Sunday, October 2, 2016

WAKULIMA WA KOROSHO WALIA NA SERIKALI KUHUSU MALIPO YAO

http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/1850408/highRes/511359/-/maxw/600/-/1045rlfz/-/wakulima.jpg

 Wakati msimu mpya wa korosho 2016/17 kufunguliwa rasmi Septemba mosi mwaka huu bado baadhi ya wakulima wameendelea kulalamika kutolipwa malipo yao ya korosho kwa msimu uliopita 2015/16.

Wakizungumza katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na mbunge wa jimbo la Ndanda,Cecil Mwambe katika kata ya Chikukwe kwaajili ya kuwashukuru wapiga kura wake baadhi ya wakulima walidai kuwa bado wanadai malipo yao ya tatu kwa msimu uliopita hali inayowavunja moyo.
Akiuliza swali Hashim Abdullah alidai msimu mpya wa ununuzi wa korosho umeanza rasmi lakini bado hawajalipwa pesa zao hali inayowatia hofu.


"Tunataka kufahamu tunapokuwa na matatizo yetu tuyawasilishe wapi , kuna matatizo mengine hatujui pa kuyapeleka mfano malipo ya tatu ya korosho kwa msimu uliopita mpaka sasa kuna watu ambao bado hawajalipwa na hawajui hatima yao na msimu mpya umeanza tayari tunapata hofu je zitalipwa kwasababu bodi nyingine za vyama vyama msingi zilivunjwa ,"alihoji Abdullah
Akizungumzia madai hayo mbunge wa jimbo la Ndanda, Cecil Mwambe alisema madai ya baadhi ya wakulima kutolipwa malipo yao anayafahamu na kwasasa unafanyika ukanguzi ili watakaobainika kudhulumu pesa za wakulima waweze kuchukuliwa hatua.

"Haya madai yapo hata waziri alipokuja aliagiza wakulima walipwe haki zao, na haikuishia hapo aliagiza ufanyike ukaguzi katika vyama vyote vya msingi na wale watakaobainika kudhulumu jasho la mkulima wachukuliwe hatua,"alisema Mwambe

Hata  hivyo alimtaka rais kuichukulia hatua bodi ya korosho nchini  (Cbt) kwa kile alichiokidai ni kuwa na matumizi mabaya ya ofisi na kuomba wafanyiwe ukaguzi wa mahesabu.

"Kama bodi ya korosho ingekuwa inatekeleza majukumu yake ipasavyo hata malalamiko ya wakulima yangepungua lakini bodi ambayo iliundwa kwa lengo la kusaidia wakulima wanajijali wao zaidi kuliko mkulima ambaye amesababisha iundwe..haiwezekani wakulima mpaka leo wanadai madai yao ya miaka ya nyuma lakini bodi wanakaa vikao vya wadau wa korosho na kulipana 1.5 milioni kama posho, "alisema Mwambe

Aidha alisema viwanda vingi vya kubangulia korosho vimeuzwa kwa watu wanaovitumia kama maghala ya kuhifadhia mazao hasa korosho jambo ambalo linakosesha ajira.
Naye kaimu mtendaji wa chama cha msingi Chamwali,Omary Mkudile alipotakiwa kueleza juu ya uwepo wa madai ya wakulima katika chama chake alikiri ni kweli chama chake kinadaiwa pesa za wakulima kiasi cha 51 milioni zikiwa ni malipo ya tatu.

"Ni kweli katika chama chetu bado tunadaiwa kiasi cha Sh 51 milioni ambazo ni malipo ya tatu ya wakulima kwa msimu wa mwaka 2015/16 ,"alisema Mkudile
Hivi karibuni naibu waziri wa kilimo, Uvuvi na Mifugo,William Ole Nasha alifanya ziara katika wilaya ya Masasi na kueleza kuwa pesa za wakulima zaidi ya Sh 4 bilioni zimepotea huku asilimia hamsini ya pesa hizo zikiwa ni za wilaya ya Masasi pekee.

No comments: