Thursday, December 24, 2015

STARTIMES LEAGUE SASA LIVE


Ligi Daraja la Kwanza nchini (StarTimes First Division League) mzunguko wa pili unaanza kutimua vumbi siku ya Jumamosi katika viwanja tisa mbalilimbali, huku michezo ya ligi hiyo ikianza kuonyeshwa moja kwa moja na kampuni ya Sahara Media kupitia kituo chake cha luninga cha StarTV.

Akiongea na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa mikutano wa TFF, Meneja Masoko wa kampuni ya StarTimes Tanzania, Damien Li amesema anashukuru michezo ya Ligi Daraja la Kwanza inaanza kuonekana moja kwa moja kwenye luninga.

Damien alisema StarTimes wanafarijika kuwa wadhamini wa kwanza kabisa wa ligi  wa daraja la kwanza nchini tangu kuanzishwa kwake, na sasa wanaviomba vilabu vyote vinavoshiriki ligi hiyo kutumia nafasi hiyo kujitangaza ndani na nje pamoja na wachezaji wao.
StarTimes ilingia udhamini wa Ligi Daraja la Kwanza wenye thamani ya milioni 900 (mia tisa) za kitanzania kwa kipindi cha miaka mitatu, huku kituo cha StarTV kikiongeza milioni 450 (mia nne hamsini) na kufanya udhamini huo kwa jumla kuwa ni bilioni 1.25 kwa kipindi cha miaka mitatu.
StarTv wataanza kuonyesha moja kwa moja mchezo wa Jumamosi, Disemba 26 kati ya Friends Rangers dhidi ya Polisi Dar mchezo utakaochezwa uwanja wa Karume, huku Jumapili Disemba 27 wakionyesha moja kwa moja mchezo kati ya Kiluvya United hidi ya Ashanti United Uwanja wa Karume jijini Dar es salaam.
Naye Afisa Habari wa TFF, Baraka Kizuguto, amevitaka vilabu vya Ligi Daraja la Kwanza kuitumia vizuri nafasi hiyo kujitangaza kimataifa, kwa kuheshimu taratibu na kanuni zinaondesha ligi hiyo.
Kizuguto amesema ligi hiyo itakuwa ikirushwa moja kwa moja na kampuni ya Sahara Media kupitia kituo chake cha StarTV, ambapo zaidi ya nchi 50 barani Afrika na Asia watapata nafasi ya kushuhudia michezo hiyo.

No comments: