Saturday, February 28, 2015

UNDANI NA UKWELI WA KIFO CHA CAPTAIN KOMBA HUU HAPA

...Komba enzi za uhai wake.
MBUNGE wa Mbinga Magharibi, Kapten John Komba amefariki dunia jioni hii jijini Dar es Salaam.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye amethibitisha kutokea kwa kifo hicho, hata hivyo hakuwa tayari kuelezea kwa undani kwa madai kuwa taarifa hizo zimemfikia sasa hivi.
Mmoja wa watoto wa Komba ambaye aliyejitambulisha kwa jina la Herman amethibitisha kutokea kwa msiba huo na akasema, huku akilia, msiba wa baba yake upo nyumbani kwake Mbezi Tangi Bovu, Dar.
Habari zinasema asubuhi ya leo Komba alikwenda kwenye shughuli zake za kikazi kama kawaida lakini baadaye akajisikia vibaya, hivyo akaamua kurudi nyumbani ambako alizidiwa ndipo familia yake ilipoamua kumkimbiza Hospitali ya TMJ lakini alipopimwa na madaktari ikathibitika kuwa alikuwa tayari ameaga dunia. habari zaidi zinasema kuwa hivi sasa mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya Jeshi ya Lugalo.
Kapteni Komba ambaye pia ni Mkurugugenzi wa Kikundi cha Maigizo cha Tanzania One Theatre (TOT),  ambacho kina kikundi cha taarabu na bendi  inayokwenda na mtindo wa Achimenengule, amekuwa akikisaidia sana chama chake, Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika kampeni zake wakati wa uchaguzi kwa kutunga nyimbo za kuhamasisha wapiga kura na kushiriki kupiga live kwenye majukwaa ya kisiasa.
 .
..alipokuwa bungeni
Enzi za uhai wake alitamani  sana na kufanya juhudi kubwa ili mtindo wa Achimenengule uwe wa kitaifa lakini ikashindikana,  na badala yake Watanzania sasa tuna muziki wa Mduara ambao umekuwa kama mtindo wa muziki wetu kwa sababu zifuatazo.
Kwanza, ni mtindo halisi wa Kitanzania uliochipuka kutoka mahadhi ya kimwambao ya Tanzania. Pili, ndiyo mtindo pekee uliowahi kutumiwa na bendi nyingi baada ya kuasisiwa na ‘mabingwa’ wa muziki wetu, wana Njenje, The Kilimanjaro Band.
Baada ya bendi hiyo kuuasisi, mtindo huo, tayari umepigwa na bendi kama TOT Plus, Chuchu Sound, Pamo Sound, Inafrika Band, wana mipasho kadhaa na mwanamuziki mahiri lakini asiyethamini kiwango chake kikubwa cha muziki, Bob Haisa.
Sababu ya tatu ni kwamba mtindo huo umekuwa wa kupigwa na bendi nyingi, vikundi vingi na wanamuziki wengi si kwa kulazimisha bali kwa mapenzi tu ya mashabiki wa muziki wa Tanzania.
Kapteni Komba awali alikuwa mwalimu wa shule ya msingi kabla ya kuingia jeshini na kuwa kiongozi wa kikundi cha maonesho cha jeshi na baadaye Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi akamshawishi aachane na jeshi na kujiunga na CCM wakati wa mfumo wa vyama mingi ulipoingizwa mwaka 1992.
“Mzee Mwinyi ndiye aliyenifanya niache jeshi wakati huo nikiwa na cheo cha ukapteni. Aliniomba nikisaidie chama kwa kuanzisha kikundi ambacho lengo lake lilikuwa kukipigia debe CCM,” aliwahi kusema hivyo Kapteni Komba.
Ameshiriki kampenzi za marais Ally Hassan Mwinyi, Benjamin William Mkapa na aliye madarakani hivi sasa, Jakaya Mrisho Kikwete. Alikuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa na Mbunge wa Jimbo la Mbinga Magharibi hadi kifo kinamchukua.
Licha ya siasa Kapteni Komba alikuwa anamiliki shule na pia alikuwa na biashara kadhaa.

Mwaka 2012 Komba aliwahi kupelekwa India kwa matibabu ambapo alifanyiwa upasuaji wa nyonga baada ya kupata ugonjwa uliosababisha mifupa kusagana sehemu hiyo ya nyonga.
Baada ya kurejea nchini alisema upasuaji huo ulichukua saa tano na ulifanyika katika Hospitali ya Apollo, India na alikanusha kuwa alikuwa na ugonjwa wa figo.Ugonjwa uliomuua ni shinikizo la damu ambalo lilikuwa likimsumbua kwa muda mrefu.
..marehemu Komba akiongea na wanahabari nyumbani kwake Mbezi tangi Bovu akielezea kuimarika kwa afya yake aliporejea kutoka India kwenye matibabu, Julai 27, 2012.
MALI ZAKE ZATISHIWA KUUZWA
Mapema mwezi uliyopita mwaka huu, mali za Kapteni John Komba zilitangazwa kupigwa mnada kutokana na kushindwa kulipa deni analodaiwa na Benki ya CRDB.
Mali hizo zilihusisha eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 2,214 lililopo Mbezi Tangi Bovu, Dar es Salaam, kiwanja namba 1030 kilichosajiliwa kwa jina la John Damiano Komba na Salome Komba.

Kwa mujibu wa tangazo lililotolewa kwenye vyombo vya habari, Kampuni ya Uwakili ya Mpoki & Associates Advocates inayoiwakilisha CRDB ilitangaza kuuza eneo hilo la kibiashara lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya mafuta, maduka makubwa, benki, sehemu ya kufanyia mazoezi, hospitali na huduma nyingine za kijamii.

Marehemu Komba ameacha mjane, Bi Salome, ambaye ni mwalimu kitaalumu na watoto kadhaa. Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi- ameen!

No comments: