Thursday, July 27, 2017

UNAITUMIAJE MITANDAO YA KIJAMII KUTANGAZA BIASHARA YAKO ?


Na Jumia Travel Tanzania


Mitandao ya kijamii ni huduma zinazopatikana kwenye intaneti ambazo zinakuwezesha kuwasiliana, kutengeneza maudhui na kuwashirikisha watu wengine waliopo mitandaoni.



Tofauti na watu wanavyoitumia, Jumia Travel ingependa kukufunua macho kwamba mitandao ya kijamii imeleta fursa kubwa ya kutangaza biasahara za aina mbalimbali. Unaweza kuitumia mitandao hiyo kwa kufanikisha malengo kama vile; kukuza jina na biashara yako, kuwafahamisha wateja juu ya bidhaa na huduma zako, kujua wateja wanaichukuliaje biashara yako, kuwavutia wateja wapya pamoja na kujenga mahusiano thabiti na wateja ulionao.



Faida za kutumia mitandao ya kijamii



Kuwafikia watu wengi. Badala ya kutegemea wateja kuja moja kwa moja ofisini kwako mitandao ya kijamii huwafikia mamilioni ya watu sehemu mbalimbali ndani ya muda mfupi.



Kuwafikia wateja unaowakusudia. Uzuri wa mitandao ya kijamii ni kwamba hutofautiana kwa aina ya watumiaji wake kama vile vijana, watu wazima, wanasiasa, wanataaluma na matabaka mengine. Hivyo hii hutoa fursa kwa mfanyabiashara kulingana na huduma au bidhaa aliyonayo kujiwekea mkakati wa namna ya kuwafikia.



Unafuu. Haikuhitaji kuwa na fedha ndipo ufungue akaunti kwenye mtandao wa kijamii mara nyingi ni intaneti tu. Lakini kama unataka kuitumia kwa malengo ya kibiashara wamiliki wake hutoza kiasi kidogo cha fedha ambacho ni rahisi kukimudu.



Kumfikia mtu binafsi. Mitandao ya kijamii inakuruhusu kujenga ukaribu au kuwasiliana na wateja wako kwa ukaribu zaidi. Uwezo wa kuyapokea na kuyajibu maswali yao au kuyasikiliza na kuyafanyia kazi maoni yao vina ushawishi mkubwa katika kuwafanya wateja kutumia huduma na bidhaa zako.



Uharaka. Ndani ya muda mfupi unaweza kusambaza taarifa juu ya huduma na bidhaa zako kwa watu wengi kwenda sehemu mbalimbali.



Urahisi. Haikuhitaji kuwa na ‘madigrii’ ya vyuo vikuu ili kuweza kutumia mitandao ya kijamii. Ni rahisi kuitumia kwa njia mbalimbali kama vile kompyuta, tabiti au simu za mikononi ambazo watu wengi wanamiliki.   

Mitandao mikuu ya kijamii unayoweza kuitumia


Facebook. Mtandao huu hutoa fursa nzuri kwa wafanyabiashara kuwasiliana na wateja wao moja kwa moja, kuweka picha na video, kutangaza ofa walizonazo, bidhaa na huduma mpya na mambo mengine.



Twitter. Mara nyingi huduma hii hutumika kutuma na kupokea jumbe fupi kutoka kwa wateja wapya na waliopo. Siku hizi pia hutumika kama nyenzo muhimu kwa kuweka viungo ambavyo vitawapeleka wasomaji kwenye tovuti.



Youtube. Mtandao huu hutumika kwa kuweka video tofauti, zinaweza kuwa juu ya huduma na bidhaa ulizonazo, namna ya kuzitumia pamoja na taarifa mbalimbali ili wateja wako wazitazame.



Blogu. Kama mfanyabishara pia unaweza kufungua mtandao huu utakaokupatia fursa kubwa ya kuwashirikisha wasomaji wako juu ya huduma na bidha zako pamoja taarifa mbalimbali.



Instagram. Mbali na mtandao huu ipo mingine pia inayowawezesha watumiaji kuweka na kuwashirikisha watu wengine picha mbalimbali. Kwa mfano hivi karibuni Instagram wameuboresha mtandao wao kwa kuwawezesha watumiaji wake kuweka picha zaidi ya moja. Hivyo kutoa fursa nzuri kwa wafanyabishara kuweka picha mbalimbali za bidhaa na huduma zao.

Mbali na kuwepo kwa faida lukuki za mitandao ya kijamii, Jumia Travel ingependa kukuasa kwamba bado unahitajika umakini mkubwa katika nanma ya kuitumia. Miongoni mwa changamoto unazoweza kukumbana nazo ni pamoja na kupoteza muda na fedha zako kwa kuwekeza kwenye  kitu ambacho hakitoleta faida, kusambaa kwa habari zisizo sahihi kuhusu biashara yako kwa wateja na kukumbana na matatizo ya kisheria endapo usipofuata au kuvunja taratibu zilizowekwa na mamlaka husika.

No comments: