Uongozi wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) umezuia mahafali ya wanafunzi  waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT ) yaliyokuwa yamepangwa kufanyika jana mchana chuoni hapo jijini Dar es Salaam, ambapo Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa alikuwa amealikwa na wanafunzi kama mgeni rasmi.
Mahafali hayo yalizuiwa jana saa 6 mchana ikiwa ni saa mbili kabla ya muda kuanza
Tangazo lililobandikwa chuoni hapo na kushuhudiwa na wanahabari likiwa linamnukuu Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Apollinary Kamuhabwa liliwataka wanafunzi hao kutoweka mikusanyiko ya aina yoyote chuoni hapo.
Profesa Kamuhabwa kupitia tangazo hilo aliwaonya wanafunzi hao kutojihusisha na masuala ya siasa wawapo chuoni kama ilivyo kwa watumishi wa umma.
Jitihada za waandishi wa habari kuzungumza na uongozi wa chuo hicho ili kupata ufafanuzi ziligonga mwamba baada ya kuelezwa kuwa hawakualika mkutano na waandishi wa habari.