Friday, September 23, 2016

MEYA WA DAR ISAYA NWITA ASHAURI WATANZANIA KUJENGA UTAMADUNI WA KUTUMIA BIDHAA ZA NGOZI ZA HAPA NCHINI

Meya wa Jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita akipata maelekezo kwa Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Kemange iliyopo Buhemba Wilayani Tarime Mkoani Mara kwenye darasa ambalo alisoma. Shule hiyo inahitaji ukarabati wa vyumba 9 vya madarasa

NA MWANDISHI WETU, Musoma

MEYA wa Jiji la Dar es Salaam Isaya Mwita ameshauri kila halmashauri kusimamia kikamilifu namna ya kuwashawishi wananchi kujenga utamaduni wa kutumia bidhaa za ngozi ambazo zinazalishwa hapa nchini ili kuongeza pato la taifa sambamba na kujiajiri wenyewe.

Meya Isaya alitoa kauli hiyo mjini hapa jana wakati alipotembelea Banda la Mamlaka ya biashara Tanzania Tan Tred ambapo alisema kwamba bila kutumia ushawishi kwa wananchi kutumia bidhaa za ndani, nchi itaendelea kubaki masikini kutokana na watu kukosa ajira.

Aidha alisema bidhaa za ndani hususani za ngozi zinaweza kuzaa matunda iwapo tu wananchi wenyewe , viongozi wakajenga utamaduni wa kutumia bidhaa za ndani na hivyo kupata nafasi kubwa ya kuzitangaza katika masoko ya nje ya nchi hii.

" Viongozi tunasafiri tunaenda nchi mbalimbali , kama tukiamua kutangaza bidhaa zetu wenyewe huko tunakokwenda , tunapata soko la kitaifa , na hata viongozi wa nchi hizo wakija wanakuwa wa kwanza kuziulizia" alisema Meya Isaya.

Aliongeza kwamba Tanzania ina rasilimali nyingi za kutosha ambazo zinaweza kuwapatia ajira vijana lakini changamoto kubwa inatokana na wananchi wenyewe kuamini bidhaa zinazo zalishwa nje badala ya zile zinazo zalishwa na wazawa.

" Sisi ndio tunakutaka na wananchi muda wote, kwa nafasi zetu tunauwezo mkubwa wa kuhakikisha kwamba bidhaa hususani hizi za ngozi zinapata soko kubwa kulingana na idadi ya wakazi ambao wapo kwenye maeneo tunayo toka, na haya sasa ndio maendeleo ambayo kama viongozi wa makini, Kata tunatakiwa kufanya" alisema Isaya.

"Ndani ya jiji langu,hili hili la bidhaa za ndani nitalipa kipaumbele ikiwa ni pamoja na kukutana na wajasiriamali wa bidhaa mbalimbali , nakuona ni kwa namna gani tunawajengea uwezo wananchi kuzipenda na kuanza kuzitumia.

Alisema kama viongozi wa halmashauri watatumia nafasi zao kuwaelimisha wananchi juu ya suala zima la ujasiriamali changamoto ya umasikini itapungua kutokana na kwamba wengi watajiajiri wenyewe na hivyo kujipatia kipato.

Alisema Wakati umefika wa watanzania kutumia bidhaa za ndani kama ilivyo kwenye nchi nyingine ambazo zimekuwa zikijipatia kipato kikubwa kupitia wajasiriamali wa bidhaa mbalimbali ambazo zinazalishwa na wajasiriamali hao.

No comments: