Tuesday, September 15, 2015

Tizama Ratiba ya Mechi za ligi kuu Tanzania Bara Kesho


Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara inatarajiwa kuendelea kesho jumatano katika viwanja saba nchini, huku timu 14 zikitarajiwa kuchuana kusaka pointi tatu muhimu katika michezo hiyo ya mzunguko wa pili.

Mabingwa watetezi wa kombe hilo klabu ya Young Africans watakuwa wenyeji wa Tanzania Prisons katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, huku Maafande wa Mgambo Shooting wakiwa wenyeji wa Simba SC katika dimba la uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Wana Lizombe Majimaji ya mjini Songea watawakaribisha wakata miwa wa Kagera Sugar katika uwanja wa Majimaji mkoani Ruvuma, jijini Mbeya watoza kodi wa jiji timu ya Mbeya City Council FC watawakaribisha maafande wa Jeshi la Kujenga Taifa JKT Ruvu katika uwanja wa Sokoine jijini humo.
Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, Stand United watakuwa wenyeji wa timu ya Azam FC, Toto Africans watawakaribisha wakata miwa wa Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa CCM Kirumba na Ndanda FC watakuwa wenyeji wa Coastal Union kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona.
Ligi hiyo itaendelea siku ya alhamis kwa mchezo mmoja tu kwa Wachimba Almasi wa mkoa wa Shinyanga, Mwadui FC watakapowakaribisha African Sports ya jijin Tanga katika mchezo utakaochezwa kwenye uwanja wa Mwadui.

No comments: