Tuesday, February 21, 2017

Serikali yaweka sawa Utaratibu wa kufuta Viroba nchini


Kufuatia kauli ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa aliyotoa tarehe 16/02/2017 huko Mererani, Mkoani  Manyara kuhusu kusitisha utengenezaji, uuzaji na matumizi ya pombe zinazofungashwa kwenye vifungashio vya plastiki kuanzia tarehe 1 Machi 2017; na kufuatia  Tamko la Serikali kuhusu dhamira hiyo lililotolewa Bungeni tarehe 2 Mei, 2016 na kwenye matangazo yaliyotolewa kwenye vyombo vya habari tarehe 01 Desemba, 2016, Ofisi ya Makamu wa Rais  inachukua fursa hii kutangaza utaratibu wa utekelezaji wa maamuzi hayo ya Serikali.

  • Waziri mwenye dhamana ya Mazingira atatunga Kanuni zitakazodhibiti uzalishaji wa vifungashio (viroba) vya pombe kali, kwa mujibu wa Kifungu 230 (2) (F) cha Sheria ya Mazingira ya  Kanuni hizi  zitaweka sharti la kutaka pombe kali inayozalishwa viwandani zifungashwe kwenye chupa zinazoweza kurejelezwa (recycled) na kwa ujazo usiopungua milligram 250.
Pia Kanuni hizo zitapiga marufuku uzalishaji, uuzaji, uingizaji nchini na matumizi  pombe  zilizofungwa kwenye viroba na mitambo ya malighafi ya vifungashio vya plastiki (viroba) vitakavyotumika kufungashia pombe kali.   Atakayebainika kukiuka masharti ya Kanuni hizi atawajibishwa kulipa faini, kufungwa jela au vyote kwa pamoja kama itakavyoainishwa kwenye Kanuni.
  • Dhamira ya Serikali sio kupiga marufuku vinywaji vya pombe kali bali ni kutekeleza Ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 ambayo inatoa haki ya kuishi katika mazingira yaliyo safi, salama na yenye afya. Haki hiyo pia imetiliwa mkazo katika sheria ya Mazingira ya 2004.  Hivyo, dhamira  ya Serikali ni kudhibiti upatikanaji kwa urahisi wa pombe kali kunakotokana na kufungwa katika plastiki na kwa ujazo mdogo, kunakopelekea kuongezeka kwa matumizi ya pombe kali hadi kwa watoto wadogo; kudhibiti uchafuzi wa mazingira unaotokana na kuzagaa kwa vifungashio hivyo; na kudhibiti ukwepaji mkubwa wa kodi kutokana na urahisi wa teknolojia na gharama za kutengeneza  pombe kali  inayofungashwa kwenye viroba. Inakadiriwa kwamba Serikali inapoteza shilingi bilioni 600 kwa mwaka kutokana na ukwepaji kodi kwenye biashara ya pombe za viroba.
  • Utekelezaji wa maamuzi haya ya Serikali unaanza mara moja. Ingawa haitegemewi, lakini iwapo kuna Wazalishaji watakaohitaji muda wa ziada wa kuhamia kwenye teknolojia ya chupa, wataomba kibali maalum cha muda mfupi ambacho hakitatolewa hadi muombaji awasilishe kabla ya tarehe 28/02/2017:- yafuatayo:-
  1. Ushahidi/Barua kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwamba amelipa kodi katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
  2. Ushahidi/Barua/Cheti kutoka Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kwamba mzalishaji amekuwa na  kibali cha usalama wa kinywaji kwa miaka yote ambayo amekuwa anazalisha;
  • Cheti au Barua kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kwamba mzalishaji  anauza bidhaa inayokidhi viwango
  1. Cheti cha Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA) au Ukaguzi wa Mazingira (EA) kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC)/Ofisi ya Makamu wa Rais;
  2. Ushahidi kwamba katika kipindi cha mpito mzalishaji atatumia teknolojia ya kudhibiti utengenezaji wa vifungashio bandia (anti-counterfeit technology);
  3. Uthibitisho kutoka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) kuhusu usajili wa kampuni na usajili wa chapa ya kinywaji (brand).
Zipo pombe za viroba zinazoingizwa nchini kutoka nje ya nchi, hasa kwenye Mikoa na Miji ya mipakani.  Wakuu wa Wilaya , kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya na Kamati za Mazingira, wanaelekezwa kufanya operesheni ya kukamata na kuzuia viroba vinavyoingizwa nchini kinyume cha utaratibu. Operesheni hii pia inahusu udhibiti wa pombe haramu ya gongo.
 
Serikali imeunda Kikosi Kazi cha Kitaifa kwa ajili ya kufanya ukaguzi na ufuatiliaji na hatua hizi.  Kikosi hicho kinajumuisha Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Fedha na Mipango,  Wizara ya Viwanda Biashara na Uwekezaji, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Mamlaka ya Kodi ya Mapato Tanzania (TRA), Idara ya Uhamiaji na Jeshi la Polisi.  Doria za ukaguzi  wa utekelezaji wa hatua hizi zitaanza wakati wowote kuanzia sasa na hatua kali zitachukuliwa kwa watakaokiuka.  Ofisi ya Makamu wa Rais itaratibu Kikosi hiki.
 
Kuhusu mifuko ya plastiki, Kanuni za Udhibiti zinaandaliwa na zuio litatangazwa wakati wowote.  Tunapenda kuwaasa wazalishaji, waagizaji na wauzaji  wa mifuko hiyo nao kujiandaa.
 
Hatua hizi za Serikali sio za ghafla au kushtukiza kwani taarifa ilitolewa Bungeni takribani mwaka mmoja sasa. Aidha Serikali ilitoa taarifa rasmi mwezi Agosti 2016 na Desemba 2016 kuhusu dhamira ya kuchukua hatua hizi.  Serikali ilitarajia kwamba wazalishaji wa pombe za viroba na mifuko ya plastiki watakuwa wamejiandaa kubadilisha teknolojia.
Ofisi ya Makamu wa Rais
20/02/2017

No comments: