Saturday, December 24, 2016

MBOWE AVUNJA UKIMYA KUHUSU KUPOTEA KWA BEN SAANANE

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema amekuwa kimya muda mrefu kuhusiana na kupotea katika mazingira ya kutatanisha, msaidizi wake Ben Saanane kwa kuwa suala hilo lipo kwenye uchunguzi. 

Mbowe alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Mbeya wakati wa uchaguzi wa viongozi wa chama hicho Kanda ya Nyasa inayojumuisha mikoa ya Iringa, Mbeya, Songwe, Njombe na Rukwa. 

Alisema yeye pia ameathiriwa na tukio hilo kama ilivyo kwa wazazi wake na ndugu wengine kwa kuwa ni mtu muhimu kwake katika kutekeleza majukumu yake. 

“Ndugu zangu Watanzania msione nipo kimya, nimefanya hivi kutokana na kuwa suala hili lipo kwenye uchunguzi kwani tukizidisha kuongea ongea wale ambao wamemteka wanaweza kupoteza uhai wake kisa maneno,” alisema Mbowe. 

Alisema, “Chadema ni taasisi ambayo ina vyombo vya ulinzi na usalama ambavyo vinaendelea kuchunguza tukio hili la aina yake.” 

Katika hatua nyingine, Mbowe aliishitumu Serikali akidai kwamba imeendelea kuwafunga wanachama wake na kwamba mpaka sasa 180 wapo mahabusu. Alisema hizo ni jitihada za kuua nguvu za upinzani. 

Akijibu madai hayo, Kamishna wa Polisi (Operesheni na Mafunzo), Nsato Marijani alisema jeshi hilo linawashikilia watu wengi kwa makosa mbalimbali vituoni na wengine mahabusu katika magereza. Alisema polisi haimkamati mfuasi wa chama cha siasa bali mtu anayekwenda kinyume cha sheria. 

“Hayo yanayosemwa siyo ya kweli, waache kulipaka tope jeshi la polisi. Tutaendelea kuwakamata watu wote wanaovunja sheria. Hata kama akiwa mjomba wangu tutamkamata.” 

Msigwa kidedea 
Katika uchaguzi huo, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa aliibuka kidedea baada ya kushinda kwa kupata kura za ndiyo 62 sawa na asilimia 58.49 kati ya kura 106 zilizopigwa. 

Akitangaza matokeo hayo, msimamizi wa uchaguzi huo Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Bara), John Mnyika alisema nafasi ya makamu mwenyekiti imechukuliwa na Sadrick Malila ambaye alipata kura za ndiyo 93 sawa na asilimia 88 ya kura zilizopigwa 106 huku kura tatu zikiharibika. 

Mnyika alisema kuwa nafasi ya  mweka hazina imechukuliwa na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Mbeya, Sophia Mwakagenda ambaye alishinda kwa kupata kura 91 ambayo ni sawa na asilimia 86 kura zote 106 zilizopigwa. 

Mnyika alisema katika uchaguzi huo wajumbe walipiga kura za ndiyo au hapana kwa lengo la kufanya uchaguzi wa maridhiano kwani uchaguzi wa kuweka wagombea wawili husababisha makundi na kuleta migogoro ndani ya chama. 

“Hivyo Kamati Kuu Taifa baada ya kuliona hilo tukaamua kuwaita wagombea wote na kuwaeleza nia yetu ya kufanya hivyo na hatujafanya huku tu, hata kanda nyingine tulizopita tumefanya hivyo" Alisema Mnyika

No comments: