Tuesday, November 12, 2013

SOMA HABARI AMBAYO IMEANDIKWA NA GAZETI MOJA LEO TANZANIA LIKIMPONDA KAMISHNA KOVA WAZI WAZI

 
                                Na Karoli Vinsent
GAZETI LA TANZANIA DAIMA LEO LIMEAMUA KUANDIKA HABARI AMBAYO IMEKUWA GUMZO SANA KATIKA VICHWA VYA HABARI JIJI DAR ES SALAAM NA TANZANIA KWA UJUMLA HABARI AMBAYO ILIKUWA NA KICHWA CHA HABARI KINACHOSEMA --BAADA YA ULIMBOKA NA KIBANDA KOVA AIBUKIA KWA DK MVUNGI.

PATA NAFASI YA KISOMA KWA MAKINI YOTE HAPA--
inaendelea hapa

         JESHI la Polisi limeonyesha wazi kuwa halina dhamira ya dhati ya kuwasaka na kuwatia nguvuni wahalifu waliowateka, kuwatesa na kuwaumiza vibaya Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri nchini (TEF), Absalom Kibanda, na Mwenyekiti wa Jumuia ya Madaktari, Dk. Steven Ulimboka.
             Ni zaidi ya mwaka mmoja na miezi minne tangu Dk. Ulimboka atendewe unyama huo lakini hadi leo suala hilo limegeuzwa sinema na jeshi hilo kwa kumkamata mtu asiyehusika ambaye baadaye walilazimika kumwachia huru.
        Hivi ndivyo imetokea pia kwa Kibanda ambaye ni Mahriri Mtendaji wa Kampuni ya New Habari (2006), kwani tangu ateswe na kung’olewa jicho, kucha, meno na kukatwa kidole, hakuna mtuhumiwa hata mmoja aliyekamatwa ikiwa ni zaidi ya miezi saba sasa.
        Lakini jana Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, akiongozana na maofisa wengine wa jeshi hilo akiwemo Kamishna wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, waliitisha mkutano na waandishi kuwataja ‘vibaka’ waliokamatwa wakihusishwa kumshambulia na kumwibia Dk. Sengondo Mvungi.
       Dk. Mvungi ni mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ambaye alivamiwa na majambazi hao takriban wiki mbili zilizopita na kukatwa mapanga na kuporwa kompyuta mpakato (laptop) na fedha.
    Kwa sasa hali yake ni mbaya akiwa bado hajitambui na hivyo kulazimika kupelekwa nchini Afrika Kusini kujaribu kuokoa maisha yake.
Hatua ya Waziri Nchimbi kujitokeza jana kuzungumzia tukio hilo na kuonyesha juhudi za haraka za kuwanasa watuhumiwa, iliwasukuma waandishi wa habari kuhoji kulikoni matukio ya Ulimboka na Kibanda yamewekwa kiporo.
Kama kawaida yake, Kamishna Suleiman Kova alijibu kuwa kila tukio lina mazingira yake, hivyo tukio la Mvungi halifanani la Kibanda wala Dk. Ulimboka na kueleza kuwa mfumo wa suala hilo kiupelelezi unakwenda vizuri.
“Tukio la Mvungi na la kina Kibanda na Ulimboka mazingira yake ni tofauti; unapeleleza halafu unatuhumiwa wewe mwenyewe, ila watapatikana,” alisema Kova.
Katika taarifa yao hiyo, Dk. Nchimbi na Kova walisema kuwa wamekamatwa watuhumiwa wengine watatu zaidi wanaodaiwa kumvamia, kumjeruhi kwa mapanga na kumpora mali Dk. Mvungi.
Kova alisema kuwa operesheni ya kuwasaka waliomshambulia Dk.Mvungi imefanikiwa kwa asilimia zaidi ya 80 ambapo mpaka sasa wamekamatwa watu tisa wakiwa na vifaa walivyotendea uhalifu huo ambavyo ni mapanga matano, simu ya mkononi na kigoda.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Msigwa Kopelo, Chibango Magozi, Ahmed Ally, Zakaria Rafael (23) dereva wa boda boda, Manda Salowaa ( 40), Paulo Jailos (29), Juma Hamisi (29), Longishu Semaliki(29) muuza ugoro Vingunguti na Masunga Makenza (40).
Dk. Mvungi ambaye pia ni mshauri wa masuala ya kisheria wa Chama cha NCCR-Mageuzi alipatwa na mkasa huo usiku wa kuamkia Novemba 3, mwaka huu, akiwa nyumbani kwake Kibamba Msakuzi, Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Baada ya kumjeruhi waliiba sh milioni moja, bastola, simu mbili za mkononi na kompyuta mpakato (laptop).
Utendaji huu wa jeshi la polisi unaacha mashaka makubwa hasa kwa matukio makubwa ya utekaji na utesaji ambayo ni mageni nchini, kwani uchunguzi wake wa kuwasaka watuhumiwa unalegalega.
Itakumbukwa kuwa mara tu baada ya tukio la Dk. Ulimboka Julai 26 mwaka jana, jeshi hilo liliunda kikosi kazi kilichowashirikisha wataalamu mbalimbali wa kanda maalumu na makao makuu.
Hadi sasa ripoti yake haikuwahi kutolewa hadharani kama Kova alivyojigamba wakati akiitangaza, badala yake hivi karibuni amekuwa akitupiana mpira na wakuu wake kuhusu ripoti hiyo.
Dk. Ulimboka kwa kiapo aliwataja watu aliowatuhumu kuhusika na tukio hilo, mmoja wao akiwa ni ofisa usalama wa taifa-Ikulu lakini hakuwahi kufanyiwa gwaride la utambuzi wala kuhojiwa na kamati hiyo ya uchunguzi.
Siku chache kabla ya Dk. Ulimboka kumtaja ofisa huyo, gazeti la MwanaHalisi lilichapisha habari iliyoeleza tukio zima lakini serikali ikalifungia kwa muda usiojulikana kwa kile kinachoitwa kosa la uchochezi.

        Tukio hilo la Dk. Ulimboka limekuwa kama sinema kwani hata mtuhumiwa pekee raia wa Kenya, Joshua Mulundi, aliyekuwa amekamatwa na kuwekwa ndani kwa muda kadhaa na kufunguliwa kesi, ukamatwaji wake ulikuwa wa kutia mashaka.
Wakati vinywa vya wananchi vikiwa bado vinatafakari unyama huo, tasnia ya habari nayo iliingiliwa kwa kushambuliwa kiongozi wa wahariri katika tukio kama lilelile la Dk. Ulimboka.
             Matukio haya ni kama ya kupangwa kutokana na kufanyika kwa ustadi wa hali ya juu na kwa muda mfupi tena bila wahusika kuchukua chochote kwa mteswaji.
Kama ilivyokuwa kwa Dk. Ulimboka, pia kwa Kibanda, iliundwa kamati ya uchunguzi iliyoongozwa na wataalam wakiwemo walewale walioshindwa kuwakamata watesaji wa Dk. Ulimboka.
        Hadi leo hakuna mtuhumiwa hata mmoja ametiwa nguvumi na jeshi la polisi ambalo kila siku viongozi wake wamekuwa wakijinasibu kuwa na intelijensia ya hali ya juu inayobaini matukio ya kihalifu kabla ya kutokea, mathalani kuzuia maandamano na mikutano ya vyama kwa madai ya kuepusha vurugu.
        Wadadisi wa maswala ya mambo wanashangaa jinsi maswala haya yakiwa yanaregarega katika kufanyiwa uchunguzi huku waandishi wa habari wakifanya uchunguzi na kufanikiwa kubaini watu wanaofanya unyama huo mfano Gazeti lilofungiwa la mwanaharisi lilifanya uchunguzi na kufainikiwa kumbaini mtuhumiwa aliyefanya unyama na pia kuthibitishwa na ulimboka mwenyewe,lakini katika hali yakushangaza serikali ikalifungia gazeti la mwanaharisi kwa madai kuwa lilifanya uchochezi huko likishindwa kumchukulia hatua mtu aliyejulikana kwa jina la Ramadhani Ighondu ambaye inasemekana ni mfanyakazi wa idara ya usalama wa taifa
Huku serikali hii sikivu ya CCm ikishindwa kusema bayana wahusika maswala haya ya kinyama.


No comments: