITOSA KUPINGA UKATILI UNAOFANYWA DHIDI ALBINO NCHINI TANZANIA


Watu wanaoishi na ualbino katika maeneo ya vijiji nchini Tanzania wanaendelea kuishi kwa hofu miongoni mwa mitazamo mingi hali inayosababisha ukatili dhidi yao, mtaalamu mmoja wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa alihitimisha baada ya ziara yake ya kwanza hapa nchini.
 
Mtaalamu wa kujitegemea kuhusu kunufaika na haki za binadamu kwa watu wenye ualbino, Ikponwosa Ero, alisema bado kunahitajika kazi zaidi ili kutatua tatizo la imani ya kiuchawi na kuelimisha umma.

“Watu wenye ualbino wanaendelea kuishi katika hali dhaifu, sanjari na sababu za msingi za mashambulizi dhidi yao zikiwa bado juu, na madhara ya zaidi ya muongo mmoja ya ukatili yalisababisha mlolongo wa athari mbaya,” alisema mwishoni mwa ziara yake ya siku 11 nchini Tanzania. “Watu wanaendelea kuishi katika hofu, hasa katika maeneo ya vijijini.”

Hata hivyo, Bi. Ero alifurahishwa na taarifa ya kupungua kwa idadi ya mashambulizi yaliyoripotiwa na aliipongeza serikali ya Tanzania kutokana na juhudi zake za kushughulikia tatizo hili – lilijojikita katika imani potofu ya kwamba viungo vya binadamu wenye ualbino vina thamanni katika vitendo vya kishirikina.

“Ninakaribisha hatua zilizochukuliwa na Serikali na Asasi za Kiraia, na hali ya kupungua kwa idadi ya mashambulizi yaliyoripotiwa,” alisema.  “Kumekuwepo na hatua chanya ili kushughulikia vitendo vya kichawi, pamoja na usajili wa waganga wa tiba ya jadi.”

 
“Hata hivyo, uangalizi kamili wa kazi yao haujafanikiwa, na bado kunaendelea kuwepo kwa hali ya mkanganyiko katika fikra za wananchi kwa ujumla baina ya vitendo vya kiuchawi na kazi ya waganga wa tiba ya jadi,” alisema Mtaalamu wa kujitegemea.

Bi. Ero aliweka mkazo juu ya saratani ya ngozi kuwa tishio kubwa linalohatarisha maisha ya watu wenye ualibino kuliko mashambulizi. , na alisema ni kipengele kingine kinachohitahitaji juhudi nyingi.

“Ni faraja kubwa kuona Serikali ikiwa inafanya kazi bega kwa bega na Asasi za Kiraia katika sekta ya elimu na ya afya, hasa kwa kutoa vifaa vya kuona na matumizi ya kliniki ya kuhama ili kuzuia kansa ya ngozi,” alisema.

“Ila programu hizi zinahitaji mno ushirikishwaji wa Serikali, ili kuwafikia watu wengi zaidi na kuhakikisha kwamba kazi hii inakuwa endelevu.”
 
Bi. Ero pia alisisitiza kuhusu wasiwasi kuhusu shule zinazotumika kama vituo vya ulinzi na usalama kwa ajili ya watoto wenye ualbino, ambako wakati mwingine vituo hivyo vilibadilika toka kuwa makazi ya muda na kugeuka kuwa makazi ya kudumu.

“Licha ya kuwa na dhamira nzuri ya ulinzi wa kuwahifadhi watoto wenye ualbino katika vituo vya shule kwa ajili ya malazi yenye ulinzi thabiti, inaonekana kwamba maeneo haya siyo tena ya muda,” alisema.

“Wanafunzi wanaosoma shule za sekondari au vyuo hawana chaguo lingine ila kurudi tena katika maeneo walimopata hifadhi baada ya kumaliza kipindi cha likizo kwa sababu wanahofu kurejea tena majumbani kwao,” alisema mtaalamu huyo. “Niliwahi kupokea ripoti kama hizi za watoto wanaosoma shule za msingi wanaohifadhiwa katika mabweni ya vituo hivi vinavyotoa malazi kwa watoto hawa.”

Bi. Ero alikaribisha upungufu mkubwa mno wa idadi ya jumla ya watoto katika vituo vya hifadhi, na aliwapongeza viongozi kutokana na bidii walioifanya kwa kuwaunganisha watoto hao na familia zao, ila aliongeza kusema kwamba bado kunahitajika kazi zaidi.

“Serikali inatakiwa kuendelea kuuelimisha umma na kuimarisha hatua za ulinzi, kwa sababu jamii kadha wa kadha hazikotayari kuwapokea watoto hawa,” alisema.
 
Katika ziara yake nchini Tanzania, Bi. Ero alikutana na viongozi mbalimbali wa ngazi ya juu na mashirika ya asasi za kiraia. Alitembelea mji mkuu wa Dodoma na jiji la Dar es Salaam, na pia alisafiri na kwenda maeneo ya kanda ya kaskazini ili kutembelea Mwanza, Shinyanga na Kigoma.. 

Alikutana na watu wenye ualbino, pamoja na wale waliosumbuliwa na vuguvugu la mashambulizi, na wanafamilia wao.

Mtaalamu wa kujitegemea, aliyeteuliwa na Baraza la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na Haki za Binadamu, anachunguza ukiukwaji wa haki zote dhidi ya watu wenye ualbino katika nchi mbalimbali, pamoja na mashambulizi, kuishi katika hofu ya kushambuliwa na watu wenye ualbino kuachwa kando katika malengo ya maendeleo. Aliwahi pia kubaini na kuhamasisha mifano bora, na kupambana dhidi ya kasumba, chuki na vitendo viovu vinavyosababisha ukiukwaji wa haki za binadamu.

No comments: