Saturday, January 30, 2016

Picha --Majangili watungua Helkopta ya Doria serengeti na kuua rubani

 Watu wanaodaiwa kuwa ni majangili na wawindaji haramu wameitungua kwa risasi helkopta ya doria ya wanyamapori katika pori la akiba la maswa lililoko wilaya ya Meatu mkoani Simiyu kusini mwa hifadhi ya taifa ya Serengeti na kumuua rubani wa helkopita na kumjeruhi askari mmoja wa wanayamapori.

Kufuatia tukio hilo, waziri wa maliasili na utalii Profesa Jumanne Maghembe amefika katika eneo la tukio na kusisitiza kwamba serikali kwa kushirikiana na vyombo vyote vya dola na vyombo vya ulinzi na usalama inaanzisha mkakati mpya wa kupambana na ujangili na uwindaji haramu wa maliasili ikiwemo Tembo ambao ni rasilimali muhimu kwa taifa na kwa uhifadhi wa taifa la Tanzania.

Waziri Maghembe ambae amefika kwenye eneo hilo ilipotunguliwa helkopita hiyo katika safari iliyokuwa na msukosuko mingi ya barabara na hasa kipindi hiki cha mvua na kuikuta helkopita iliyokuwa inarushwa na kepten Roger Gower raia wa Uingereza ambae alifariki baada ya kujeruhiwa kwa risasi amesema tukio hilo limewakera wadau wote wa uhifadhi na serikali kwa ujumla na kamwe haliwezi kuachwa lipite bila hatua madhubuti kuchukuliwa huku akiwaonya baadhi ya watumishi wa serikali na askari wa wanyamapori wanaoshirikiana na wahalifu kuwa sasa kiama chao kimefika.

Nae kamanda wa upelelezi wa mkoa wa Simiyu Jonathan Shana amesema tukio hilo lilitokea jana jioni wakati helkopita hiyo ikiwa katika doria baada ya kusikika milio ya risasi ya majangili katika pori hilo ambapo Tembo watatu waliuwawa na kwamba watu watatu wanashikiliwa na polisi wakihojiwa kufuatia tukio hilo ambapo mkurugenzi mkuu shirika la hifadhi za taifa Tanzania Tanapa Allan Kijazi amesisistiza umuhimu wa wadau kuongeza nguvu katika kukabiliana na matatizo ya ujangili nchini.

No comments: