Tuesday, October 27, 2015

TAARIFA TATU KUTOKA TFF LEO


Kocha Mkuu wa timu ya Taifa Tanzania (Taifa Stars) inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager, Charles Boniface Mkwasa leo ametangaza kikosi cha wachezaji 28 watakoingia kambini Jumapili jioni kujiandaa na mchezo dhidi ya Algeria Novemba 14 jijini Dar es salaam, na marudiano kufanyika Novemba 17 nchini Algeria.
Akiongea na waandishi wa habari katika hoteli ya Serena jijini Dar es salaam, Mkwasa amesema kikosi chake hicho kitaweka kambi nchini Omani kwa takribani siku 10 kujiandaa na mchezo kuwania kufuzu kwa hatua ya makundi ya Kombe la Dunia nchini Urusi mwaka 2018 dhidi ya Algeria.
Katika kikosi hicho, Mkwasa amewaita wachezaji wapya sita wakiwemo Salim Mbonde, Jonas Mkude, Salum Abubakar, Malimi Busungu, Ramadhani Kessy na Malimi Busungu na kufanya idadi ya wachezaji 28.
Wachezaji aliowaita ni Magolikipa ni Ally Mustafa (Yanga), Aishi Manula (Azam), Said Mohamed (Mtibwa Sugar), walinzi wa pembeni Kessy Ramadhani, Mohamed Hussein (Simba), Juma Abdul, Haji Mwinyi (Yanga) na Shomari Kapombe (Azam), Walinzi wa kati ni Salim Mbonde (Mtibwa Sugar), Hassan Isihaka (Simba), Kelvin Yondani na nahodha Nadir Haroub (Yanga).
Viungo ni Salum Telela (Yanga), Salum Abubakar, Himid Mao, Mudathir Yahya, Frank Domayo (Azam), Jonas Mkude na Said Ndemla (Simba), washambuliaji wa pembeni Farid Musa (Azam), Saimon Msuva (Yanga) na Mrisho Ngasa (Free State Stars – Afrika Kusini).
Washambuliaji wa kati ni John Bocco (Azam), Elias Maguri (Stand United), Ibrahim Hajibu (Simba), Malimi Busungu (Yanga), Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe – Congo DR).

Ligi Kuu ya Vodacom inatarajiwa kuendelea kesho kwa michezo sita kuchezwa katika viwanja mbalimbali, ikiwa inaingia katika raundi ya tisa huku kila timu ikisaka ushindi wa pointi tatu muhimu.
Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, Simba SC watawakaribisha Coastal Union kutoka jijini Tanga, mchezo utakaonza majira ya saa 10:30 jioni, huku Ndanda FC wakiwa wenyeji wa Stand United uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.
Wachimba Almasi wa Mwadui FC watawakaribisha Yanga SC katika uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, Toto African watakua wenyeji wa maafande wa Mgambo Shooting katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Wakata miwa wa Turiani, Mtibwa Sugar watakua wenyeji wa Kagera Sugar katika uwanja wa Manungu Complex mkoani Morogoro, huku watoza ushuru wa jiji la Mbeya katika uwanja wa Sokoine Mbeya City watakua wenyeji wa Majimaji kutoka mkoani Ruvuma.
Ligi hiyo itaendelea siku ya Alhamis kwa michezo miwili kuchezwa, Tanzania Prisons watakua wenyeji wa African Sports katika uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, JKT Ruvu watakua wenyeji wa Azam FC katika uwanja wa Karume jijini Dar es salaam.

Timu ya Taifa Tanzania ya Wanawake ya Mpira wa Miguu (Twiga Stars) inatarajiwa kucheza mchezo wa kirafiki na timu ya Taifa ya Wanawake ya Malawi Novemba 7, 2015 jijini Dar es salaam.
Mchezo huo wa kirafiki ni sehmu ya kujipima kwa Twiga Stars inayonolewa na kocha Rogasian Kaijage, ambayo ilishiriki Fainali za Michezo ya Afrika (All Africa Games) mwezi Agosti – Septemba nchini Congo – Brazzavile.
Awali Twiga Stars ilikua icheze mchezo huo nchini Malawi Oktoba 24, kabla ya chama cha soka nchini humo (FAM) kuahirisha mchezo huo, na sasa mchezo huo utacheza nchini Tanzania Novemba 07, 2015.

No comments: