Friday, June 26, 2015

CHADEMA NA ACT WAMLILIA MWANDISHI NGULI EDSON KAMUKARA


CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
SALAAM ZA RAMBIRAMBI MSIBA WA EDSON KAMUKARA
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimepokea kwa mshtuko na majonzi makubwa kifo cha aliyekuwa mmoja wa waandishi wa habari mahiri na mhariri wa gazeti la mtandaoni, Mwanahalisi Online, Edson Kamukara, kilichotokea ghafla jana jioni katika mazingira yanayodaiwa kuwa ni ajali ya moto.

Kumwelezea Edson Kamukara ambaye kabla ya kuhamia Mwanahalisi Online linalomilikiwa na Hali Halisi Publishers, alikuwa Mhariri wa Gazeti la Tanzania Daima, akiwa ametokea Gazeti la Jambo Leo ambalo alijiunga nalo akitokea Gazeti la Majira, katika nafasi hii ya salaam za pole yenye ukurasa mmoja, linaweza kuwa jambo gumu sana.


Marehemu Kamukara alikuwa mmoja wa waandishi makini na mahiri ambao tasnia ya habari ingeweza kujivunia kuwa nao (wakiwa hai) kwa muda mrefu, hususan katika changamoto kadhaa ambayo taaluma hiyo adhimu inapitia kwa sasa nchini Tanzania.
Katika salaam hizi, CHADEMA kupitia Idara ya Habari na Mawasiliano ambayo kutokana na majukumu yake ya kila siku ilifanya kazi kwa ukaribu wa kitaaluma na kikazi na Kamukara, inaweza kutaja sifa nne kati ya nyingi alizokuwa nazo Kamukara;

1.     Uthubutu wa kukataa rushwa na kusimamia maadili ya taaluma.
2.     Kupenda kazi yake.
3.     Nidhamu ya kazi.
4.     Uwezo wa kutimiza majukumu yake kazini.

Mbali ya kumsaidia kupata zawadi katika mashindano ya tuzo za umahiri wa uandishi wa habari, chini ya Baraza la Habari Tanzania (MCT), tunaamini sifa hizo pia zilimfanya Kamukara awe miongoni mwa waandishi vijana walioweza kuaminiwa na kukabidhiwa majukumu ya uhariri katika vyombo vya habari vikubwa akiwa na umri mdogo, baada ya kuwa ameandaliwa na kuiva kuchukua nafasi muhimu katika kutimiza uandishi wa habari unaowajibika kwa umma.

Zinahitajika kurasa kadhaa kuweza kumwelezea Edson. Kwa masikitiko makubwa CHADEMA kupitia Idara ya Habari na Mawasiliano, kinatoa salaam za pole na rambirambi kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki na wote walioguswa kwa namna moja au nyingine na msiba huu wa Kamukara.

Salaam hizi za pole pia ziwafikie wafanyakazi wenzake katika Kampuni ya Hali Halisi Publishers wamiliki wa Gazeti la Mwanahalisi Online kwa kuondokewa na mtumishi mwenzao ambaye tunaamini hadi mauti yanamkuta si tu walifanya naye kazi lakini waliishi naye vizuri.

Aidha chama kinatoa salaam za pole kwa tasnia nzima ya habari nchini hususan kwa waandishi wa habari kwa kuondokewa na mwandishi mwenzao katika wakati ambao mchango wake ulikuwa bado ukihitajika katika mapambano ya kitaaluma na kikazi.
Tunaungana pia katika maombolezo ya msiba huu na wapenzi wote wa kazi za Kamukara ambao wengi wao hususan baada ya kuwa wamesoma makala yake kwenye Gazeti la Mawio toleo la Alhamis wiki hii (jana) ambako alikuwa akiandika mara kwa mara, watakuwa bado hatawaki kuamini kuwa Edson Kamukara katutoka na hatuko naye tena katika ulimwengu huu wa kimwili.

Wakati tukimwombea mapumziko ya amani huko aliko Edson Kamukara, tunamwomba Mwenyezi Mungu awatie nguvu wafiwa wote na kuwajaalia ujasiri wa kuukubali ukweli huu mchungu na moyo wa subira katika wakazi huu wa majozni mazito.
Bwana alitoa, Bwana ametwaa. Jina lake lihimidiwe.
Imetolewa leo Ijumaa, Juni 26, 2015 na;
Idara ya Habari na Mawasiliano
CHADEMA



      TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUTOKA ACT WAZALENDO
CHAMA cha Alliance ForChange and Transparance( ACT- Wazalendo.)kinachozingatia msingi wa utu, undugu  na uzalendo kwa Taifa,kimepokea kwa masikitiko makubwa kifo cha Mwandishi wa Habari Edson Kamukara.

Kutokana na msiba huo Chama kinatoa salamu za pole kwa  familia ya Marehemu, ndugu jamaa na marafiki,waaandishi wa Habari na wafanyakazi wote wa Halisi Publishers kwa kuondokewa na mtu ambaye mchango wake kwa Taifa ulikuwa unahitajika kwa kiasi kikubwa hasa wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu katika nchi

Tunawaombea kwa mungu  wawe na uvumilivu na kuzidi kumuombea marehemu apate pumziko la amani.

Kichama tumempoteza mtu aliyekuwa akituelekeza upungufu wetu kupitia kalamu yake hali iliyotufanya tujirekebishe kila tunapobaini ukweli wa ukosoaji wake.

Tunazidi kumuombea kwa Mungu ampe faraja katika utangulizi wake huu, huku tukiwa na mengi mema ya kujifunza kutoka kwake.


Imetolewa na

Samson Mwigamba
Katibu Mkuu Taifa ACT-Wazalendo

26/06/2015

No comments: