Wednesday, June 24, 2015

MAYANJA ATUA COASTAL UNION, ASAINI MIAKA MIWILI KUIFUNDISHA COASTAL UNION

Kulia ni Katibu Mkuu wa Coastal Union,Kassim El Siagi akipokea mkataba wa Kocha Mkuu mpya wa timu hiyo,Jackson Mayanja mara baada ya kuusaini leo ambapo amesaini mkataba wa miaka miwili kuifundisha  timu hiyo,katika Halfa iliyofanyika mjini hapa,Picha kwa Hisani ya Coastal Union.
 NA MWANDISHI WETU,TANGA.
MABINGWA wa Ligi kuu soka Tanzania bara mwaka 1988,Coastal Union,Wagosi wa Kaya imeingia mkataba wa miaka miwili na aliyekuwa Kocha Mkuu wa Kagera SugarJackson Mayanja ambaye ni raia wa Uganda kuifundisha timu ya Coastal Union katika msimu ujao wa Ligi kuu soka Tanzania Bara itakayoanza Mwezi Agosti mwaka huu .
Utiliaji wa saini wa Kocha huyo ulifanyika (leo)jana mjini hapa na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa timu ya Coastal Union akiwemo Mjumbe wa Kamati ya Utendaji Albert Peter na Katibu Mkuu wa timu hiyo,Kassim El Siagi.
Kocha Mkuu mpya wa timu ya Coastal Union,Jackson Mayanja kushoto akisaini mkataba wa miaka miwili kuifundisha timu hiyo kulia ni Katibu Mkuu wa Coastal Union,Kassim El Siagi,Picha kwa Hisani ya Coastal Union.
Akizungumza baada ya kumalizika zoezi hilo,Ofisa Habari wa Coastal Union,Oscar Assenga amesema kuwa kutokana na umahiri aliokuwa nao kocha huyo wanaimani kubwa ataipa mafanikio timu hiyo hasa katika harakati za kuhakikisha inafanya vizuri ligi kuu msimu ujao.

Amesema kuwa uwezo wa Kocha huyo utaleta matumaini makubwa ya mafanikio hasa ukizingatia ni kocha mwenye uwezo mzuri wa kufundisha na kuzipa mafanikio timu hivyo tunaamini kuja wake kwetu itakuwa chachu katika maendeleo.
Mayanja ambaye aliwahi kuzifundisha timu za soka Kiyuvu FC ya Rwanda,Timu ya Mamlaka ya Mapato nchini Uganda (URA),Vipers  FC ya Bunamwaya  na KCC ya Uganda amesema kutua kwenye timu hiyo kumpa faraja kubwa hivyo atahakikisha anatoa mchango wake kwenye kuipa mafanikio.
Amesema kuwa mipango yake mikubwa ni kuhakikisha timu hiyo inang’ara katika michuano ya Ligi kuu msimu ujao ikiwemo kubadili aina ya mchezo wa timu hiyo ili iweze kupata mafanikio kwa kuweka umoja baina ya wachezaji mashabiki, wanachama na wapenzi.

Amesistiza pia umuhimu wa mshikamano baina ya wapenzi,wanachama na viongozi ili kuiwezesha timu hiyo kuchukua Ubingwa wa Ligi kuu msimu ujao kwani dhamira yake ni kutaka kuona timu hiyo inang’ara kwenye medani za kitaifa na kimataifa.
Mwisho.


Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano cha Coastal Union.

No comments: