Monday, October 29, 2012

Utajiri wa Kamanda Barlow waanikwa

 

 

         SIKU chache baada ya Jeshi la Polisi kutoa taarifa yake ya uchunguzi kuhusu kifo cha aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, umeibuka utata wa mali alizokuwa akimiliki, huku akidaiwa kumiliki utajiri wa kutisha likiwamo jengo la ghorofa.

Habari za kiuchunguzi zilizopatikana zinaeleza kuwa mbali ya jengo hilo, Kamanda Barlow anadaiwa pia kumiliki magari zaidi ya saba yakiwamo malori mawili aina ya Fuso, malori mawili ya mchanga, gari dogo aina ya Toyota Cresta pamoja na Toyota Hilux Double Cabin.

Magari hayo yanadaiwa kuhifadhiwa eneo la Nyakato mjini Mwanza, yakisimamiwa na mfanyabiashara mmoja kwa niaba yake.

Mbali na magari hayo kamanda hyo anatajwa kumiliki nyumba ya kifahari mkoani Mara, ambayo aliijenga alipokuwa RPC mkoani humo, huku nyumba nyingine ikiwa maeneo ya Capri-Point jirani na Ikulu ndogo mkoani Mwanza, inayoelezwa kuwa aliinunua baada ya Serikali kutangaza uuzaji wa nyumba zake kwa watumishi wake.

Umiliki wa mali hizo umeibua maswali mengi, wengi wakitaka kujua iwapo zinalingana na kipato cha Kamanda Barlow, licha ya kuwa na cheo cha Kamanda wa Polisi wa mkoa.

No comments: