Saturday, November 28, 2015

AMOS MAKALLA APIGA MARUFUKU LIKIZO ZA MA DC, WAKURUGENZI NA WAKUU WA IDARA MKOANI KILIMANJARO


Na Mwandishi Wetu, Kilimanjaro
KATIKA hali inayoonyesha ni joto kali la kuwatumikia Watanzania, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla, amepiga marufuku likizo za Wakuu wa wilaya, Wakurugenzi na Wakuu wa Idara kwenye mkoa wake ili kutekeleza kwa vitendo hotuba na maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr John Pombe Magufuli.

RC Makalla aliyasema hayo juzi katika kikao cha kazi na wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri, wakuu wa idara wa halmashauri na Kamati ya Ulinzi na usalama ya mkoa huo kwa ajili ya kupeana mikakati ya majukumu ya kuwatumikia Wana Kilimanjaro na Watanzania kwa ujumla, ikiwa ni hatua nzuri ya kwenda na kasi ya Dr Magufuli.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla, akizungumza na Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na Wakuu wa Idara katika Mkoa huo ili kujipanga katika majukumu mbalimbali ya kuwatumikia wana Kilimanjaro na Watanzania kwa ujumla. Picha na Mpiga Picha Wetu.
Baadhi ya watendaji wa Mkoa Kilimanjaro wakimsikiliza kwa makini Mkuu wa Mkoa huo, Aamos Makalla alipozungumza nao jana. Katika kikao hicho, RC Makalla alipiga marufuku likizo kwa Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na Wakuu wa Idara ili kujipanga na maagizo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr John Pombe Magufuli.

Alisema kuwa Dr Magufuli ameagiza mambo mengi mazuri na yenye kuhitaji utendaji uliotukuka, ikiwamo elimu bure, mikakati ya kubana matumizi, kupambana na maradhi mbalimbali, ugonjwa wa kipindupindu, usimamizi wa pembejeo na kuzuia pia matukio mbalimbali yenye kugharimu pesa, sanjari na mapambano ya dawa za kulevya na uwadijibikaji kazini.

“Hakuna muda wa kupoteza katika kufanyia kazi maagizo ya rais Magufuli, hivyo sote kwa pamoja tunapaswa kujipanga na kwenda na kasi ya serikali yetu ili kuhakikisha kwamba nchi yetu inapiga hatua kubwa kama yalivyokuwa makusudio yetu ya kuhakikisha watoto wanasoma bure, hivyo sitaki kusikia likizo kutoka kwa Ma DC, Wakurugenzi na Wakuu wa Idara katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro. “Suala la kubana matumizi, pembejeo kwa wakulima, vita ya madawa ya kulevya na mengineyo yanapaswa kuanza sasa, huku tukihakikisha kwamba maadhimisho ya siku ya Uhuru yanajikita zaidi kwenye suala zima la usafi kuanzia kaya, mtaa au kijiji na kwingineko,” Alisema Makalla.

Katika hatua nyingine, RC Makalla alionyesha kukerwa na ugonjwa wa kipindu kipindu na kusema kuwa kamwe hataki kuona ugonjwa huo unaingia kwenye Mkoa wake wa Kilimanjaro, akiwataka wataalamu wa afya na watendaji wa serikali kujipanga kikamilifu.

Kwa mujibu wa Makalla, endapo watajipanga imara katika suala zima la usafi, usimamizi wa rasilimali na utendaji uliotukuka katika maeneo yao, Mkoa huo utazidi kupiga hatua kubwa kiuchumi, hivyo kufanikisha kwa vitendo dhamira kubwa ya Dr Magufuli ya kuwakwamua wananchi wake na Watanzania kwa ujumla. RC Makalla ni miongoni mwa viongozi wa juu wanaopambana kwenda na kasi ya Rais Magufuli, ikiwa ni siku chache tangu alipoapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, huku wananchi wengi wakionyesha kuwa na Imani kubwa na rais huyo wa awamu ya tano

No comments: