Thursday, April 9, 2015

ZITTO ALIWAHI KUANDIKA MAKALA GAZETINI AKISIFIA KATIBA NA MISINGI YA CHADEMA,SIO MBAYA UKISOMA ITAKUSAIDIA

LEO NIMEKUWEKEA  MAKALA HII ALIYOIANDIKA ZZK KATIKA GAZETI TANZANIA DAIMA DESEMBA 30, 2012 MAKALA AMBAYO ALIIPA JINA LA FUATA MISINGI USIFWATE WATU



'Fuata Misingi sio watu'
MEI mwaka 2003 tukiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam tulitembelewa na mgeni kutoka Chama cha SWAPO cha Namibia. Wakati huo nchini Namibia (na Afrika kwa ujumla) kulikuwa kuna mjadala kuhusu kubadili katiba ya nchi hiyo ili kumruhusu Rais Sam Nujoma kugombea kipindi cha tatu.

Mgeni huyu alikuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa SWAPO na alialikwa na vijana wa CCM pale Mlimani, kina Wilman Kapenjama na Martin Shigella. Walimleta kwenye moja ya kumbi za semina ili kufanya mjadala kuhusu Afrika. Nilimuuliza swali kwamba msimamo wake nini kuhusu mabadiliko ya Katiba ya Namibia ili kumwezesha Nujoma kugombea kipindi cha tatu cha urais.


Akanijibu kwamba wao vijana wa SWAPO wanaunga mkono lolote ambalo Sam Nujoma atataka! Mmoja wa washirika wa mkutano ule Kitila Mkumbo, alisimama na kumwambia kijana yule ‘hupaswi kufuata mtu, fuata misingi’. Alitoa kauli hii kwa ukali kidogo. Nadhani ndiyo maana bado ni kauli ambayo imenikaa mpaka hivi sasa.

Hivi sasa hapa nchini kumezuka wimbi la wanasiasa kuwa na makambi ambayo yanatokana na ufuasi kwa mtu au kiongozi wa kambi husika badala ya ufuasi kwa misingi ya chama cha siasa au basi angalau misingi ya kambi husika ya chama hicho. Makambi ni utamaduni ambao umeshamiri zaidi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ingawa hata vyama vya upinzani sasa vimeingia kwenye mtego huo hatari sana kwa demokrasia.

Huu ni mfululizo wa makala sita, zitakazokuwa zinaelezea misingi mbalimbali ya chama ambacho mimi ni mwanachama, CHADEMA, na namna ambavyo viongozi mbalimbali wa chama hicho wamekuwa wakisimamia kwa vitendo misingi hiyo. Makala hizi zitakuwa zinatoka kila wiki ya mwisho ya mwezi katika kipindi cha nusu ya kwanza cha mwaka 2013. Chama cha siasa ni jumuiko la watu wenye nia moja na lengo moja la kisiasa.

Ni mchanganyiko wa watu wenye kuunganishwa na misingi fulani. Misingi hii inapokosekana au kupondwapondwa basi uwepo wa jumuiko hilo linaloitwachama cha siasa unakuwa shakani. Kwa kutolea mfano wa chama changu, CHADEMA, ni chama cha siasa ambacho tangu kuanzishwa kwake kimekuwa wazi kabisa kuhusu misingi yake inayosimamia. Iwapo wana CHADEMA watashindwa kuheshimu misingi ya chama basi uhai wa chama hicho utakuwa shakani na hatimaye hata uhai wa mfumo imara wa vyama vingi nchini Tanzania.

CHADEMA sasa imejijenga kama chama cha siasa kinachopinga ufisadi, kinachosimamia uwajibikaji na uwazi katika uendeshaji wa serikali, kinachopigania siasa za ukweli, kinachotetea haki za raia – haki za kuishi na kushiriki siasa, kinachotetea rasilimali za nchi.
Katika katiba ya chama hicho kuna misingi 12 ambayo chama kimejengwa juu yake. Iwapo wanachama wake watasimamia kwa dhati misingi hii badala ya kusimamia watu, kamwe hapawezi kutokea malumbano yasiyo na msingi yanayopoteza malengo ya ukombozi mpya kwa Mtanzania. Inasikitisha sana hivi sasa kwenye siasa za Tanzania, kwa vyama vyote vya siasa, kumekuwa na ufuasi wa watu badala ya ufuasi wa misingi.

Watu si mawe, hugeuka. Misingi inabaki misingi. Ama unafuata misingi hiyo au unajiunga na chama kinachofuata misingi unayoitaka, au unaanzisha misingi mingine katika chama kipya. Ufuasi wa mtu kwenye chama cha siasa unapaswa kuangaliwa kwa ufuasi kwa misingi inayojenga chama hicho. Ufuasi wa kiongozi wa CHADEMA unapaswa kupimwa kwa kuangalia ni namna gani kiongozi huyo anatekeleza kwa vitendo misingi ya chama iliyotajwa hapo juu (kupinga ufisadi, kusimamia uwajibikaji).
Uadilifu wa mwanachama wa chama hicho utapimwa si kwa uaminifu kwa kiongozi au mwanachama mwingine wa chama au kikundi cha wanachama, bali kwa uaminifu na utekelezaji wake wa misingi ya chama. Kiongozi au mwanachama atakuwa ni msaliti iwapo anakwenda kinyume cha misingi ya chama.
CHADEMA imejipambanua wazi wazi katika ‘utetezi wa rasilimali za taifa’, kwamba utajiri wa nchi uwe ni ardhi, madini, misitu, maji, gesi asilia vinatumika kwa maendeleo ya Watanzania na si kwa kikundi cha watu wachache. Hata masuala ya rasilimali fedha pia imekuwa mstari wa mbele kama chama kisichotaka mchezo kabisa na kutapanywa kwa mali za taifa.
Katika miaka ya hivi karibuni kumekuwa kuna malalamiko makubwa ya wananchi kuhusu uporaji wa ardhi, migogoro ya ardhi kati ya wafugaji na wakulima na kati ya wanavijiji na wawekezaji. Malalamiko haya yalikuwa yanaandikwa na vyombo mbalimbali vya habari vya hapa nchini na hata nje ya nchi. Katika Bonde la Mto Rufiji maelfu ya ekari za ardhi yamegawiwa kwa wanaoitwa wawekezaji wakubwa kwa ajili ya kulima miti ya mibono kaburi.

Kule Mkoa wa Katavi katika Wilaya ya Mulele kumekuwa na sintofahamu kuhusiana na ardhi ambayo ilikuwa inakaliwa na wakimbizi kutoka nchini Burundi na sasa kugawiwa kwa wawekezaji. Kilosa mkoani Morogoro kumekuwa na vurugu za mara kwa mara zikihusisha wakulima na wafugaji.

Mkoani Manyara na mkoani Mbeya kumekuwa na malalamiko ya wananchi kuhusu mashamba yaliyokuwa ya NAFCO na sasa yamebinafsishwa kwa wawekezaji ambao wamehodhi ardhi bila kuifanyia uzalishaji wowote ilhali wananchi hawana ardhi. Msingi mkubwa hapa ni kulinda maliasili ya nchi kwa ajili ya matumizi ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo. Kuzuia uharibifu wa rasilimali za nchi unaofanywa na kikundi cha watu wachache dhidi ya wengi ama unaofanywa na kizazi cha sasa dhidi ya vizazi vijavyo ni kazi ambayo chama hicho kimeifanya kupitia wabunge wake.

Mwanachama au kiongozi yeyote wa CHADEMA ambaye hasimamii msingi huu anakwenda kinyume cha chama na anapaswa kutafuta chama kingine ambacho kitampa uhuru wa kuruhusu rasilimali za nchi kutumika vibaya. Viongozi wa chama hicho na hasa wabunge wanapaswa kuwa mstari wa mbele kusimamia msingi huu. Malalamiko ya wananchi yalikuwa ni malalamiko tu yanayoibuka na kuzama mpaka pale mbunge kijana alipoamua kushughulikia suala hilo, si kwa kupiga kelele au kuendeleza kulalamika, bali kwa kutumia njia za kidemokrasia kupitia Bunge.

Katika Mkutano wa Tisa wa Bunge la 10, Mbunge wa Kawe alifanikiwa kupitisha hoja bungeni kuhusu usimamizi bora wa ardhi ya Tanzania. Kiongozi huyu aliona kuwa kuna changamoto zilizoanishwa hapo juu lazima zifanyiwe kazi kwa faida ya wananchi wa kizazi cha sasa na kizazi kijacho.

Bunge bila kujali itikadi za kisiasa lilipitisha azimio la kutaka kufanyika kwa tathmini ya ardhi nchi nzima ili kuweza kufahamu ni ardhi kiasi gani imegawanywa mpaka hivi sasa na kwa nani. Lengo ni kuweka maamuzi ya kisera kuhusiana na ugawaji wa ardhi ili kulinda wananchi maskini ambao kila kukicha wamekuwa wakinyang’anywa ardhi kwa kisingizio cha uwekezaji.

Haya ni mafanikio ya kazi za waabunge wa CHADEMA wanaosimamia misingi ya chama kwa kutekeleza kwa vitendo misingi hiyo. Kutokana na hoja yenyewe ya ardhi inavyo nufaisha watu binafsi au vikundi vya watu ambao Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, anawafahamu au asiowafahamu, mbunge huyu angeendekeza ufuasi wa watu badala ya misingi ya chama asingefanikiwa kufanya masuala haya mazito kwa nchi, yenye mafanikio kwa wananchi wote bila kujali vyama vyao.

Faida kubwa ya ufuasi wa misingi ni kwamba mafanikio yoyote yanayopatikana katika utekelezaji wa misingi ya chama,kila mwanachama anajivunia nayo. Hata hivyo, pale ambapo chama kimegawanyika kwa misingi ya ufuasi wa watu au vikundi vya watu ni nadra mafanikio ya misingi ya chama inayotekelezwa na mwanachama ambaye wewe si mfuasi wake kuyaona kama ni mafanikio ya chama.

Mafanikio yote yatakayopatikana kutokana na hoja yenye kuhusiana na ardhi yanapaswa kuwa mafanikio ya kujivunia kwa wana CHADEMA wote. Chama hicho kisione aibu kujivunia mafanikio ya viongozi wake wanaotekeleza misingi kwa vitendo. Mwelekeo wa siasa za zama hizi ni ya ufuasi wa misingi na si ufuasi wa watu. Mfuasi wa misingi hawezi kuyumbishwa kwani misingi haiyumbi.


Mwezi ujao nitatolea mfano msingi wa kupinga ufisadi ambapo tutaona kuhusu usimamizi kwa vitendo wa vita dhidi ya rushwa na ufisadi kupitia kwa viongozi wa chama hicho.

No comments: