Sunday, June 28, 2015

MEMBE AWATAKA WATANZANIA WASIKUBALI KUTISHWA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Bernard Membe akizungumza na umati wa wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliofika mjini Kigoma jana, kwa ajili ya kumdhamini ili aweze kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao kwa tiketi ya chama hicho.
WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, amesema Chama cha Mapinduzi (CCM) na Serikali yake, haviwezi kutishwa na mtu yeyote katika kutekeleza maamuzi yoyote kutokana na kuwa na historia ya kuwa na msimamo usioyumba na uongozi thabiti.
Membe ambaye ni miongoni mwa wana CCM waliotangaza nia ya kuwania urais kupitia chama hicho, amesema yeye binafsi hatokuwa na kinyongo kwa maamuzi yoyote yatakayochukuliwa na chama hicho hata ikiwa yatakuwa maamuzi machungu kwake.

Akizungumza na wanachama wa CCM wa mkoa wa Kigoma waliofika kumdhamini juzi Jumamosi, Membe amesema Watanzania wakatae vitisho na ulaghai kutoka kwa mtu yeyote katika maandalizi ya uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
“Watanzania tukatae aina yoyote ya vitisho wala ulaghai katika uchaguzi wetu. Sisi na wengine katika makundi yetu tutakaa kusubitri maamuzi sahihi ya chama chetu, ambacho hakikufanya makosa miaka yote ya nyuma…  Tutaheshimu maamuzi yatakayotoka Dodoma siku ile hata yangekuwa machungu kama pilipili. Na ole wao ama ole wake mtu yeyote atakayejitia kuletaleta bughudha pale eti kwa kisingizio kwamba eti chama hakikuchukua hatua sahihi, mtachukua hatua sahihi maana muna uzoefu wa kufanya hivyo.

“Nataka kuwambia Dodoma wajumbe wa Mkutano Mkuu ni watu makini sana na wewe (akimuelekeza kiongozi wa CCM Kigoma), mwaka 2012 tulipochagua wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, wajumbe walimuangalia mtu usoni na kumuuliza maswali, mtu anaposema Fulani asichaguliwe, unamuuliza kwanini asichaguliwe (sauti ikasikika ikisema “tulipambana sana”) walisema Fulani mchagueni na Fulani usimchague, wajumbe walihoji kama wewe unakuja na hela mifuko miwili, mmoja unasema mchague huyu na mwingine usimchague Fulani, lakini mulihoji kwanini na kusema huyu si mwenzetu.
“Ndugu zangu Watanzania kataeni upuuzi wa aina hiyo, angalieni vigezo mukiangalia familia zenu kwamba na kuhoji kama nikimpa huyu kesho nitakuwa salama!” Alisema Membe huku akishangiliwa na wana CCM waliokuwapo   utoka kwa yeyote  mkoani Kigoma
Alisema ni wajibu wana CCM kumpa kiongozi ambaye wakiangalia watakuwa na imani kwamba nchi na familia zao  zitakuwa salama na heshima na amani ya nchi itakuwa katika mikono salama na si vinginevyo.
Akizungumzia kuhusu maendeleo ya Kigoma alikomalizia mkoa wa 31, Membe alisema ataimarisha miundombinu ya reli na barabara na kuwasaidia kupata mwekezaji atakeyefanikisha mpango huo.
Alisema kampuni moja ya Kichina imeonyesha nia ya kuboresha huduma ya reli ikiwa ni pamoja na kujenga reli ya kisasa kati ya Dar es Salaam na Kigoma ambayo itawezesha safari ya siku moja.
Membe ambaye amekuwa akiahidi kusimamia uchumi wa viwanda unaotegemea kilimo, alisema viongozi waliotangulia akiwamo maraisi Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na sasa Jakaya Kikwete, wameweka misingi imara katika maenndeleo, na hivyo itakuwa ni rahisi kwake kuendeleza walipoishia.
Jana alipokua Sumbawanga na Mpanda, alimsifia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye alisema ni mmoja wa watangaza nia mwenye sifa za kuwa kiongozi wa nchi kutokana na historia yake ya uadilifu ndani na nje ya serikali na kwamba ingekuwa si mwanasiasa huyo angekwisha kujiona mteule ndani ya CCM.

No comments: