Tuesday, October 13, 2015

Fastjet, Emirates waingia makubaliano ya kibiashara


Katika hatua ya kuhakikisha kuwa wateja wake wanaunganishwa na usafiri wa kimataifa, kampuni ya ndege ya kiafrika yenye gharama nafuu Fastjet Tanzania imesaini makubaliano ya ushirikiano na shirika kubwa la ndege la Kimataifa Emirates.


Kupitia makubaliano hayo  ambayo yanaanza rasmi Oktoba 15, 2015, Emirates kwa upande mwingine watanufaika kutokana na abiria wake kuweza kufikia mtandao wa njia wa Fastjet ambao unakua ndani katika eneo la Mashariki na Kusini mwa Afrika.

Akitangaza kusainiwa nkwa makubaliano hayo, meneja mkuu wa Fastjet Afrika Mashariki, Jimmy Kibati alisema kuwa abiria wa Emirates  hivi sasa wataweza kukata tiketi za Fastjet  kutoka kwenye mitandao yote  ya Emirates  kwa kutumia mtandao wa kompyuta  uliounganishwa  baina ya mashirika hayo mawili.
Kibati alisema, “Tunayo furaha kubwa kufanya kazi na shirika la ndege linaloheshimika na lenye mafanikio duniani. Sio tu kwamba  hali hiyo itatuwezesha sisi kuwafikia mamilioni ya abiria ambao husafiri na Emirates bali pia ni uthibitisho mkubwa wa uendeshaji wetu makini, ubora wa huduma na  bei zetu nafuu. Tunatarajia  kusalimiana na abiria wa Emirates watakaokuwa wamepakia kwenye ndege zetu.”
 
Kibati aliongeza, “ubia wetu utaenda mbali  kutunufaisha  sote Fastjet na Emirates na kutuhakikishia usafirishaji mkubwa wa abiria na utawapa wasafiri ndani ya Afrika  fursa ya kuunganika na sehemu nyingine ulimwenguni kupitia kituo kikuu cha Emirates cha Dubai, ambapo Fastjet itaingiza abiria kituoni hapo kutoka miji na majiji ya Afrika.
 
Emirates ni shirika kubwa la ndege la kimataifa lenye makao yake makuu Dubai katika Himaya za Muungano wa Imarati. Hivi sasa Emirates linafanya safari hadi kwenye vituo 140 duniani vikiwemo 20 ndani ya Afrika, wakati Fastjet ni kampuni ya ndege inayoongoza ya kiafrika inayokuwa kwa kasi na yenye gharama nafuu.

No comments: